Maswahabah wote wameritadi baada ya kufa Mtume

al-Kashshiy amepokea miongoni mwao – kwa mujibu wao huyu ndiye mtambuzi na mwaminifu zaidi wa hali za wapokezi – kutoka kwa Imaam Ja´far as-Swaadiyq (Radhiya Allaahu ´anh) – Allaah amemtakasa kutokamana na hayo – ya kwamba amesema:

“Pindi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipokufa Maswahabah wote walitoka katika Uislamu isipokuwa watu wanne; al-Miqdaad, Hudhayfah, Salmaan na Abu Dharr (Radhiya Allaahu ´anhum). Akaambiwa: “Vipi kuhusu hali ya ´Ammaar bin Yaasir?” Akasema: “Alifukuzwa kisha akarejea.”

Ujumla huu wenye kutiliwa mkazo unapelekea ´Aliy na watu wa familia ya Mtume (Swall Allaahu ´alayhi wa sallam) kuritadi, japo hawaonelei hivo. Huku ni kubomoa msingi wa dini. Msingi wake ni Qur-aan na Hadiyth. Tukichukulia kuwa wale waliopokea kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wameritadi isipokuwa watu wachache ambao maelezo yao hayafikii mapokezi yaliyopokelewa kwa njia nyingi (Mutawaatir), basi Qur-aan na Hadiyth vitatiliwa shaka. Tunajilinda kwa Allaah kutokamana na imani inayopelekea kuibomoa dini.

Wakanamungu wameyachukua maneno haya ya Raafidhwah kuwa ni hoja kwao na wakasema: “Vipi Allaah atasema:

كُنتُمْ خَيْرَ أُمَّةٍ أُخْرِجَتْ لِلنَّاسِ

“Mmekuwa Ummah bora kabisa uliotolewa kwa watu.” (03:110)

ilihali waliritadi wote baada ya kufa Mtume wao isipokuwa tu watu watano au wasita katika wao kwa sababu ya kumtanguliza kwao mbele Abu Bakr juu ya ´Aliy ambaye ndiye wasii?

Tazama maneno yaliyosemwa na mkanamungu huyu utaona kuwa yametokamana na Raafidhwah. Watu hawa wana madhara makubwa katika dini kuliko mayahudi na manaswara.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ar-Radd ´alaa ar-Raafidhwah, uk. 52-53
  • Imechapishwa: 23/04/2017