Swali 336: Imepokelewa kutoka kwa Ibn ´Abbaas ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikusanya al-Madiynah baina ya Dhuhr na ´Aswr na kati ya Maghrib na ´Ishaa pasi na safari wala mvua. Ni lini kunafanywa hivo?

Jibu: Hadiyth hii sio kama wanavofikiria wanafunzi wengi mtu kujifanyia tu hivo pasi na sababu. Kipindi ambapo muislamu anakuwa ni mkazi basi ni lazima kwake kuchunga kutekeleza swalah ndani ya wakati wake. Atapopatwa na udhuru au uzito ndipo anaondokewa kwa sababu ya uzito huo. Hapo ndipo itafaa kwake kukusanya; ni mamoja mkusanyo wa kutanguliza au mkusanyiko wa kuchelewesha.

Sababu ya Kishari´ah ya mkusanyo huu ni kwa sababu ya kuwaondoshea uzito waislamu. Ama kusipokuwa na uzito haifai kukusanya. Kwa hivyo ni lazima kuipokea Hadiyth kwa ukamilifu wake. Hivyo ndivo Hadiyth inatimia. Watu walimuuliza Ibn ´Abbaas: “Alikusudia nini kwa jambo hilo?” Akajibu:

“Alitaka asiwatie uzito Ummah wake.”

Kwa hivyo kukusanya kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika hali ya ukazi pasi na udhuru wa mvua ni kwa ajili ya kuwabainishia watu kufaa kukusanya kwa lengo la kuwaondoshea watu uzito. Kwa hivyo hapakuweko udhuru wa Kishari´ah ulio wazi. Lakini ni jambo linalofungamana na yule mfanya ´ibaadah kwa nafsi yake mwenyewe. Kwa sababu kwa mfano anapata uzito wa kutekeleza kila swalah za vipindi viwili hivyo ndani ya wakati wake. Haina maana kwamba inafaa kwake kukusanya kwa hali zote.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Fataawaa al-Mar´ah al-Muslimah, uk. 128
  • Imechapishwa: 04/09/2019