84. Uwajibu wa kumpenda Allaah na Mtume na yale waliyokuja nayo

Mapenzi ya kumpenda Allaah (´Azza wa Jall) ndio aina kubwa kabisa ya ´ibaadah. Kisha kunafuatia mapenzi ya kumpenda Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kupenda Sunnah zake. Mapenzi ya kumpenda Allaah na mapenzi ya kumpenda Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) yanapelekea kupenda yale yaliyokuja kutoka kwa Allaah na kwa Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kuchukia kitu katika yale yaliyokuja kutoka kwa Allaah au kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) yanapelekea kumbughudhi Allaah au Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Huku ni kuritadi na kumkufuru Allaah (´Azza wa Jall).

Hivyo ni wajibu kwa muislamu kupenda yale yaliyokuja kutoka kwa Allaah katika Qur-aan na apende yale yaliyokuja kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hayo yanakuwa baada ya kumpenda Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kuipenda dini hii. Akichukia kitu katika hayo, basi hii ni dalili ya kutokuwa na imani.

Ijapokuwa atakifanya… – Bi maana hawi muumini. Kwa ajili hiyo wanafiki walipokuwa wanamchukia Allaah na kumchukia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), walikuwa wakichukia Wahy unaoteremshwa na wala hawautaki. Amesema (Subhaanah):

وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ تَعَالَوْا إِلَىٰ مَا أَنزَلَ اللَّـهُ وَإِلَى الرَّسُولِ رَأَيْتَ الْمُنَافِقِينَ يَصُدُّونَ عَنكَ صُدُودًا

“Wanapoambiwa: “Njooni katika yale aliyoyateremsha Allaah na kwa Mtume, basi utawaona wanafiki wanakugeuka kikwelikweli.”(an-Nisaa´ 04:60-61)

Kwa nini wanakengeuka? Kwa sababu wanaichukia Qur-aan na Sunnah. Hata kama kwa uinje watayafanyia kazi, lakini wanayachukia hayo ndani ya mioyo yao. Kuyafanya kwao kwa uinjenje ni hambo halisaidii kitu. Kwa sababu ni unafiki na ngao. Vinginevyo ndani ya mioyo yao wanaichukia Qur-aan na Sunnah. Kwa ajili hiyo ndio maana Allaah akawahukumu ukafiri na akawafanya kuwa katika tabaka ya chini kabisa Motoni, pamoja na kwamba kwa uinje wanaitendea kazi Qur-aan na Sunnah. Lakini midhali wanayachukia hayo katika nyoyo zao wakawa ni makafiri wabaya mno na adhabu yao ikawa mbaya kabisa. Wao watakuwa katika tabaka ya chini kabisa Motoni.

Kuhusu wale makafiri wa asili wao kimsingi ni kwamba wanachukia nyujumbe na wanachukia Vitabu. Amesema (Ta´ala):

وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ تَعَالَوْا إِلَىٰ مَا أَنزَلَ اللَّـهُ وَإِلَى الرَّسُولِ قَالُوا حَسْبُنَا مَا وَجَدْنَا عَلَيْهِ آبَاءَنَا

”Wanapoambiwa: “Njooni katika yale aliyoyateremsha Allaah na kwa Mtume”, basi husema: “Yanatutosheleza yale tuliyowakuta nayo baba zetu”. (al-Maaidah 104)

Wanasema yanatutosheleza yale tuliyowakuta nayo baba zetu katika desturi mbalimbali, kufuata kichwa mchunga na maoni na hukumu za kipindi cha kikafiri. Katika Aayah nyingine imekuja:

وَإِذَا قِيلَ لَهُمُ اتَّبِعُوا مَا أَنزَلَ اللَّـهُ قَالُوا بَلْ نَتَّبِعُ مَا أَلْفَيْنَا عَلَيْهِ آبَاءَنَا ۗ أَوَلَوْ كَانَ آبَاؤُهُمْ لَا يَعْقِلُونَ شَيْئًا وَلَا يَهْتَدُونَ

”Wanapoambiwa: “Fuateni yale aliyoyateremsha Allaah” basi husema: “Bali tunafuata tuliyowakuta nayo baba zetu.” – je, japokuwa baba zao walikuwa hawaelewi kitu chochote na wala hawaongoki?” (al-Baqarah 02:170)

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Nawaaqidh-il-Islaam, uk. 111-113
  • Imechapishwa: 20/11/2018