Ibn ´Uthaymiyn mwanamke kukataa kuolewa kwa sababu ya kusoma chuo kikuu

Mwanamke kumaliza masomo katika chuo kikuu sio jambo la lazima. Inatosha kwa mwanamke kujua namna ya kusoma na kuandika. Kisha ajifunze yatayomnufaisha nyumbani kwake, jinsi ya kuwaangalia watoto na mume wake. Hana haja ya kusoma chuo kikuu. Akifanya hivo baadae atataka afanye kazi kwa mujibu wa masomo yake. Kuanzia hapo ndipo atakuwa ni mwenye kushughulishwa na kitu ambacho ni muhimu zaidi katika kuwalea watoto wake, nyumba ya mume wake na mengine.

Ninasema kwamba haifai kabisa kwa mwanamke kukataa kuolewa eti kwa sababu anataka kumaliza masomo yake kwenye chuo kikuu. Akichukua cheti cha sekondari ndani yake kina kheri kubwa na atakuwa amejifungulia mlango kwa yule anayetaka kujizidishia elimu. Kwa sababu atakuwa amefika katika upeo ambao anaweza kusoma na kuandika. Hili lina kheri kubwa.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Liqaa’ ash-Shahriy (20)
  • Imechapishwa: 30/12/2018