98. Sura ya tatu: Msimamo wa Ummah Kiislamu kutokamana na wazushi

Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah ni wenye kuendelea siku zote kuwaraddi watu wa Bid´ah, kuwakaripia Bid´ah zao na wanawakataza kuziendeleza. Hapa tunakupigia baadhi ya mifano ya jambo hilo:

1- Umm-ud-Dardaa´  ameeleza:

“Abud-Dardaa´ aliingia nyumbani kwangu akiwa ni mwenye kukasirika. Nikamuuliza: “Una nini?” Akajibu: “ Ninaapa kwa Allaah kwamba sikutambua chochote katika dini ya Muhammad zaidi ya kuwaona tu wakiswali mkusanyiko.”[1]

2- ´Amr bin Yahyaa ametueleza: Nilimsikia baba yangu akieleza kutoka kwa baba yake ambaye amesema:

“Tulikuwa tukikaa nje ya mlango wa ´Abdullaah bin Mas´uud (Radhiya Allaahu ´anh) kabla ya Fajr na anapotoka tunaenda naye mpaka msikitini. Siku moja akatujia Abu Muusa al-Ash´ariy (Radhiya Allaahu ´anh) na kusema: “Abu ´Abdir-Rahmaan ameshakujieni?” Tukasema: “Hapana.” Akakaa na sisi mpaka alipotoka. Alipotoka sote tukasimama. Abu Muusa akamwambia: “Ee Abu ´Abdir-Rahmaan! Hivi karibuni nimeona msikitini kitu nimechokipinga na ilikuwa ni kitu cha kheri tu.” Akasema: “Ni kipi?” Akasema: “Ukiishi utakiona. Msikitini nimewaona watu wamekaa mzunguko wakisubiri swalah. Katika kila mzunguko kuna mtu na kwenye mikono yao wana vijiwe vidogo vidogo. Anasema: “Semeni: “Allaahu Akbar” mara mia”, wanafanya hivo. Kisha anasema: “Semeni: “Laa ilaaha illa Allaah” mara mia”, wanafanya hivo. Kisha anasema: “Semeni: “Subhaana Allaah” mara mia”, wanafanya hivo.” Akasema: “Uliwaambia nini?” Akasema: “Sikuwaambia kitu. Ninasubiri neno lako au amri yako.” Akasema: “Ungeliwaamrisha wahesabu madhambi yao na kuwadhamini kuwa hakuna chochote katika mema yao kitachopotea.” Halafu akaenda na tukafuatana naye. Alipofika katika mzunguko mmoja miongoni mwa mizunguko ile akasimama na kusema: “Nini haya ninayoona mnafanya?” Wakasema: “Ee Abu ´Abdir-Rahmaan! Ni vijiwe tu ambavyo tunafanya navyo Takbiyr, Tahliyl na Tasbiyh.” Akasema: “Hesabuni madhambi yenu. Mimi ninakudhaminini hakuna chochote katika mema yenu kitachopotea. Ee Ummah wa Muhammad! Ole wenu! Ni haraka iliyoje mmeangamia! Hawa hapa Maswahabah wa Mtume wenu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) bado wamejaa, nguo zake hazijaharibika na chombo chake hakijapasuka. Ninaapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko Mkononi Mwake ima nyinyi mkono katika dini bora kuliko dini ya Muhammad au mmefungua mlango wa upotevu.” Wakasema: “Ee Abu ´Abdir-Rahmaan! Hatukukusudia jengine isipokuwa kheri tu.” Akasema: “Ni wangapi wenye kutaka kheri na hawaifikii! Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ametueleza kuwa kutakuwepo watu wataoisoma Qur-aan bila ya kuvuka koo zao. Ninaapa kwa Allaah sijui pengine wengi wao ndio nyinyi wenyewe.” Kisha akatoka pale akenda zake.” ´Amr bin Salamah amesema: “Tuliona wengi katika wao wakishirikiana na Khawaarij siku ya Nahrawaan.”[2]

3- Kuna mtu alikuja kwa Imaam Maalik bin Anas (Rahimahu Allaah) akasema: “Nahirimia kwa wapi?” Akasema: “Katika kituo kilichowekwa na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na akahirimia kutokea kwa hapo.” Mtu yule akasema: “Vipi ikiwa nitahirimia mbali na hapo?” Maalik akasema: “Sikushauri kufanya hivo.” Mtu yule akauliza: “Unachelea nini juu ya hilo?” Akasema: “Nachelea juu yako fitina.” Akauliza: “Fitina ipi?” Maalik akasema: “Allaah (Ta´ala) anasema:

فَلْيَحْذَرِ الَّذِينَ يُخَالِفُونَ عَنْ أَمْرِهِ أَن تُصِيبَهُمْ فِتْنَةٌ أَوْ يُصِيبَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ

“Basi watahadhari wale wanaokhalifu amri yake; isije kuwapata fitina au ikawapata adhabu iumizayo.”[3]

Kuna fitina ipi kubwa inayoshinda wewe kufanywa maalum kwa fadhilah ambayo hakufanywa kwayo maalum Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam)[4]?

 Hii ni baadhi tu ya mifano. Bado wanachuoni ni wenye kuendelea kuwakaripia wazushi katika kila zama. Himdi zote njema anastahiki Allaah.

[1] al-Bukhaariy (650).

[2] ad-Daarimiy (208).

[3] 24:63

[4] Haya yametajwa na Abu Shaamah katika kitabu ”al-Baa´ith ´alaa Inkaar-il-Bid´ah wal-Hawaadith”, uk. 14 akinukuu kutoka kwa Abu Bakr al-Khallaal.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ´Aqiydat-ut-Tawhiyd, uk. 189-191
  • Imechapishwa: 07/07/2020