Swali: Tangu mama yangu afariki namswalia Rak´ah mbili. Je, kitendo changu hichi ni sahihi?

Jibu: Si sahihi. Kilichowekwa katika Shari´ah ni wewe kumwombea du´aa, kumtakia rehema, kumtolea swadaqah, kumuhijia au kumfanyia ´umrah. Yote haya yamesuniwa na ni yenye kumnufaisha. Kuhusu kumswalia ni jambo halina msingi. Hatukuwekewa Shari´ah ya kuwaswalia wafu. Lakini hajj haina neno. Vivyo hivyo ´umrah na swadaqah haina neno. Yote haya yamewekewa Shari´ah. Hali kadhalika kumwombea du´aa na kumtakia rehema. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Anapofariki mwanadamu basi matendo yake yote hukatika isipokuwa vitu vitatu; swadaqah yenye kuendelea, elimu ambayo watu wananufaika kwayo au mtoto mwema anayemuombea du´aa.”[1]

Hakusema kuwa amswalie. Bali amesema:

“… anayemuombea du´aa.”

Kwa hivyo mwombee du´aa mama yako na mtakie msamaha. Pia mwombee rehema na nafasi ya juu Peponi, kusamehewa madhambi, kumtolea swadaqah katika yale aliyosahilisha Allaah katika chakula, fedha, kuwapa nguo mafuraha na wahitaji. Yote haya ni mambo mazuri.

[1] Muslim (3084) na tamko ni lake, at-Tirmidhiy (1297) na Ahmad (8489).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majmuu´-ul-Fataawaa (11/416)
  • Imechapishwa: 16/11/2021