92. Mtu asitafute radhi za watu ikiwa kuna kumkasirisha Allaah

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Hili hukosea watu wengi. Wanasema: “Kwa hakika hii ni haki. Tunafahamu hili na tunashuhudia ya kwamba ni haki, lakini hatuwezi kulifanya na wala haijuzu [kutofautiana] na watu wa mji wetu isipokuwa kwa yale yanayoafikiana na wao”, au mfano wa nyudhuru kama hizo.

MAELEZO

Watu wengi wanajua haki katika suala hili. Wanasema kuwa wanajua kuwa haya ni haki lakini hawawezi kuyafanya kwa sababu yanaenda kinyume na yale waliyomo watu wa miji yao. Vilevile wanakuja na nyudhuru nyinginezo. Allaah (´Azza wa Jall) hatowapa udhuru kwa hilo. Lililo la wajibu kwa mtu ni kujibidisha ili aweze kupata radhi za Allaah (´Azza wa Jall), hata kama yatawafanya watu kukasirika. Mtu asitafute kupata radhi za watu ikiwa hilo linamkasirisha Allaah (´Azza wa Jall). Hili linakumbushia wale ambao walikuwa wakijadili kwa yale waliyokuwemo mababu zao. Allaah ameeleza kuwa wamesema:

إِنَّا وَجَدْنَا آبَاءَنَا عَلَىٰ أُمَّةٍ وَإِنَّا عَلَىٰ آثَارِهِم مُّهْتَدُونَ

“Hakika sisi tumewakuta baba zetu juu ya dini na hakika sisi tunaongoka kwa nyayo zao.” (43:22)

وَكَذَٰلِكَ مَا أَرْسَلْنَا مِن قَبْلِكَ فِي قَرْيَةٍ مِّن نَّذِيرٍ إِلَّا قَالَ مُتْرَفُوهَا إِنَّا وَجَدْنَا آبَاءَنَا عَلَىٰ أُمَّةٍ وَإِنَّا عَلَىٰ آثَارِهِم مُّقْتَدُونَ

“Na hivyo ndivyo hatukutuma kabla yako katika mji mwonyaji yeyote yule isipokuwa wamesema matajiri wake wenye starehe na taanusi: “Hakika sisi tumewakuta baba zetu juu ya dini, na hakika sisi kwa nyayo zao ni wenye kufuata.”” (43:23)

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 100-101
  • Imechapishwa: 28/11/2023