Maelezo ya Hadiyth “Mwenye kulingania katika uongofu basi ana ujira mfano wa ujira wa yule… “

Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kulingania katika uongofu basi ana ujira mfano wa ujira wa yule atakayemfuata. Hakupungui chochote kutoka kwenye ujira wao. Mwenye kulingania katika upotevu basi ana madhambi mfano wa madhambi ya yule atakayemfuata. Hakupungui chochote kutoka kwenye ujira wao.”

Ameipokea Muslim.

Hadiyth na mfano wake ndani yake kuna mahimizo ya kulingania katika uongofu, mambo ya kheri na fadhilah za mlinganizi. Sambamba na hilo kuna matahadharisho ya kulingania katika upotevu na upindaji na jirima kubwa ya yule mwenye kufanya hivo na adhabu yake.

Uongofu ni ile elimu yenye manufaa na matendo mema. Kila yule mwenye kufunza elimu au akawaelekeza wenye kujifunza juu ya kupita katika njia ambayo kwayo watapata elimu basi huyo amelingania katika uongofu.

Kila yule mwenye kulingania katika matendo mema yanayohusiana na haki ya Allaah au haki za watu wote kwa jumla au watu maalum basi huyo amelingania katika uongofu.

Kila yule ambaye ametoa nasaha ya kidini au ya kidunia inayomwelekeza mtu katika dini, basi huyo amelingania katika uongofu.

Kila yule ambaye wengine watamuiga katika elimu au matendo yake, basi huyo amelingania katika uongofu.

Kila yule ambaye atawatangulia wengine katika kufanya kheri au mradi wa kijumla na wenye manufaa, basi anaingia ndani ya andiko hili.

Mambo ni kinyume na hivo pia kuhusu yule ambaye analingania katika upotevu.

Wanaolingania katika uongofu ni wale maimamu wa wachaji Allaah. Wanaolingania katika upotevu ni wale maimamu wa wale ambao wanalingania kuelekea Motoni.

Kila yule mwenye kuwasaidia wengine katika wema na kumcha Allaah, basi ni katika wenye kulingania katika uongofu.

Kila yule mwenye kuwasaidia wengine katika madhambi na uadui, basi huyo ni katika wanaolingania katika upotevu.

  • Mhusika: ´Allaamah ´Abdur-Rahmaan bin Naaswir as-Sa´diy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bahjatu Quluub-il-Abraar, uk. 22-23
  • Imechapishwa: 26/01/2019