Hadiyth pekee iliyosihi kuhusu Kursiy

109- Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mbingu saba ukizilinganisha na Kursiy si kitu isipokuwa ni kama mfano wa kijipete cha chuma kilichotupwa katika uwanja mkubwa. ´Arshi ukiilinganisha na Kursiy ni kama huo uwanja mkubwa ukiulinganisha na kijipete hicho.”

Ameipokea Muhammad bin Abiy Shaybah katika “Kitaab-ul-´Arsh”[1].

Hadiyth kwa njia zote hizi ni Swahiyh.

Hadiyth ni dalili ya wazi yenye kuonyesha kwamba Kursiy ndio kiumbe kikubwa zaidi baada ya ´Arshi na kwamba ni kitu kilichosimama kivyake na si kitu cha kimaana. Hapa kuna Radd kwa wale wenye kufasiri Kursiy kwamba ni ufalme na utawala ulioenea, kama ilivyotajwa katika baadhi ya tafsiri ya Qur-aan. Imepokelewa kutoka kwa Ibn ´Abbaas alisema kuwa ni elimu, lakini cheni ya wapokezi wake si Swahiyh. Katika cheni ya wapokezi yupo Ja´far  bin Abiyl-Mughiyrah ambaye kapokea kutoka kwa Sa´iyd bin Jubayr ambaye kapokea kutoka kwa Ibn ´Abbaas. Upokezi huo umepokelewa na Ibn Jariyr. Ibn Mandah amesema:

“Ibn Abiyl-Mughiyrah si mwenye nguvu kabisa inapokuja kwa Ibn Jubayr.”[2]

Tambua kwamba hakukusihi kitu kuhusu Kursiy isipokuwa Hadiyth hii tu. Zipo Hadiyth zinazosema kwamba Kursiy ni mahali pa kuwekea miguu, kwamba ina sauti kama kitako cha farasi, kwamba inabebwa na Malaika wane ambapo kila Malaika ana nyuso nne na nyoyo zao ziko chini ya mwamba ulioko chini ya ardhi ya saba na kadhalika. Hakuna chochote katika hayo kilichosihi kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

[1] 1/114.

[2] Tazama ”adh-Dhwa´iyfah” (2/307).

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Silsilat-ul-Ahaadiyth as-Swahiyhah (1/1/226)
  • Imechapishwa: 23/06/2019