82. Radd kwa anayedai ya kwamba mtu amuache mwenye kusema “hakuna mungu wa haki ila Allaah” hata kama atafanya kitu cha kumtoa katika Uislamu

Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Mlango wa kumi na nne

Radd kwa anayedai ya kwamba mtu amuache mwenye kusema “hakuna mungu wa haki ila Allaah” hata kama atafanya kitu cha kumtoa katka Uislamu

Washirikina wana hoja tata nyingine nyingine. Wanasema: “Kwa hakika Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimkataza Usaamah pindi alipomuua mtu aliyesema: “Hakuna mungu wa haki isipokuwa Allaah”. Na akamwambia:

“Hivi kweli umemuua baada ya yeye kusema “Hakuna mungu wa haki isipokuwa Allaah?” Hali kadhalika amesema:

“Nimeamrishwa kuwapiga vita watu mpaka watakaposema “Hakuna mungu wa haki isipokuwa Allaah.”

Vilevile kuna Hadiyth zingine zinazozungumzia kukomeka [kumsalimisha] kwa yule mwenye kuitamka.

Makusudio ya hawa wajinga ni kwamba mwenye kuitamka hawezi si kukufuru wala kuuawa, walau atafanya yakufanya.

MAELEZO

Mbali na zile hoja tata nyenginezo zilizotangulia, washirikina wana hoja tata nyingine. Wanasema kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alimkaripia Usaamah bin Zayd (Radhiya Allaahu ´anh) baada ya kumuua mtu aliyesema “Hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah.” Akamwambia:

“Hivi kweli umemuua baada ya yeye kusema “Hakuna mungu wa haki isipokuwa Allaah?”

Akaendelea (´alayhis-Swalaatu was-Salaam) kusema hivo mpaka Usamaah akasema:

“Nilitamani ningekuwa bado sijawa muislamu.”[1]

Vivyo hivyo amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Nimeamrishwa kuwapiga vita watu mpaka watakaposema “Hakuna mungu wa haki isipokuwa Allaah.”[2]

Kuna Hadiyth nyenginezo wanazotumia kama dalili juu ya kwamba yule mwenye kusema “Hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah” hawezi kukufuru wala kuritadi. Wanasema hivi hata kama mtu atakuwa ni mwenye kushirikisha kwa mitazamo mingine. Huu ni ujinga wa kupindukia. Neno “Hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah” hayamuokoi mtu na Moto wala kumsalimisha mtu na kutumbukia katika shirki ikiwa anashirikisha kwa njia nyinginezo.

[1] al-Bukhaariy (4269) na Muslim (159).

[2] al-Bukhaariy (1399) na Muslim (32).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kashf-ish-Shubuhaat, uk. 91-92
  • Imechapishwa: 28/11/2023