Faida ya tatu: Msomaji anaona pia kwamba neno “bwana” (سيد) hakuna katika du´aa za kumsifu. Kwa ajili hiyo wanachuoni waliokuja nyuma wametofautiana juu ya uweko wake katika Shari´ah. Hakuna muda wa kuchambua kwa undani juu ya maudhui haya na kuwataja wale ambao hawaonelei kuwa jambo hilo limewekwa katika Shari´ah. Sisi tunafuata mafunzo kamilifu ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa Ummah wake. Wakati alipoulizwa ni vipi inatakiwa kumsifu (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), akaamrisha kusema:

اللهم صل على محمد

“Ee Allaah! Msifu Muhammad… “

Vilevile napenda kumnukulia msomaji maoni ya Haafidhw Ibn Hajar al-´Asqalaaniy juu maudhui haya. Haya kwa kuzingatia kwamba ni mmoja katika wanachuoni wakubwa wa Shaafi´iyyah ambaye anamairi vyema Hadiyth na Fiqh. Ni jambo lililoenea kati ya Shaafi´iyyah waliokuja nyuma kwenda kinyume na mafunzo haya ya kinabii na matukufu.

Haafidhw Muhammad bin Muhammad bin Muhammad al-Gharaabiyliy (mwanafunzi wa Ibn Hajar) amesema:

“Aliulizwa (Haafidhw Ibn Hajar) ni vipi Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anatakiwa kusifiwa ndani ya swalah na nje ya swalah, ni mamoja tuseme kuwa ni wajibu au ni jambo tu lililopendekezwa. Je, ni sharti kuweka neno “bwana” kwa mfano kusema:

“Ee Allaah! Msifu bwana wetu Muhammad, bwana wa viumbe au bwana wa wanadamu.?”

Au mtu atosheke kusema:

اللهم صل على محمد

“Ee Allaah! Msifu Muhammad… “?

Ni lipi bora kati ya mawili hayo? Mtu ataje neno “bwana” kwa sababu ni sifa imethibiti kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), au mtu asilitaje kwa sababu halikupokelewa katika mapokezi? Akajibu (Radhiya Allaahu ´anh):

“Ndio, kufuata na kushikamana na matamshi yaliyopokelewa ni jambo lenye uzito zaidi. Haitakiwi kwa mtu kusema kwamba huenda (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliacha kulitumia neno hilo kwa sababu ya unyenyekevu kama ambavyo hakuwa na mazowea ya kujiombea swalah na salamu wakati anapojitaja mwenyewe. Ummah wake wameamrishwa kusema hivo kila pale (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anapotajwa. Lau kama hilo lingekuwa na uzito zaidi basi lingepokelewa na Maswahabah na Taabi´uun. Pamoja kuwepo kwa mapokezi mengi sikupata upokezi wowote kutoka kwa mmoja katika Maswahabah wala Taabi´uun kwamba alisema hivo. Imaam ash-Shaafi´iy (ambaye ni mmoja katika wale wenye kumuadhimisha Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema katika utangulizi wa kitabu chake ambacho ni nguzo katika madhehebu yake:

“Ee Allaah! Msifu Muhammad… kila anapotajwa na wale wenye kukumbuka na kila anaposahaulika na wale wenye kusahau.”

Ni kama kwamba ameyachambua hayo kutoka kwenye Hadiyth Swahiyh inayosema:

سبحان الله عدد خلقه

“Allaah ametakasika kutokamana na mapungufu kwa idadi ya viumbe Wake.”

Imethibiti kwamba (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alisema kumwambia mama wa waumini baada ya kumuona namna anavyomsabihi Allaah kwa wingi na kwa muda mrefu:

“Baada yako nimetaja maneno matatu. Lau yangelitiwa kwenye mzani pamoja na yale uliyosema basi yangeliyashinda uzito:

سبحان الله عدد خلقه سبحان الله رضا نفسه سبحان الله زنة عرشه سبحان الله مداد كلماته

“Ametakasika Allaah kwa idadi ya viumbe Wake. Ametakasika Allaah kama anavyoridhia Mwenyewe. Ametakasika Allaah ilivyo nzito ´Arshi Yake. Ametakasika Allaah kwa idadi ya maneno Yake.”

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akipendezwa na du´aa zilizo fupi zenye maana pana.

al-Qaadhwiy ´Iyaadhw ameweka mlango kwenye kitabu “ash-Shifaa” unaozungumzia ni namna gani Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) anatakiwa kusifiwa. Ndani yake ametaja mapokezi mengi kutoka kwa Maswahabah na Taabi´uun na hakuna Swahabah hata mmoja wala mwingine yeyote aliyetumia neno “bwana wetu”. Mmoja wao ni ´Aliy (Radhiya Allaahu ´anh) ambaye alikuwa akiwafunza watu namna ya kumsifu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ifuatavyo:

“Ee Allaah! Ambaye umeitandaza ardhi na kuziinua mbingu. Ziweke sifa Zako zilizotangulia, baraka Zako za zaidi na zizidishe salamu Zako kwa mja na Mtume Wako Muhammad – ambaye amefunga vilivyofungwa.”

