8. Wanawake bora zaidi walikuwa wakijifunika nyuso zao

3- Kauli ya Allaah (Ta´ala):

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ قُل لِّأَزْوَاجِكَ وَبَنَاتِكَ وَنِسَاءِ الْمُؤْمِنِينَ يُدْنِينَ عَلَيْهِنَّ مِن جَلَابِيبِهِنَّ ۚ ذَٰلِكَ أَدْنَىٰ أَن يُعْرَفْنَ فَلَا يُؤْذَيْنَ ۗ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا

“Ee Nabii! Waambie wake zako na mabinti zako – na wanawake [wote] wa Waumini – ya kwamba [nje ya nyumbani] wajiteremshie mavazi yao ya juu; hivyo kunapeleka karibu zaidi watambulikane [kuwa ni wanawake wa heshima] na wasiudhiwe. Na Allaah ni Mwingi wa kusamehe, Mwenye kurehemu.”[1]

Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anhumaa) amesema:

“Allaah amewaamrisha wanawake pindi wanapotoka majumbani wafunike nyuso zao kwa mavazi yao ya juu na waoneshe jicho moja tu.”[2]

Tafsiyr ya Swahabah ni hoja. Kuna wanachuoni waliyofikia mpaka kusema kuwa ina hukumu moja kama ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Kauli yake (Radhiya Allaahu ´anh) “… na waoneshe jicho moja tu” ni kwa sababu tu amelazimika kuona njia. Ama ikiwa hana haja hiyo, hafai hata kuonesha jicho hilo. Mavazi ya juu, Jilbaab, ni yale yanayowekwa juu ya kichwa. Umm Salamah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesema baada ya kuteremka Aayah hii:

“Wanawake wa Answaar walitoka walikuwa watulivu kana kwamba kunguru amekaa juu ya vichwa vyao. Walikuwa wamevaa mavazi ya juu meusi.”[3]

´Abiydah as-Salmaaniy na wengine wameeleza jinsi wanawake waumini walivokuwa na mavazi yao juu ya vichwa vyao ili kusionekana chochote zaidi ya macho yao tu kwa ajili ya njia.

[1] 33:59

[2] Tazama ”Tafsiyr al-Qur-aan al-´Adhwiym” ya Ibn Kathiyr (3/569).

[3] Ameipokea Ibn Abiy Haatim, kama ilivyotajwa katika ”Tafsiyr al-Qur-aan al-´Adhwiym” ya Ibn Kathiyr (2/569).

  • Mhusika: Imaam Muhammad bin Swaalih bin ´Uthaymiyn
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Hijaab, uk. 11-12
  • Imechapishwa: 26/03/2017