Kwanini tunaswali swalah ya kupatwa kwa jua kwa sifa moja tu?

Swali: Ni kwa nini namna ya swalah ya kupatwa kwa jua inaswaliwa kwa sifa moja ilihali tunajua kuwa imepokelewa kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) zaidi ya sifa moja pamoja na kuwa baadhi ya wanachuoni wamesema kuwa ni dhaifu? Kwa sababu tunaona kuwa kupatwa kwa jua kunakariri. Ni kwa nini basi isiswaliwe kwa namna nyingi?

Jibu: Ni jambo linalojulikana kwamba kupatwa kwa jua hakukutokea baada ya kuhajiri kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) isipokuwa mara moja tu. Hivyo swalah zake zitakuwa ngapi? Swalah moja. Ikiwa al-Bukhaariy na Muslim wameafikiana kuwa ni Rukuu´ mbili katika kila Rak´ah, kisha Muslim au mwengine akapwekeka ya kwamba ni Rak´ah tatu, basi walioafikiana kwayo al-Bukhaariy na Muslim ndio yenye kutegemewa.

Shaykh-ul-Islaam (Rahimahu Allaah) amesema kwamba yaliyohifadhiwa katika swalah ya kupatwa kwa jua ni Hadiyth ya ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) ambapo amesimulia kuwa (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliswali Rak´ah mbili ambapo katika kila Rak´ah kulikuwa na Rukuu´ mbili na Sujuud mbili. Mengineyo ni dhaifu. Lakini hata hivyo imesihi kutoka kwa Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) ya kwamba waliswali Rukuu´ tatu katika kila Rak´ah moja.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Liqaa’ ash-Shahriy (38) http://binothaimeen.net/content/854
  • Imechapishwa: 19/06/2018