Kumswalia Mtume kwa sauti ya juu baada ya adhaana ni Bid´ah

Swali: Baadhi ya watu huku kwetu Jordan na baadhi ya miji mingine ambapo muadini anasema baada ya kuadhini:

اللهم صل على سيدنا محمد، وعلى آله وصحبه أجمعين

“Ee Allaah! Msifu bwana wetu Muhammad, kizazi chake na Maswahabah zake wote.”

Je, kuna ubaya kufanya hivo? Ni ipi hukumu yake?

Jibu: Mahali hapa panahitajia upambanuzi. Ikiwa muadhini anasema hivo kwa sauti ya chini, basi jambo hilo limewekwa katika Shari´ah kwa muadhini na wengineo wanaomuitikia muadhini. Kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mkimsikia muadhini basi semeni mfano wa anavosema, kisha niswalieni. Kwani hakika anayeniswalia mara moja basi Allaah humswalia mara kumi. Kisha niombeeni al-Wasiylah. Hakika hiyo ni ngazi Peponi ambayo haimstahikii isipokuwa mja miongoni mwa waja wa Allaah. Natumai kuwa mimi ndiye. Ambaye ataniombea kwa Allaah al-Wasilah basi umemthubutukia uombezi wangu.”

Ameipokea Muslim.

al-Bukhaariy amepokea katika “as-Swahiyh” yake kupitia kwa Jaabir bin ´Abdillaah (Radhiya Allaahu ´anhumaa) ambaye ameeleza kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Atakayesema wakati wa kusikia adhaana:

اللهم رب هذه الدعوة التامة والصلاة القائمة، آت محمداً الوسيلة والفضيلة، وابعثه مقاماً محموداً الذي وعدته

“Ee Allaah, Mola wa mwito huu uliotimia, swalah iliosimama, mpe bwana wetu Muhammad, al-Wasiylah na fadhilah na mfikishe daraja yenye kusifiwa ambayo umemuuahidi” basi utamthubutukia uombezi wangu siku ya Qiyaamah.”

Lakini ikiwa muadhini anasema hivo kwa sauti ya juu kama vile adhaana ni Bid´ah. Inaleta dhana kwamba ni sehemu katika adhaana. Haifai kuzidisha katika adhaana. Mwisho wa sentesi ya adhaana ni:

لا إله إلا الله

“Hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah.”

Kwa hivyo haijuzu kuzidisha juu ya hayo. Laiti kufanya hivo ingelikuwa ni kheri basi wangetutangulia Salaf. Bali Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) angewafunza Ummah wake na akawawekea hilo katika Shari´ah. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Atakayefanya kitendo kisichoafikiana na amri yetu atarudishiwa mwenyewe.”

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake. Msingi wake uko kwa al-Bukhaariy na Muslim kupitia kwa ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majmuu´-ul-Fataawaa (10/362)
  • Imechapishwa: 29/09/2021