Miongoni mwa mienendo ya watu wenye maoni batili na ´Aqiydah mbovu zinazopingana na Qur-aan, Sunnah na uelewa wa Salaf wa Ummah ambao tumeamrishwa kuwaiga ni kutaka kuwababaisha wasomaji kwa ibara wasizofahamu dalili zake isipokuwa kwa wale wanaojua mifumo yao. Mfano wa hilo ni pale al-Khaliyliy aliposema:

“Hakika maneno ya Imaam Ibn-ul-Qayyim ambayo ameyatolea dalili kutoka katika Qur-aan, Sunnah na maneno ya Salaf ya kwamba Allaah (´Azza wa Jall) anazungumza pale anapotaka kuwa ni hoja kwake juu ya imani inayosema kwamba maneno ya Allaah yameumbwa” katika maneno hayo kunaingia vilevile Qur-aan ambayo imeumbwa.””

Anachokusudia kwa “kuzungumza kwa Allaah” ni kuzua maneno katika wakati yanapokuwa. Kwa msemo mwingine anachokusudia kwa neno “kuzua” ni kuyaumba maneno kipindi kile cha kuyazungumza na kwamba Allaah ameyaumba maneno haya katika kipindi hichi na sifa hii ya maneno haikuwa ni yenye kusimama katika dhati ya Allaah (Ta´ala). Ndio maana hakusema:

“Allaah alizungumza katika wakati aliotaka kuzungumza kwa mujibu wa matakwa na utashi wake.”

Amesema kwa kutumia ibara ya “kuzua”, ambayo kwa mujibu wake ni kuyaumba maneno.

Ibn-ul-Qayyim hakumaanisha yale al-Khaliyliy aliyoyaelewa kimakosa ya kwamba kuzuka maneno katika nyakati hizi mbalimbali maana yake ni “kuyaumba”. Anachotaka kusema ni kwamba maneno ni sifa ya kidhati na ya kimatendo na kwamba Allaah anazungumza pindi anapotaka na kwa namna anayoitaka. Vilevile amekusudia kuwaambia Mu´attwilah katika wakati wake na kwa wale warithi wake katika wakati huu wa leo – kama mfano wa al-Khaliyliy na watu mfano wake – ya kwamba dalili za Qur-aan na Sunnah zinafahamisha waziwazi ya kwamba Allaah anazungumza kwa matakwa na utashi wake katika kila wakati na zama, mchana na usiku, duniani na huko Aakhirah…

Haya ndio yenye kuingia akilini ambayo yanapokelewa na akili zilizosalimika na fahamu zilizonyooka. Tukiangalia siza kamilifu na pungufu walizonazo viumbe, basi itatubainikia kuwa mtu anayeweza kuzungumza na aliyesalimika kutokamana na madhara ni mkalifu zaidi katika sifa hii kuliko bubu asiyeweza kutamka. Tutapata kuwa yule ambaye ni muweza wa kuzungumza ile sifa ya maneno/kuzungumza imesimama naye na haikutengana naye, kama wanavyoonelea Mu´tazilah na vifaranga vyao. Anapotaka kuzungumza basi huzungumza kwa kile anachokitaka kwa kuwa ni muweza wa kuzungumza. Upande mwingine bubu hawezi kuzungumza kwa kuwa ile sifa ya maneno haikusimama naye. Hata kama atataka kuzungumza hatoweza.

Kwa haya inapata kumbainikia msomaji ya kwamba al-Khaliyliy hamthibitishii Allaah (´Azza wa Jall) sifa ya maneno iliyosimama Kwake (Ta´ala) na haonelei kuwa anazumgumza pale anapotaka na kwa kile anachokitaka kwa maneno yasiyofanana na kiumbe. Kwani Allaah:

لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ ۖ وَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ

“Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.”[1]

[1] 42:11

  • Mhusika: Allaamah ´Aliy bin Naaswir al-Faqiyhiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ar-Radd al-Qawiym, uk. 127-128
  • Imechapishwa: 08/04/2017