Ibn ´Uthaymiyn kuhusu swawm katika Sha´baan

Swali: Je, Sha´baan ufanywe ni mwezi maalum kwa ajili ya funga tofauti na miezi mingine?

Jibu: Ndio. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akikithirisha kufunga ndani  yake kiasi cha kwamba alikuwa akifunga siku nyingi isipokuwa chache tu. Kujengea juu ya hili mtu anatakiwa kufunga sana katika mwezi wa Sha´baan kwa kumuiga Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Kufunga tarehe 15 pekee kumepokelewa Hadiyth ambazo ni dhaifu hazikusihi kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kwa hivyo hazitakiwi kutendewa kazi. Kwa sababu kila kitu ambacho hakukithibiti kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) haifai kwa mtu akamuabudu Allaah kwacho. Kujengea juu ya hili haijuzu kwa mtu kufunga tarehe 15 pekee kwa sababu jambo hilo halikusihi kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kitu ambacho hakikuthibiti basi hicho ni Bid´ah.

Kuhusu fadhila za usiku wa tarehe 15 Sha´baan kumepokelewa Hadiyth. Lakini hata hivyo ni dhaifu ambazo hazikusihi kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu alayhi wa sallam). Kujengea juu ya hili usiku wa tarehe 15 Sha´baan ni kama usiku wa tarehe 15 Rajab au miezi mingine. Kwa hivyo usiku huu usifanywe ni maalum kwa kufanya kitu chochote. Bali ni kama nyusiku zengine. Kwa sababu Hadiyth zilizopokelewa juu ya hilo ni dhaifu.

Vilevile kuufanya usiku huo maalum kwa kusimama usiku ni Bid´ah kwa sababu haikuthibiti kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwamba alikuwa akiukhusisha usiku huo kwa kusimama. Bali usiku huo ni kama nyusiku zengine. Kama mtu ana mazowea ya kuamka usiku basi aamke usiku huo kama anavyoamka nyusiku zengine. Kama hana mazowea ya kuamka usiku basi asiukhusishe usiku huo wa tarehe 15 Sha´baan kwa kusimama. Kwa sababu jambo hili halikuthibiti kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Jambo lililo mbali zaidi [na uongofu] ni kuwa baadhi ya watu wanaufanya maalum kwa kuswali idadi ya Rakaa´ maalum ambazo hazikuthibiti kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kwa hivyo usiku usikhusishwe usiku huo kwa kusimama.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: http://ajurry.com/home/%D8%A3%D8%AD%D9%83%D8%A7%D9%85-%D8%B4%D9%87%D8%B1-%D8%B4%D8%B9%D8%A8%D8%A7%D9%86/
  • Imechapishwa: 20/04/2018