Dalili katika Qur-aan juu ya uongozi wa Abu Bakr as-Swiddiyq

Allaah (´Azza wa Jall) amesema:

صِرَاطَ الَّذِينَ أَنْعَمْتَ عَلَيْهِمْ غَيْرِ الْمَغْضُوبِ عَلَيْهِمْ وَلَا الضَّالِّينَ

“Njia ya wale Uliowaneemesha na si ya walioghadhibikiwa wala waliopotea.” (01:07)

Hapa kuna tanbihi mbili:

1- Tunapata faida kutoka katika Aayah hii tukufu kusihi kwa uongozi wa Abu Bakr as-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ´anh). Kwa sababu anaingia miongoni mwa wale ambao Allaah ametuamrisha katika Suurah “al-Faatihah” kumuomba Allaah atuongoze katika njia yao. Kwa hivyo hiyo ni dalili inayofahamisha kuwa njia yao ndio iliyonyooka. Hayo ni katika maneno Yake (Ta´ala):

اهْدِنَا الصِّرَاطَ الْمُسْتَقِيمَ صِرَاطَ الَّذِينَ أَنْعَمْتَ عَلَيْهِمْ غَيْرِ الْمَغْضُوبِ عَلَيْهِمْ وَلَا الضَّالِّينَ

“Tuongoze njia iliyonyooka. Njia ya wale Uliowaneemesha na si ya walioghadhibikiwa wala waliopotea.” (01:06-07)

Allaah amebainisha ni kina nani aliowaneemesha. Miongoni mwa akaorodhesha wale wakweli mno (as-Swiddiqiyn).

Isitoshe Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amebainisha kuwa Abu Bakr ni miongoni wa wakweli mno. Hilo ni wazi ya kwamba anaingia miongoni mwa wale aliowaneemesha ambao Allaah ametuamrisha kumuomba atuongoze katika njia yao. Kwa hivyo hakukubaki utatizi wowote ya kwamba Abu Bakr as-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ´anh) yuko juu ya njia iliyonyooka na kuwa uongozi wake ni haki.

  • Mhusika: Imaam Muhammad al-Amiyn ash-Shanqiytwiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Adhwaa’-ul-Bayaan (1/178-179)
  • Imechapishwa: 09/06/2017