91. Wajibu wa kuitekeleza Tawhiyd kwa moyo, ulimi na kwa vitendo

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Mlango wa kumi na sita

Wajibu wa kuitekeleza Tawhiyd kwa moyo, ulimi na kwa vitendo

Tunahitimisha maneno – Allaah (Ta´ala) akitaka – kwa masuala makubwa ambayo ni muhimu sana yanayofahamika kupitia yale tuliyotangulia kuyataja. Lakini tutayagawa kutokana na ukubwa wake na kutokana na makosa yanayofanywa kwayo.

Tunasema: “Hakuna tofauti ya kwamba Tawhiyd ni lazima iwe kwa moyo, ulimi na matendo. Mtu akiacha kitu katika haya, hawi muislamu. Akiijua Tawhiyd na asiifanyie kazi, ni kafiri mwenye ukaidi, kama kufuru ya Fir´awn na Ibliys na mfano wao.

MAELEZO

Mtunzi anamalizia hoja tata hizi kwa mambo makubwa. Mambo haya ni kwamba ni lazima kwa mtu awe mpwekeshaji kwa moyo, maneno na matendo yake. Akiwa ni mpwekeshaji ndani ya moyo wake pasi na maneno na matendo yake, atakuwa sio mkweli katika madai yake. Upwekeshaji wa moyo unafuatwa na upwekeshaji wa maneno na vitendo. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Hakika katika kiwiliwili kuna kiungo. Kikitengemaa, basi kiwiliwili kizima kinatengemaa. Kikiharibika, basi kiwiwili kizima kinaharibika. Nacho ni moyo.”

Akidai kwamba yeye anampwekesha Allaah kwa moyo wake pasi na maneno na matendo yake, ni miongoni mwa Fir´awn na watu mfono wake ambao waliendelea kukufuru na kufanya ukaidi pamoja na kuwa anajua haki. Aliendelea katika hali yake na akasema kuwa eti ni mola. Allaah (Ta´ala) amesema:

وَجَحَدُوا بِهَا وَاسْتَيْقَنَتْهَا أَنفُسُهُمْ ظُلْمًا وَعُلُوًّا

“Wakazikanusha na hali kuwa nafsi zao zimeziyakinisha kwa dhuluma na majivuno.” (27:14)

Amesema (Ta´ala) kuwa Muusa alimwambia Fir´awn:

لَقَدْ عَلِمْتَ مَا أَنزَلَ هَـٰؤُلَاءِ إِلَّا رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ بَصَائِرَ

“Kwa hakika umekwishajua kwamba hakuna Aliyeteremsha haya isipokuwa Mola wa mbingu na ardhi kuwa ni dalili za kuonekana dhahiri.” (17:102)

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 100
  • Imechapishwa: 28/11/2023