Nimesoma gazeti la al-Jaziyrah idadi namba 12602 toleo la jumamosi tarehe 12 Rabiy´ al-Awwal makala ya Dr. Muhammad ´Abduh al-Yamaaniy kwa kichwa cha khabari “Min hunaa yabda´-ul-Hubb lir-Rasuuli Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambapo ndani yake anahimiza kuadhimisha sherehe ya kizushi katika mnasaba wa mazazi ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Anadai – kama ilivyo wazi katika kichwa cha khabari chake – ya kwamba kumpenda Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kunaanza kwa kusherekea mazazi yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hili linapelekea ya kwamba yule asiyesherehekea mnasaba huu hampendi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuanzia kwa Maswahabah watukufu na karne bora zilizosifiwa na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), kwa kuwa wao wao hawakusherehekea mnasaba huu. Tunamraddi Dr. huyu kwa kumwambia yafuatayo:

Kumpenda Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kunapelekea kumuamini yeye na ujumbe wake. Hiyo ni haki yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) juu yetu sisi. Allaah (Ta´ala) amesema:

إِنَّمَا وَلِيُّكُمُ اللَّـهُ وَرَسُولُهُ وَالَّذِينَ آمَنُوا

“Hakika mpenzi wenu ni Allaah na Mtume Wake na wale walioamini.” (05:55)

Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Hatoamini mmoja wenu mpaka mimi niwe ni mwenye kupendwa zaidi kwake kuliko mtoto wake, baba yake na watu wote.”

Katika Hadiyth nyingine imekuja ya kwamba ni lazima kwa muumini awe ni mwenye kumpenda Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) zaidi kuliko anavyoipenda nafsi yake mwenyewe. Hayo yametajwa katika Hadiyth ya ´Umar (Radhiya Allaahu ´anh). Lakini hata hivyo alama ya kumpenda sio kwa kuhuisha mnasaba wa kuzaliwa kwake, kwa kuwa hii ni Bid´ah. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ametahadharisha kutokamana na Bid´ah pale aliposema:

“Nakutahadharisheni na mambo ya kuzua. Hakika kila kitachozushwa ni Bid´ah na kila Bid´ah ni upotevu.”

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Yule atakayezua katika amri yetu hii yale yasiyokuwemo atarudishiwa mwenyewe.”

Katika upokezi mwingine imekuja:

“Atakayefanya kitendo kisichoafikiana na amri yetu atarudishiwa mwenyewe.”

Allaah (Jalla wa ´Alaa) amesema:

وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا

“Yale anayokupeni Mtume yachukueni, na yale anayokukatazeni, yaacheni.” (59:07)

Kusherehekea mazazi ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni Bid´ah iliyozuliwa baada ya karne bora. Ni jambo halina dalili kutoka katika Qur-aan na Sunnah. Ni kitendo chenye kurudishwa. Ni kumuasi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa kuwa yanaingia ndani ya jumla ya mambo yaliyozuliwa ambayo kayakataza Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Dr. Muhammad amesema:

“Laiti tungelifanya siku moja kuwa maalum kwa ajili ya kusoma historia ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).”

Tunamraddi Dr. kwa kumwambia:

Waislamu katika kipindi chote cha mwaka ni wenye kuendelea kusoma historia ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika masomo na misikiti. Kufanya siku moja maalum kwa ajili ya kuisoma ni jambo linaloingia katika Bid´ah. Isitoshe jambo hili linashusha umuhimu wa kuisoma historia yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kwa kuwa hiyo itakuwa na maana historia yake haisomwi isipokuwa tu mara moja kwa mwaka, nayo ni ile siku aliyozaliwa peke yake.

Dr. Muhammad amesema:

“Mataifa yote ulimwenguni yanasherehekea matukio mbali mbali ya wakuu wao yanayopitika katika historia yao na vilevile wanasherehekea ukumbusho wa wakuu wao kuanzia wanamume, wafikiriaji na viongozi wao.”

Tunamraddi Dr. kwa kumwambia:

Hakika kiigizo chetu ni Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah wake (Radhiya Allaahu ´anhum). Hawakuwa wakisherehekea yale uliyoyataja. Viongozi wa ulimwenguni sio viigizo vyetu. Amesema (Ta´ala):

وَإِن تُطِعْ أَكْثَرَ مَن فِي الْأَرْضِ يُضِلُّوكَ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ

“Kama ukiwatii wengi walioko ulimwenguni watakupoteza kutokamana na njia ya Allaah.” (16:116)

Kwa hiyo kiigizo chetu ni Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah wake. Baada ya hapo Dr. akataja sifa kadhaa za Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na baadhi ya kheri nyingi juu ya Ummah ambazo Allaah alizipitisha kupitia kwake. Halafu baada ya hapo Dr. akasema:

“Hivi kweli Mtume mtukufu hastahiki kutoka kwa Ummah wake kusherehekea siku ya kuzaliwa kwake?”

Tunamraddi kwa kumwambia:

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) haridhii hayo. Ni Bid´ah na kupetuka mipaka katika haki yake. Ametukataza Bid´ah na kufanya mambo ya kuzua. Sisi ni wenye kufuata na sio wenye kuzua.

