Maelezo kuhusu kukusanya na kufupisha kwa msafiri

Swali: Wiki iliopita katika barnamiji “Nuur ´alaa ad-Darb” uliulizwa swalah kuhusiana na kukusanya na kufupisha katika hali ya safari. Kuna ndugu mmoja ambaye alifahamu kuwa umefutu kwamba inafaa kukusanya kati ya Dhuhr na ´Aswr safarini japokuwa mtu atakuwa hana uzito wowote. Kwa msemo mwingine hata kama atafika katika mji ambapo anakwenda. Shaykh! Naomba kuwekewa wazi.

Jibu: Hili ni sahihi. Imeruhusiwa kufupisha safarini. Bali kufupisha ni jambo limesuniwa. Vilevile imeruhusiwa kukusanya. Ni mamoja mtu ametua sehemu au bado ni mwenye kuendelea na safari. Lakini akiwa bado ni mwenye kuendelea na safari basi kukusanya ndio Sunnah na ndio bora zaidi kuliko mtu kutokukusanya. Akiwa ametua sehemu basi kukusanya inafaa na sio Sunnah. Katika hali hiyo bora ni kutokukusanya isipokuwa wakati wa haja. Dalili ya hilo ni kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika vita vya Tabuuk alikuwa akiswali Dhuhr na ´Aswr hali ya kukusanya. Vilevile katika hajj ya kuaga alikuwa ni mwenye kutua Abtwaah nyuma kidogo ya Makkah. Abu Juhayfah ambaye ni Swahabah (Radhiya Allaahu ´anh) akataja kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alitoka siku hiyo akiwa na koti nyekundu ambapo akapewa bakora na akaswali Dhuhr Rak´ah mbili na ´Aswr Rak´ah mbili. Huku ni kukusanya katika sehemu ambapo mtu ametua na ni miongoni mwa safari zake za mwisho alizosafiri Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kujengea juu ya hayo unatakiwa kufahamu kwamba kufupisha safarini ni jambo limependekezwa kwa njia ya moja kwa moja na kukusanya safarini ni jambo limependekezwa kwa yule ambaye bado ni mwenye kuendelea na safari na ni jambo linalojuzu kwa yule ambaye ametua. Lakini wanaume wanatakiwa kutambua kwamba kama wako katika nchi ambayo kunaswaliwa swalah za mkusanyiko na hawana uzito wowote wa kwenda msikitini, basi ni wajibu kwao kwenda misikitini na waswali pamoja watu wengine. Katika hali hiyo wasikusanye na wala wasifupishe. Wakienda na wengine watatakiwa kuswali kikamilifu. Wakiswali na wengine watatakiwa kuswali Dhuhr kwa wakati wake, ´Aswr kwa wakati wake na swalah zengine zilizobaki pia kwa wakati wake.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Liqaa’ ash-Shahriy (49) http://binothaimeen.net/content/1124
  • Imechapishwa: 27/04/2019