93. al-´Ayyaashiy upotoshaji wake wa nne wa an-Nisaa´

al-´Ayyaashiy amesema alipokuwa akifasiri Aayah:

إِنَّ اللَّـهَ يَأْمُرُكُمْ أَن تُؤَدُّوا الْأَمَانَاتِ إِلَىٰ أَهْلِهَا وَإِذَا حَكَمْتُم بَيْنَ النَّاسِ أَن تَحْكُمُوا بِالْعَدْلِ ۚ إِنَّ اللَّـهَ نِعِمَّا يَعِظُكُم بِهِ ۗ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ سَمِيعًا بَصِيرًا

“Hakika Allaah anakuamrisheni kurudisha amana kwa wenyewe na pindi mtakapohukumu kati ya watu, basi mhukumu kwa uadilifu. Hakika uzuri ulioje anayokuwaidhini nayo Allaah. Hakika Allaah ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.”[1]

“Abu ´Abdillaah amesema: “Inatulenga sisi na kwamba yule wa kwanza amrudishie imamu vitabu, elimu na silaha baada yake.”

وَإِذَا حَكَمْتُم بَيْنَ النَّاسِ أَن تَحْكُمُوا بِالْعَدْلِ

“… na pindi mtakapohukumu kati ya watu, basi mhukumu kwa uadilifu.”

Bi maana mlionao mbele yenu.”[2]

Katika Aayah hii kuna Shari´ah yenye kuenea juu ya Ummah wa Muhamamd (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) mpaka siku ya Qiyaamah; ya kurudisha amana kwa wenyewe na kuwahukumu watu kwa uadilifu pindi wanapozozana katika mambo ya kidini na ya kidunia. Amana zilizoamrishwa zinajumuisha zile amana/haki zote za wajibu za Allaah juu ya mja.

Tafsiri hii ya kipumbavu ambayo iko dhidi ya Kitabu cha Allaah haiendani na maneno ya mtu, sembuse maneno ya Allaah. Allaah amemtakasa Abu ´Allaah juu ya uongo huu. Ninaapa kwa Allaah hawakulengwa maimamu katika Aayah hii tukufu.

Isitoshe mtu anaweza kujiuliza viko wapi vitabu hivi vilivyofichwa, elimu hizi zilizofichwa na silaha za ndoto ambazo maimamu wanapeana kwa mujibu wa mwenendo wa Baatwiniyyah. Waislamu wote ulimwenguni wamefaidika nini na hayo katika hii miaka yote hii elfu moja na mia nne? Baatwiniyyah na maadui wa Uislamu, waislamu na familia ya Mtume! Kuna faida gani ya vitabu hivi, elimu hii na silaha hii? Hakuna kitu. Hii ni njia moja wapo wanayotumia Raafidhwah Baatwiniyyah ili waweze kula pesa za wapumbavu kwa kutumia jina la familia ya Mtume.

Halafu jengine ni kwamba hakuna imamu yeyote baada ya ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anh) aliyeshika utawala juu ya waislamu. Ni vipi watahukumu kwa uadilifu? Lau walikuwa ni wenye kuweza kufanya hivo lakini wakaacha kufanya hivo, basi ni madhalimu wakubwa na wenye kuasi maamrisho ya Allaah.

[1] 04:58

[2] Tafsiyr al-´Ayyaashiy (1/246-247).

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Intisaar li Kitaab-il-´Aziyz al-Jabbaar, uk. 141
  • Imechapishwa: 23/11/2017