Swali: Tunataraji utatuwekea wazi maoni sahihi juu ya yule mwenye kuswali Maghrib nyuma ya ambaye anaswali ´Ishaa pamoja na kwamba kuna tofauti kwa vile ule muonekano wa wazi hauendani. Ni vipi mtu anaweza kujibu maneno ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Imamu amewekwa ili aweze kufuatwa. Hivyo msitofautiane naye.”?

Jibu: Swali lililoulizwa ni kama inafaa kwa mtu kuswali nyuma ya imamu ambaye wana nia tofauti; imamu anaswali ´Ishaa ambapo akaingia mswaliji anayeswali Maghrib. Katika hali hii nia ni zenye kutofautiana. Je, inajuzu kwake kujiunga naye pamoja na kwamba nia zinatofautiana? Ndio, inafaa. Kizuizi kiko wapi? Kitendo hichi hakitofautiani na maneno ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) pale aliposema:

“Imamu amewekwa ili aweze kufuatwa. Hivyo msitofautiane naye.”

Kwa sababu maneno haya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ameyafasiri kwa kusema:

“Akisema ´Allaahu Akbar` nanyi semeni “Allaahu Akbar” na akirukuu nanyi rukuuni.”

Ama kutofautiana kwa swalah zao ni jambo halidhuru. Kwa sababu mswaliji huyu akijiunga na imamu anayeswali ´Ishaa katika ile Rak´ah ya kwanza, swalah yake ya Maghrib inaisha pindi imamu anaposimama kwenda katika Rak´ah ya nne. Hapo anatakiwa kujitenga pamoja na imamu kwa yeye kunuia kujitenga, asome Tashahhud na akamilishe. Baada ya hapo ajiunge tena pamoja na imamu katika zile Rak´ah zilizobaki za ´Ishaa. Akiunga pamoja na imamu katika Rak´ah ya pili, katika hali hii atoe Tasliym pamoja naye na wala haimdhuru. Baadhi ya watu wanasema kwamba akijiunga pamoja naye katika Rak´ah ya pili, mswaliji huyu atakaa katika Rak´ah ya kwanza. Atakaa baada ya Rak´ah ya kwanza kwa sababu Rak´ah ya kwanza ya mswaliji huyu itakuwa ni Rak´ah ya pili kwa yule imamu. Vivyo hivyo imamu akisimama katika Rak´ah ya nne basi yeye atatakiwa kukaa kwa sababu yule anayeswali Maghrib hukaa katika Rak´ah ya tatu. Wanaona kuwa hatakiwi kukaa chini bali anatakiwa kumfuata imamu. Matokeo yake anakuwa amefanya Tashahhud mahali pasipokuwa kwenye Tashahhud na ameacha kufanya Tashahhud mahali ambapo ni pa Tashahhud. Tunasema kuwa tofauti hii haidhuru. Mnaonaje lau mtu atajiunga na imamu katika swalah ya Dhuhr kwa nia ya Dhuhr, lakini akajiunga naye katika Rak´ah ya pili. Je, muonekano wa swalah zao zitatofautiana au hapana? Zitatofautiana. Akijiunga pamoja na imamu kwa nia ya Dhuhr na imamu anaswali Dhuhr, lakini hata hivyo amejiunga naye katika Rak´ah ya pili, katika hali hii atafanya Tashahhud katika ile Rak´ah ya kwanza na kuacha kufanya Tashahhud katika Rak´ah ya pili na hatimaye afanye Tashahhud katika Rak´ah ya tatu. Haya hayadhuru. Hayadhuru yale aliyoyafanya yasiyokuwemo ndani ya swalah yake kwa sababu yeye ameamrishwa kumfuata imamu.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Liqaa´ ash-Shahriy (66) http://binothaimeen.net/content/1491
  • Imechapishwa: 02/02/2020