Swali: Ni kiwango gani mwanamke anaweza kujifunua mbele ya wanaume maharimu wake? Je, inajuzu kufunua mpaka kwenye nusu ya mkono? Vilevile kifua kabla ya matiti? Vipi inafaa vilevile kuonyesha mwanzoni mwa kifua? Vipi kuhusu wasichana kuvaa nguo fupi? Ni yepi katika hayo yaliyotangulia yanayofaa kuyaonyesha mbele ya wanawake na ni ipi hukumu vilevile kumuonyesha mwanamke daktari au muuguzi wa kikafiri?

Jibu: Hili swali ni refu. Lakini sisi tunasema kuwa wanawake wa Maswahabah walikuwa wakivaa mavazi yenye kuwafunika kuanzia kwenye muundi mpaka kwenye vitanga vya mikono ilihali wako nyumbani. Ama nyumbani Hadiyth ya Umm Salamah (Radhiya Allaahu ´anhaa) imetambulisha kwamba wakati Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipomwambia: “Warefushe shibiri moja.” Akasema: “Ee Mtume wa Allaah! Nyayo zetu zitaonekana.” Akasema:

“Basi warefushe dhiraa moja na wala wasizidishe.”

Hii ni dalili inayofahamisha kuwa mwanamke anatakiwa kujifunika mpaka kwenye nyayo zake pindi anapotoka kwenda sokoni. Kuhusu akiwa nyumbani pamoja na wanawake wenzie, mambo ni mepesi. Mwanamke afunue kichwa chake, uso wake, vitanga vyake vya mikono na mikono yake. Hakuna neno. Lakini hata hivyo nguo yake ni lazima iwe pana. Mwanamke akiwa na nguo ilio pana na akafunua mikono yake kwa ajili ya kufanya kazi miongoni mwa kazi na pembezoni mwake wakawepo wanawake wengine au maharimu hakuna neno.

Lakini sisi haturuhusu mavazi mafupi kabisa. Kuna tofauti kati ya kuonyesha mikono, shongo, kichwa, kuacha wazi kichwa mpaka kwenye kifua na mfano wa hayo na kati ya mavazi kuwa mepesi, yenye kuonyesha, yenye kubana na mafupi. Mavazi haya dalili zimeonyesha kuwa ni haramu. Mtume (Swalla ´alayhi wa sallam) amesema:

“Kuna watu aina mbili wa Motoni sijawaona; wanaume walio na bakora kama mkia wa ng´ombe ambazo wanawapiga kwazo watu, na wanawake waliovaa vibaya, uchi, Maaylaat na Mumiylaat. Vichwa vyao ni kama nundu ya ngamia. Hawatoingia Peponi na wala hawatonusa harufu yake. Harufu yake inapatikana umbali wa kadhaa na kadhaa.”

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Liqaa’ ash-Shahriy (36) http://binothaimeen.net/content/814
  • Imechapishwa: 23/02/2018