Swali: Nyinyi mnawaraddi Ahl-ul-Bid´ah, wanaoenda kinyume na mfumo wa Salaf na wale wanaothibitisha masuala fulani na wanatumia Hadiyth dhaifu. Lakini hata hivyo Imaam al-Barbahaariy amethibitisha masuala fulani na akatumia Hadiyth zilizotungwa na dhaifu. Ni vipi utawaraddi wale wenye kutumia Hadiyth dhaifu na wakati huo huo unawaacha baadhi ya maimamu wa Salaf?

Jibu: Kwanza mimi sikubali ya kwamba al-Barbahaariy anatumia Hadiyth dhaifu na zilizotungwa. Tubainishie madai yako na kile khaswa unachotukemea. Mimi nawaheshimu Salaf wote na wala simpondi yeyote katika wao. Hakuna tunaowaraddi isipokuwa Ahl-ul-Bid´ah peke yao. Ama Salaf wanaotambulika kwa Ikhaasw, ukweli na dini – hata kama watakosea tunayazingatia ya kwamba ni mwenye kupewa ujira katika kosa lao hilo:

“Atakayejitahidi na akapatia basi ana ujira mara mbili. Yule mwenye kujitahidi na akakosea basi ana ujira mara moja.”[1]

Mtu akitambulika kwa uchaji, wema na ukweli katika kuitafuta haki kisha akakosea, huyo ni mwenye kupewa ujira.

Kuhusu Ahl-ul-Bid´ah hayawahusu. Ahl-ul-Bid´ah wao ni wenye kufuata matamanio yao. Kwa ajili hii utaliona jitu lenye kufuata matamanio yake halijirudi. Ama huyu mwengine anajirudi mwenyewe. Akiambiwa kuwa amekosea anajirudi. ash-Shaafi´iy alijirudi mwenyewe. Utamuona Ahmad anatoka maoni haya na kwenda mengine. Yote haya kwa ajili ya kuitafuta haki na kuitendea kazi dalili. Hachezi na nafsi yake. Anaweza kukosea na akajirudi. Abu Bakr na wengine ndivyo walivyokuwa. Watu wa haki ambao tunatambua kutoka kwao Ikhlaasw na kwamba wanajirudi katika haki ni wenye kupewa ujira pindi wanaposea. Hilo haliwadhuru. Kuhusu Ahl-ul-Ahwaa´ hawana:

فَأَمَّا الَّذِينَ فِي قُلُوبِهِمْ زَيْغٌ فَيَتَّبِعُونَ مَا تَشَابَهَ مِنْهُ ابْتِغَاءَ الْفِتْنَةِ وَابْتِغَاءَ تَأْوِيلِهِ

“Ama wale ambao katika nyoyo zao mna upotovu hufuata zile zisizokuwa wazi maana zake kutafuta fitina na kutafuta kuzipotosha.”[2]

Kwa ajili hii utawaona Ahl-ul-Ahwaa´ hawajirudi. Kwa ajili hii ndio maana amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Wanatoka katika dini kama vile mshale unavotoka kwenye upinde wake. Kisha hawarudi kwayo mpaka siku ya Qiyaamah.”[3]

Hivi sasa mzushi wa aina yoyote ile harudi katika haki. Utampa makumi ya dalili kunako suala fulani na utamletea maneno ya wanachuoni lakini hata hivyo harudi katika haki. Hivi ndivyo walivyo Ahl-ul-Ahwaa´.

[1] al-Bukhaariy (7352) na Muslim (1716).

[2] 03:07

[3] al-Bukhaariy (6933) na Muslim (1064).

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Usuwl-is-Sunnah, uk. 61-62
  • Imechapishwa: 20/08/2017