Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) ameeleza kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Swalah tano, ijumaa hadi ijumaa nyingine, Ramadhaan hadi Ramadhan nyingine, ni kifutio cha yaliyoko kati yake muda wa kuwa kunaepukwa madhambi makubwa.”[1]

Mja akifanya matendo haya matatu na akajiepusha na madhambi makubwa, basi Allaah humsamehe madhambi na makosa yake madogomadogo. Ni katika mifano mikubwa inayoingia ndani ya maneno ya Allaah (Ta´ala):

إِنَّ الْحَسَنَاتِ يُذْهِبْنَ السَّيِّئَاتِ

“Hakika mema yanaondosha mabaya.”[2]

Kutokana na upole Wake Allaah amefanya kule kuyaepuka madhambi makubwa ni sababu ya kusamehewa yale madhambi madogomadogo:

إِن تَجْتَنِبُوا كَبَائِرَ مَا تُنْهَوْنَ عَنْهُ نُكَفِّرْ عَنكُمْ سَيِّئَاتِكُمْ وَنُدْخِلْكُم مُّدْخَلًا كَرِيمًا

“Endapo mtajiepusha na madhambi makubwa mnayokatazwa, basi Tutakufutieni madhambi yenu madogo na tutakuingizeni katika mahali patukufu.”[3]

[1] Muslim.

[2] 11:114

[3] 4:31

  • Mhusika: ´Allaamah ´Abdur-Rahmaan bin Naaswir as-Sa´diy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bahjat-ul-Abraar, uk. 73
  • Imechapishwa: 23/02/2021