Swali: Mawaidha ya maimamu na kule kuwakumbusha kwao watu katika mbasaba wa mwaka mpya wa Hijr na nasaha zao ambapo wanawaambia watu wazihesabu nafsi zao na kwamba wamshukuru Allaah kuudiriki mwaka mpya na kwamba mbora wa watu ni yule ambaye umerefuka uhai wake na yakawa mazuri matendo yake kunahesabika ni katika Bid´ah? Kwa sababu haikuzoeleka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwamba alikuwa akifanya hivo mwanzoni mwa kila mwaka.

Jibu: Hii sio Bid´ah. Huku ni kukumbushana kwa minasaba kwa minajili ya kuwasisitiza watu na kuwabainishia kwamba wanatakiwa kuupokea mwaka wao kwa kufanya bidii na juhudi, ´ibaadah, kulingania kwa Allaah (´Azza wa Jall), matangamano mazuri na mfano wa hayo. Huu ni mnasaba.

Ama kusema kwamba ni jambo halikuzoeleka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni kweli. Kwa sababu kalenda hii haikuwekwa isipokuwa baada ya kufa kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na baada ya kufa Abu Bakr (Radhiya Allaahu ´anh). Ni jambo halikujulikana isipokuwa katika zama za  ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh) wakati alipokuwa akiandika barua mbalimbali kwenda kwa viongozi wenzake. Wakati barua zinawafikia wanakuwa si wenye kujua ni lini kiongozi wa waumini aliiandika na wakawa wamemuomba aandike tarehe. Hapo ndipo akaweka kalenda katikati ya uongozi wake (Radhiya Allaahu ´anh).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Liqaa’ ash-Shahriy (35) http://binothaimeen.net/content/783
  • Imechapishwa: 18/01/2018