10Mke mwema kweli, apatikana wapi?

Huyo ana thamani kuliko johari!

11Mumewe humwamini kwa moyo,

kwake atapata faida daima

12Kamwe hamtendei mumewe mabaya,

bali humtendea mema maisha yake yote.

13Hutafuta sufu na kitani,

na kufanya kazi kwa mikono yake kwa bidii.

14Yeye ni kama meli za biashara:

Huleta chakula chake kutoka mbali.

15Huamka kabla ya mapambazuko,

akaitayarishia jamaa yake chakula,

na kuwagawia kazi watumishi wake.

16Hufikiria kununua shamba, kisha hulinunua,

na kulima zabibu kwa faida ya jasho lake.

17Huwa tayari kufanya kazi kwa nguvu

na kuiimarisha mikono yake.

18Hutambua kwamba shughuli zake zina faida;

hufanya kazi hata usiku kwa mwanga wa taa yake.

19Husokota nyuzi kwa mikono yake mwenyewe,

kwa vidole vyake mwenyewe husuka nguo zake.

20Huufungua mkono wake kuwapa maskini,

hunyosha mkono kuwasaidia fukara.

21Hawahofii watu wake ijapo baridi ya kipupwe,

maana kila mmoja anazo nguo za kutosha.

22Hujitengenezea matandiko,

mavazi yake ni ya zambarau ya kitani safi.

23Mume wake ni mtu mashuhuri barazani,

anakoshiriki vikao vya wazee wa nchi.

24Mwanamke huyo hutengeneza nguo na kuziuza,

huwauzia wafanyabiashara mishipi.

25Nguvu na heshima ndizo sifa zake,

hucheka afikiriapo wakati ujao.

26Hufungua kinywa kunena kwa hekima,

huwashauri wengine kwa wema.

27Huchunguza yote yanayofanyika nyumbani mwake,

kamwe hakai bure hata kidogo.

28Watoto wake huamka na kumshukuru,

mumewe huimba sifa zake:

29Husema: “Wanawake wengi wametenda mambo ya ajabu,

lakini wewe umewashinda wote.”

30Madaha huhadaa na uzuri haufai,

bali mwanamke amchaye Mwenyezi Mungu atasifiwa.

31Jasho lake lastahili kulipwa,

shughuli zake hazina budi kuheshimiwa popote.

  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Methali 31:10-31
  • Imechapishwa: 15/01/2020