Kusoma al-Faatihah katika swalah za kusoma kwa sauti ndio maoni yenye nguvu

Swali: Ni ipi hukumu ya kusoma al-Faatihah katika swalah?

Jibu: Kisomo cha al-Faatihah inapokuja kwa imamu na yule anayeswali peke yake ni nguzo. Swalah zao hazisihi mpaka waisome. Imamu na yule mwenye kuswali peke yake endapo wataacha kusoma al-Faatihah katika Rak´ah yoyote ile swalah zao zinabatilika. Haya ni kwa maafikiano. Kwa kuwa kusoma al-Faatihah ni nguzo miongoni mwa nguzo za swalah.

Kuhusu maamuma anatakiwa kuisoma katika swalah za kusoma kimyakimya. Haya ni kwa makubaliano.

Ama katika swalah za kusoma kwa sauti ndipo wanachuoni wametofautiana. Wanachuoni wengi wanaonelea kuwa maamuma hatakiwi kusoma al-Faatihah katika swalah za kusoma kwa sauti na kwamba atosheke na kisomo cha imamu. Anaposema “Aamiyn” anazingatiwa ni kama kwamba na yeye amesoma. Wametumia dalili nyenginezo vilevile ikiwemo kwamba Muusa (´alayhis-Salaam) alipoomba dhidi ya Fir´awn Haaruun alikuwa akiitikia “Aamiyn”. Amesema:

وَقَالَ مُوسَىٰ رَبَّنَا إِنَّكَ آتَيْتَ فِرْعَوْنَ وَمَلَأَهُ زِينَةً وَأَمْوَالًا فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا رَبَّنَا لِيُضِلُّوا عَن سَبِيلِكَ ۖ رَبَّنَا اطْمِسْ عَلَىٰ أَمْوَالِهِمْ وَاشْدُدْ عَلَىٰ قُلُوبِهِمْ فَلَا يُؤْمِنُوا حَتَّىٰ يَرَوُا الْعَذَابَ الْأَلِيمَ

“Muusa akasema: “Ee Mola Wetu! Hakika Wewe Umempa Fir’awn na wakuu wake mapambo na mali katika uhai wa dunia. Ee Mola wetu, ili wapoteze kutokamana na njia Yako. Mola wetu! Ziangamize mali zao na fanya nyoyo zao ziwe ngumu kwani hawatoamini mpaka waione adhabu iumizayo.” (10:88)

Hapa Muusa alikuwa anaomba du´aa na huku Haaruun akiitikia “Aamiyn”.

Ndipo Allaah akasema:

قَالَ قَدْ أُجِيبَت دَّعْوَتُكُمَا

“Imekwishaitikiwa du’aa yenu nyinyi wote wawili.” (10:89)

Amewafanya wote wawili ni waombaji. Vilevile Imaam Ahmad (Rahimahu Allaah) amesema juu ya maneno Yake (Ta´ala):

وَإِذَا قُرِئَ الْقُرْآنُ فَاسْتَمِعُوا لَهُ وَأَنصِتُوا لَعَلَّكُمْ تُرْحَمُونَ

“Inaposomwa Qur-aan, basi isikilizeni na nyamazeni ili mpate kurehemewa.” (07:204)

“Aayah hii imeteremka wakiwa katika swalah.”

Wanachuoni wengine wanaonelea kuwa maamuma wanatakiwa kusoma al-Faatihah. Wanaonelea kuwa ni lazima na ni katika mambo yaliyovuliwa kutokanaa na ujumla wa maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Hana swalah yule asiyesoma ufunguzi wa Kitabu.”

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) pindi alipowageukia:

“Ni kwa nini mnanivuruga. Huenda mnasoma nyuma ya imamu wenu?” Maswahabah wakaitika: “Ndio.” Akasema: “Msifanye hivo isipokuwa mama wa Qur-aan. Kwani hana swalah yule asiyeisoma.”

Haya ndio maoni yenye nguvu. Maamuma anatakiwa kuisoma katika zile sehemu ambazo imamu ananyamaza. Asiponyamaza basi aisome kwa siri. Kwa sababu ni katika mambo yaliyovuliwa. Hilo ndio salama zaidi na ndio chaguo la kundi katika wanachuoni wahakiki. Ndio maoni ya al-Bukhaariy, Shaykh-ul-Islaam [Ibn Taymiyyah], Shaykh ´Abdul-´Aziyz bin Baaz (Rahimahumu Allaah), ndio madhehebu ya ash-Shaafi´iyyah, Abu Hurayrah na kundi la  wanachuoni wahakiki.

  • Mhusika: ´Allaamah ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah ar-Raajihiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: http://www.alharamain.gov.sa//index.cfm?do=cms.AudioDetails&audioid=67930&audiotype=lectures&browseby=speaker
  • Imechapishwa: 29/07/2017