Kuchemua – neema kutoka kwa Allaah

Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Haki za muislamu juu ya muislamu mwenzie ni sita.” Kukasemwa: “Ni zipi hizo, ee Mtume wa Allaah?” Akasema: “Ukikutana naye, basi msalimie. Akikualika, basi mwitikie. Akikutaka umshauri, basi mshauri. Akipiga chafya na akamuhimidi Allaah, basi mwombee rehema. Akiwa mgonjwa, basi mtembelee. Akifa, basi fuata jeneza lake.”[1]

Kuchemua ni neema kutoka kwa Allaah. Kwa kupiga chafya kunatoka ule upepo uliofungamana kutoka katika viungo vya mwili vya mwanadamu. Allaah amefanya kuwepo njia kwa upepo huu ili umpumzishe mtu. Ndipo Allaah akasunilisha yule mwenye kwenda chafya amshukuru juu ya neema hii, akasunilisha kwa nduguye kumwabia:

يَرْحَمُكَ الله

“Allaah akurehemu.”

Baada ya hapo yule aliyechemua atasema:

يَهْدِيكم الله وَيُصْلِحُ بَالَكُمْ

“Allaah akuongoze na akutengenezee mambo yako.”[1]

Mchemuaji ambaye hamumuhimidi Allaah basi hastahiki kuombewa rehema. Hana mwengine wa kumlaumu isipokuwa nafsi yake mwenyewe kwa sababu yeye mwenyewe ndiye ambaye amejikosesha neema mbili: neema ya kumhimidi Allaah na neema ya nduguye kumwombea du´aa ya rehema.

[1] al-Bukhaariy (1240) na Muslim (2162).

  • Mhusika: ´Allaamah ´Abdur-Rahmaan bin Naaswir as-Sa´diy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Bahjat-ul-Abraar, uk. 92
  • Imechapishwa: 02/03/2021