Anapanga safari Ramadhaan ili aweze kukwepa kufunga

Swali: Ni ipi hukumu ya kusafiri katika Ramadhaan kwa ajili ya kutaka kula?

Jibu: Kimsingi kufunga ni wajibu kwa mtu. Bali ni wajibu na ni nguzo moja wapo miongoni mwa nguzo za Uislamu kama inavyotambulika. Haijuzu kwa mtu kufanya hila katika jambo la wajibu Kishari´ah ili aweze kulikwepa. Mwenye kusafiri kwa ajili ya kutaka kula basi safari yake hii itakuwa ni haramu. Kula pia itakuwa ni haramu juu yake.

Ni wajibu kwake kutubu kwa Allaah (´Azza wa Jall) na kurudi kutoka safarini mwake na afunge. Asiporudi ni wajibu kwake kufunga hata kama atakuwa safarini. Kwa kifupi ni kwamba haijuzu kwa mtu kufanya hila kwa ajili ya kutaka kula katika Ramadhaan. Kufanya hila juu ya kuangusha jambo la wajibu halianguki kama ambavyo kufanya hila juu ya jambo la haramu haligeuki kuwa lenye kuruhusiwa.

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Majmuu´-ul-Fataawaa (19/133)
  • Imechapishwa: 21/06/2017