Kuna mambo maalum ya kufanya kwa ajili ya kuipokea Ramadhaan?

Swali: Je, kuna mambo maalum ambayo muislamu anatakiwa kufanya ili kuikaribisha Ramadhaan?

Jibu: Mwezi wa Ramadhaan ndio mwezi mtukufu kwa mwaka. Kwa sababu Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) ameufanya kuwa maalum kwa kuujaalia kuwa faradhi na nguzo ya nne ya Uislamu na akawawekea waislamu kusimama nyusiku zake. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

”Uislamu umejengwa juu ya mambo matano; kushuhudia ya kwamba hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad ni Mtume wa Allaah, kusimamisha swalah, kutoa zakaah, kufunga Ramadhaan na kuhiji nyumba.”[1]

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mwenye kusimama Ramadhaan kwa imani na kwa matarajio, basi atasamehewa madhambi yake yaliyotangulia.”[2]

Sijui kitu maalum cha kuupokea mwezi wa Ramadhaan mbali na waislamu kuupokea kwa furaha, kufurahika, kumshukuru Allaah kwa kuwafikisha katika Ramadhaan na kuwatunuku kuwajaalia kuwa miongoni mwa waliohai ambao wanashindana katika matendo mema. Kufika katika Ramadhaan ni neema kubwa kutoka kwa Allaah. Kwa ajili hii ndio maana Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiwapa bishara njema Maswahabah zake kwa kufikiwa na Ramadhaan na huku akiwabainishia fadhilah zake na zile thawabu kubwa ambazo Allaah amewaandalia wafungaji na watakaosimama [nyusiku zake].

[1] al-Bukhaariy (08) na Muslim (09).

[2] al-Bukhaariy (2014) na Muslim (760).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majmuu´-ul-Fataawaa (15/09-10)
  • Imechapishwa: 14/05/2018