Dalili yenye kuonyesha kuwa Maulidi ni Bid´ah

Allaah (´Azza wa Jall) ameeleza katika Qur-aan kwamba ni wajibu kwa kila mtu kumtii Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), kwamba ni lazima na kwamba hakuna budi kumtii Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Allaah (Ta´ala) amesema:

وَمَا كَانَ لِمُؤْمِنٍ وَلَا مُؤْمِنَةٍ إِذَا قَضَى اللَّـهُ وَرَسُولُهُ أَمْرًا أَن يَكُونَ لَهُمُ الْخِيَرَةُ مِنْ أَمْرِهِمْ ۗ وَمَن يَعْصِ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ فَقَدْ ضَلَّ ضَلَالًا مُّبِينًا

“Haiwi kwa muumini mwanamume na wala kwa muumini mwanamke pindi anapohukumu Allaah na Mtume Wake jambo lolote iwe wana khiyari katika jambo lao; na anayemuasi Allaah na Mtume Wake, basi hakika amepotoka upotofu wa wazi.”[1]

Hakuna yeyote ambaye ana khiyari juu ya amri ya Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Amesema (Ta´ala):

فَلْيَحْذَرِ الَّذِينَ يُخَالِفُونَ عَنْ أَمْرِهِ أَن تُصِيبَهُمْ فِتْنَةٌ أَوْ يُصِيبَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ

“Basi watahadhari wale wanaokhalifu amri yake; isije kuwapata fitina au ikawapata adhabu iumizayo.”[2]

وَمَا آتَاكُمُ الرَّسُولُ فَخُذُوهُ وَمَا نَهَاكُمْ عَنْهُ فَانتَهُوا

”Kile alichokupeni Mtume basi kichukueni na kile alichokukatazeni basi kiacheni.”[3]

Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Ummah wangu wote utaingia Peponi isipokuwa yule atakayekataa.” Kukasemwa: “Ni nani atakayekataa, ee Mtume wa Allaah?” Akasema: “Yule atakayenitii, ataingia Peponi, na atakayeniasi, amekataa.”

Kwa hivyo alama ya kumpenda Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni kumfuata, kujisalimisha na kunyenyekea juu ya yale aliyokuja nayo (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Haiwi kwa kufanya mambo ambayo Allaah hakuteremsha dalili yoyote juu yake. Baadhi ya watu wanaweza kuchukulia wepesi mambo yaliyozuliwa kwa hoja eti hakuna walichokusudia isipokuwa kheri tupu, wana makusudio mazuri na kwamba wanafanya jambo kwa lengo jema. Ni lazima malengo mazuri yaafikiane na Sunnah.

Miongoni mwa mambo yaliyozuliwa ambayo wamepewa mtihani kwayo watu wengi ni kusherehekea maulidi ambayo ni kuzaliwa kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Jambo hili halina msingi katika dini. Dalili yenye kuonyesha kuwa ni jambo lisilokuwa na msingi wowote ni kwamba zile karne tatu bora zote zimepita na hawajui kabisa kitu kinachoitwa ´maulidi`. Karne zote hizi tatu zilipita na hakukupatikana jambo la kusherehekea maulidi. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakusherehekea maulidi yake na wala hakusunisha kusherehekea maulidi yake. Maswahabah wakiwemo makhaliyfah waongofu (Radhiya Allaahu ´anhum) – ambao ndio watu walio msitari wa mbele kabisa katika kila kheri na waliowashinda watu wote katika kila kheri – hawakufanya hivo. Maswahabah wote zama zao ziliisha na hakukupatikana kitu katika hayo. Taabi´uun na waliokuja baada yao hali ni hiyohiyo karne zao zilikatika na hakukupatikana kitu katika hayo. Kisha waliokuja baada ya Taabi´uun karne zao zilikatika na hakukupatikana kitu katika hayo. Miaka miatatu kamilifu hakukuweko kabisa kitu kinachoitwa ´sherehe ya mazazi ya Mtume`. Lau ingelikuwa ni kheri basi wangetutangulia kwalo watanguliaji na waliowafuata kwa wema (Radhiya Allaahu ´anhum); Maswahabah wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

[1] 33:36

[2] 24:63

[3] 59:07

  • Mhusika: ´Allaamah ´Abdul-Muhsin bin Hamad al-´Abbaad
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: http://www.ajurry.com/vb/showthread.php?t=36078
  • Imechapishwa: 01/11/2019