´Aliy amesema vilevile:

“Sifa za Allaah, Muumbaji na Mwenye kurehemu, Malaika waliokurubishwa, Mitume, wakweli, mashahidi na waja wema na kila chenye kukutakasa kutokamana na mapungufu, ee Mola wa walimwengu, zimwendee Muhammad bin ´Abdillaah ambaye ndiye Mtume wa mwisho na kiongozi wa wachaji.”

´Abdullaah bin Mas´uud alikuwa akisema:

“Ee Allaah! Ziweke sifa Zako, baraka Zako na rehema Zako kwa mja na Mtumne Wako Muhammad – kiongozi bora na Mtume wa huruma.”

al-Hasan al-Baswriy alikuwa akisema:

“Anayetaka kunywa kwenye kikombe kinachokata kiu kutoka kwenye hodhi ya mteule (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) basi aseme: “Ee Allaah! Msifu Muhammad, jamaa zake, Maswahabah wake, wakeze, watoto wake, kizazi chake, watu wa nyumbani kwake, wakweze, wasaidizi wake, wafuasi wake na wapenzi wake.”

Haya ni baadhi ya mapokezi yaliyomo katika “ash-Shifaa” kutoka kwa baadhi ya Maswahabah na wengineo kuhusu kumsifu. Ni kweli kwamba imepokelewa kuwa Ibn Mas´uud (Radhiya Allaahu ´anh) alisema pindi alipomsifu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Ee Allaah! Ziweke bora ya sifa, rehema na baraka Zako juu ya bwana wa Mitume… “

Ameipokea Ibn Maajah. Lakini cheni ya wapokezi wake ni dhaifu. Upokezi wa ´Aliy uliotangulia ameupokea at-Twabaraaniy kwa cheni ya wapokezi isiyokuwa na neno. Ndani yake kuna matamshi ya kigeni niliyoyapokea katika kitabu “Fadhwl-un-Nabiy (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) cha Abul-Hasan bin Faaris”.

Shaafi´iyyah wamesema kwamba mtu akiapa kuwa atamsifu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa njia ilio bora kabisa, basi inatosha kwake kusema:

“Ee Allaah! Msifu Muhammad kila anapotajwa na wale wenye kukumbuka na kila anaposahaulika na wale wenye kusahau.”

an-Nawawiy amesema:

“Usawa ambao unatakiwa kukatwa ni kusema:

…اللهم صل على محمد و على آل محمد كما صليت على إبراهيم

“Ee Allaah! Msifu Muhammad, jamaa zake na Muhammad kama Ulivyomsifu Ibraahiym… “”

Wanachuoni wengi wamemkosoa kwa jambo hilo kwa sababu katika jumla hizo mbili hakuna kitu kinachofahamisha juu ya ubora inapokuja katika matamshi yenyewe. Ama inapokuja katika maana bora ubora ni wenye kudhihiri katika ile ya kwanza. Masuala haya ni yenye kutambulika katika vitabu vya Fiqh. Kikusudiwacho kwa haya yote ni kwamba hakuna mwanachuoni yeyote aliyezungumzia maudhui haya ambaye alitaja neno “bwana wetu” (سيدنا). Lau ziada hii ingelikuwa imependekezwa basi isingefichikana kwao wote. Kheri yote inapatikana katika kufuata.”

Maoni ya Haafidhw Ibn Hajar (Rahimahu Allaah) kwamba haikuwekwa katika Shari´ah kumtaja (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa njia ya ubwana wakati wa kumsifu na vilevile ndio maoni ya Hanafiyyah. Ndio ambayo yanapaswa kufuatwa kwa sababu ndio dalili ya kweli juu ya kumfuata (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“qul inkuntum…ghafuru rahim” 03:31

Kwa ajili hiyo Imaam an-Nawawiy amesema katika “Rawdhwat-ut-Twaalibiyn”:

“Kumsifu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kuliko kukamilifu ni kusema:

اللهم صل على محمد و على آل محمد كما صليت على إبراهيم [و آل إبراهيم]، إنك حميد مجيد. و بارك على محمد و على آل محمد كما باركت على [إبراهيم و]آل إبراهيم، إنك حميد مجيد

“Ee Allaah! Msifu Muhammad, jamaa zake Muhammad kama Ulivyomsifu Ibraahiym [na jamaa zake Ibraahiym]. Kwani hakika Wewe ni Mwenye kuhidimiwa na Mwenye kutukuzwa. Ee Allaah! Na mbariki Muhammad, jamaa zake Muhammad kama Ulivyombariki [Ibraahiym] na jamaa zake Ibraahiym. Kwani hakika Wewe ni Mwenye kuhidimiwa na Mwenye kutukuzwa.””[1]

Ile sifa ya tatu na hakutaja ndani yake bwana.

[1] Rawdhat-ut-Twaalibiyn (1/265).

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swifatu Swalaat-in-Nabiy, uk. 149-152
  • Imechapishwa: 07/01/2019