Bi mdogo amemuhalalishia mumewe kuegemea kwa bi mkubwa

Swali: Mimi nimeolewa na kijana wa chuo kikuu. Nimejaaliwa kupata watoto wa kiume na wa kike. Mume wangu ameoa juu yangu mwanamke mwingine ambaye anampendelea juu yangu. Nataka kujua mambo yafuatayo; je, dhimma ya mume wangu inatakasika akiniomba nimhalalishie ambapo nikamhalalishia kwa mdomo wangu tu kwa sababu ya kumuogopa?

Jibu: Ni wajibu kwa mume aliye na wake wawili kufanya uadilifu kati yao kwa kiasi cha anavoweza. Afanye uadilifu katika maneno, vitendo, wakati wa kustarehe nao. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Atakayekuwa na wake wawili ambapo akapinda kwa mmoja wao, basi atakuja siku ya Qiyaamah na bega lake moja limepinda.”

Lakini mtu haadhibiwi kwa kitu ambacho hana uwezo nacho kama mfano wa mapenzi, mahaba na yenye kuambatana na hayo. Amesema (Ta´ala):

لَا يُكَلِّفُ اللَّـهُ نَفْسًا إِلَّا وُسْعَهَا

”Allaah hakalifishi nafsi yoyote isipokuwa kwa kadiri ya uwezo wake.”[1]

Ikiwa mwanaume huyu ambaye ameashiriwa na mwanamke ameegemea kwa huyo mke mwengine, kitendo hicho ni haramu kwake na hakijuzu kwake. Akimhalalishia kwa mdomo wake pasi na moyo wake dhimma yake haitakasiki isipokuwa hapa duniani tu. Dhimma yake inatakasika duniani tu. Lakini anaweza kuwa na udhuru mbele ya Allaah siku ya Qiyaamah akiegemea kwa huyo mke mwengine na yeye mke wa kwanza amekwishamhalalishia. Kwa sababu mume wake hayajui yaliyomo ndani ya moyo wake. Ikiwa hayajui yaliyomo ndani ya moyo wake hakalifishwi kwa kitu asichokijua. Anaweza kutumia hoja kwamba yeye alimhalalishia na kama ameshafanya hivo kwamba yeye hajui yaliyomo ndani ya moyo wake na kwamba yeye ndiye kamuidhinishia na ataendelea kumili kwa huyo mke mwengine. Kwa hoja hiyo pengine akawa ni mwenye kupewa udhuru mbele ya Allaah.

Lakini pamoja na haya mwanamke anapaswa awe muwazi ili mume wake awe juu ya ubainifu na utambuzi. Baada ya hapo ima afanye uadilifu kati yao au ashindwe. Akishindwa atampa khiyari ima ya kuendelea kuishi naye katika hali hiyo au atengane naye.

[1] 02:286

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Nuur ´alaad-Darb (13) http://binothaimeen.net/content/6778
  • Imechapishwa: 08/02/2021