Kisha Dr. akakokoteza tena kusoma historia ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kuwafunza nayo wanafunzi, jambo ambalo ni haki. Waislamu wanaisoma historia ya Mtume wao (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wanaifunza watoto wao masomoni na wanaisoma kwa jumla misikitini na kupitia vyombo mbali mbali vya mawasiliano. Yeye Dr. anachotaka ni kuliwekea hilo kikomo na kufanya maalum iwe siku ile anayodai kuwa ndio kazaliwa (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Baada ya hapo Allaah akamtamkisha Dr. haki kwa kusema:

“Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ndio kiigizo, ruwaza njema na kiumbe kitukufu. Allaah ametukirimu kupitia yeye na akatufanya kuwa katika Ummah wake. Vilevile tumeamrishwa kumfuata, kumuiga na kumpenda. Harufu ya maadhimisho haya yanapitika siku ile aliyozaliwa.”

Tunamraddi kwa kumwambia:

Midhali Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ndio kiigizo chetu na Allaah ametuamrisha kumfuata, je, Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akihuisha mnasaba huu kila mwaka katika siku maalum mpaka sisi tuweze kumuiga katika hilo? Jibu ni hapana. Bali aliliacha. Kile alichokiacha, nasi tunakiacha. Ametukataza Bid´ah. Kile alichotukataza, basi tunakomeka. Miongoni mwa hayo ni kuhuisha siku ya kuzaliwa kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Kuhusu yale yaliyotajwa na Dr. ya kwamba alikuwa akifurahikia siku ya kuzaliwa kwake, akiisherehekea na akiitilia umuhimu, tunamuuliza: “Iko wapi dalili ya hayo?” Dr. kutumia dalili ya kwamba alikuwa akifunga siku ya jumamatatu na kueleza kuwa hiyo ndio siku aliyozaliwa, tunamraddi kwa kumwambia:

1- Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakuwa akisherehekea siku ya kuzaliwa kwake. Alichofanya ni kufunga tu. Kwa hiyo kufunga ni Sunnah kwa kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alifanya hivo. Kuhusu kusherehekea ni Bid´ah kwa kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakufanya hivo.

2- Kufunga kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) siku ya jumatatu sio kwa sababu tu ni siku aliyozaliwa. Bali ni kwa sababu vilevile ni siku anayoonyeshwa Allaah matendo ya waja. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa anapenda matendo yake aonyeshwe Allaah ilihali amefunga, kama ilivyosihi kutoka kwake. Kadhalika alikuwa (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akifunga siku ya alkhamisi kwa sababu hiyo hiyo.

Kisha Dr. akasema:

“Katika ya wajibu juu yetu ni sisi kufuata Sunnah zake, kuifuata historia yake, kumuiga na kufanya kama alivyokuwa akifanya.”

Tunamjibu kwa kumwambia:

Umefanya vizuri. Lakini je, kumuiga kwa kufanya aliyofanya kunakuwa kwa kuzua kitu ambacho hakukifanya na wala hakukiamrisha? Hakika kufanya hivi kunahesabika ni kwenda kinyume na kumuiga (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kuzua katika dini yake.

Ee Dr – Allaah akuwafikishe – kumuadhimisha Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), tabia zake na matendo yake matukufu kunakuwa kwa yale aliyoyaweka katika Shari´ah juu ya haki yake kwa vile amenyanyua utajo wake na amefanya udhalilifu na uyonge kwa yule mwenye kwenda kinyume na amri yake. Amefanya kutajwa kwa Mtume kunaenda sambamba pamoja na utajo wake katika adhaana na iqaamah usiku na mchana katika vipindi vitano na katika Tashahhud ndani ya swalah. Bali Allaah amefanya kuingia katika Uislamu ni kwa kutamka shahaadah mbili; kushuhudia ya kwamba hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad ni Mtume wa Allaah. Kitendo chochote kitachofanywa na muislamu katika matendo ya kheri basi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anapata thawabu za mfano wa mtendaji huyo, kwa kuwa yeye ndiye kaelekeza katika hilo.

Halafu Dr. akamalizia makala yake kwa kusema:

“Kwa kumalizia nasema kuwa ni lazima nisisitize ya kwamba mapenzi ya kikweli kumpenda bwana wetu Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kunaanza kwa kuzifuata Sunnah zake na kupita juu ya mwongozo wake na yeye ndiye kafanywa kiigize chema katika matendo yetu yote. Tunamwambia:

Umesema kweli. Lakini, je, katika kumfuata na kumuiga (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni kuzua kitu juu ya haki yake ambacho hakutuwekea katika Shari´ah kama mfano wa kuzua kusherehekea mnasaba wa mazazi yake? Je, kitendo hichi ni katika Sunnah?

Ee Allaah! Tuwafikishe sisi, Dr. Muhammad na waislamu wote katika kuzitendea kazi Sunnah za Mtume wake na kuacha yale yanayoenda kinyume nayo – hakika wewe Mwenye kusikia na Mwenye kuziitikia du´aa. Swalah na salaam zimwendee Mtume wetu Muhammad, kizazi chake na Maswahabah wake.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: http://alfawzan.af.org.sa/node/2309
  • Imechapishwa: 12/02/2017