89. Uombezi wa Mtume kwa Maswahabah wakati wa uhai wake

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Likithibiti hilo, mtu ataona kwamba kuwaomba kwao msaada Mitume siku ya Qiyaamah lengo wanataka kutoka kwao wamuombe Allaah awafanyie hesabu watu, ili watu wa Peponi watolewe katika kisimamo cha hali nzito. Na hili ni jambo linajuzu duniani na Aakhirah. Ni mfano wa kumuendea mtu mwema aliye hai akakaa na wewe na kusikiliza maneno yako, halafu ukamwambia: “Niombee kwa Allaah”, kama jinsi Maswahabah wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) walivyokuwa wakimuomba hilo katika uhai wake. Ama baada ya kufa kwake, hawakumuomba kamwe kwenye kaburi lake, bali as-Salaf as-Swaalih wamekataza kwa mwenye kukusudia kumuomba Allaah kwenye kaburi lake [Mtume]. Vipi tusemeje kumuomba yeye mwenyewe (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam)?

MAELEZO

Hili ni jibu la pili. Watu watawaomba msaada Mitume ili wamuombe Allaah (´Azza wa Jall) ili awapumzishe viumbe kutoka katika kisimamo hiki kizito. Huku sio kuwaomba wao, bali watawaomba wamuombe Allaah (´Azza wa Jall). Hiki ni kitendo kinachojuzu. Maswahabah (Radhiya Allaahu ´anhum) walikuwa wakimuomba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) awaombee. Katika “as-Swahiyh” ya al-Bukhaariy na ya Muslim wamepokea kwamba Anas (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kuwa kuna mtu aliingia msikitini siku ya ijumaa na Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akikhutubu. Akasema:

“Ee Mtume wa Allaah! Mali zimeangamia na njia zimekatika. Muombe Allaah atuteremshie mvua.”

Hakumwambia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) awanyeshelezee. Alimuomba amuombe du´aa Allaah ili aweze kuwanyeshelezea. Ndipo Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akanyanyua mikono yake juu na kusema:

“Ee Allaah! Tupe mvua.”

Alikariri hivo mara tatu. Ndipo Allaah (Subhaanahu wa Ta´ala) akafanya mvua kunyesha. Kulipita wiki nzima na jua halionekani mvua inaendelea kunyesha. Ijumaa iliofuata akaja msikitini mtu yuleyule, au mwingine, na kusema:

“Ee Mtume wa Allaah! Mali inaangamia na nyumba zinabomoka. Muombe Allaah (Ta´ala) asitishe mvua.” Akanyanyua mikono yake na kuomba: “Ee Allaah! [Ifanye inyeshe] pembezoni mwetu na si juu yetu. Ee Allaah! [Ifanye inyeshe] kwenye milima, mabonde na miti mikubwa na midogo.”[1]

Mvua ikawa imesita na Maswahabah wakatoka kwenda na huku jua likiangaza.

Hili ni katika kumuomba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amuombe Allaah (´Azza wa Jall). Haihusiani na kumuomba Mtume wa Allaah wala kumuomba msaada. Hapa itabainika kuwa hoja tata hii wanaobabaisha kwayo watu hawa haiwafai kitu. Uhalisia ni kwamba ni hoja tata isiokuwa na maana yoyote mbele ya Allaah (´Azza wa Jall).

Halafu mtunzi (Rahimahu Allaah) akataja kuwa inajuzu kumuomba mja mwema akuombee du´aa kwa Allaah. Hii ni haki. Pamoja na hivyo mtu asichukulie hayo yakawa ni mazowea yake. Haya hayakuwa ni mazowea ya Salaf (Radhiya Allaahu ´anhum). Hali kadhalika kitendo hichi kina kutegemea du´aa za wengine. Ni jambo lenye kujulikana kwamba lililo bora zaidi ni mtu kumuomba Mola Wake mwenyewe, kwa sababu kitendo hicho ni ´ibaadah anachojikurubisha kwacho mbele ya Allaah (´Azza wa Jall). Kwani hakika du´aa ni ´ibaadah. Allaah (Ta´ala) amesema:

وَقَالَ رَبُّكُمُ ادْعُونِي أَسْتَجِبْ لَكُمْ ۚ إِنَّ الَّذِينَ يَسْتَكْبِرُونَ عَنْ عِبَادَتِي سَيَدْخُلُونَ جَهَنَّمَ دَاخِرِينَ

“Na Mola wenu Amesema: “Niombeni, Nitakuitikieni. Hakika wale wanaotakabari na ‘ibaadah Yangu wataingika [Moto wa] Jahannam hali ya kuwa ni wadhalilifu.” (40:60)

Mtu akimuomba Mola Wake mwenyewe, basi analipwa kwa kitendo hichi. Isitoshe anamtegemea Allaah (´Azza wa Jall) ili kufikia manufaa na kuepuka madhara. Hili halihusiani na yule mwenye kuwaomba wengine wamuombee kwa Allaah. Mtu kama huyo anawategemea hao wengine kuliko Mola na hali kadhalika atawaelekea wengine zaidi kuliko anavyomuelekea Allaah (´Azza wa Jall). Hili ni jambo la khatari. Shaykh-ul-Islaam (Rahimahu Allaah) amesema:

“Mtu kumuomba mwengine amuombee du´aa ni katika mambo yenye kusimangwa.”

Endapo mtu atamuomba mwengine amuombee, basi anatakiwa anuie kumnufaisha huyo mwingine kwa maombi hayo. Analipwa thawabu kwa hilo na pengine akapata kile kilichotajwa katika Hadiyth:

“Hakuna muislamu anayemuombea ndugu yake nyuma ya mgongo wake, isipokuwa Malaika husema: “Aamiyn! Nawe pia upewe mfano wake.””[2]

[1] al-Bukhaariy (1016) na Muslim (897).

[2] Muslim (2732) na Abu Daawuud (1534).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 98-99
  • Imechapishwa: 28/11/2023