79. Mtazamo wa Khawaarij na Mu´tazilah juu ya mtenda dhambi kubwa

Khawaarij wanasema kuwa mtenda dhambi kubwa ni kafiri na kwamba ametoka katika Uislamu. Wanaona kuwa akifa pasi na kutubia atadumishwa Motoni kama makafiri.

Mu´tazilah wanasema kuwa anatoka katika imani na wakati huohuo hawaonelei kuwa ameingia katika ukafiri. Wanaona kuwa yuko katika daraja kati ya daraja mbili. Lakini akifa pasi na kutubia atadumishwa Motoni milele. ´Aqiydah zote mbili ni batili na zinatofautiana na dalili. Allaah (Jalla wa ´Alaa) anasema:

إِنَّ اللَّـهَ لَا يَغْفِرُ أَن يُشْرَكَ بِهِ وَيَغْفِرُ مَا دُونَ ذَٰلِكَ لِمَن يَشَاءُ

“Hakika Allaah hasamehi kushirikishwa na anasamehe yaliyo chini ya hayo kwa Amtakae.” (04:48)

Kadhalika imekuja katika Hadiyth:

“Ambaye ndani ya moyo wake mna imani ndogo ndogo ndogo kabisa sawa na mbegu ya hardali atatolewa Motoni.”[1]

Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Na hiyo ni imani dhaifu kabisa.”[2]

Atatoka baada ya kuungua na hali ya kuwa ameshakuwa mkaa. Halafu atawekwa kwenye mto wa Peponi na uchipuke mwili wake kama inavyochipuka mbegu. Baada ya hapo ataingizwa Peponi.

Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema:

“… kutoka Motoni miili iliyoungua na itatupwa.”

Viwiliwili vyao vitaungua na kuwa makaa kutokana na adhabu. Allaah (Jalla wa ´Alaa) atavirudishia viwiliwili hivyo uhai na baada ya hapo waingie Peponi.

Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema:

“[Iwekwe] kwenye mto wa Firdaws… ”

Firdaws ndio Pepo ilio juu kabisa na katikati ya Pepo ambapo mto huyu unapita kuanzia hapo.

Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema:

“… kama vile punje iliyobebwa… ”

Kama ilivyokuja katika Hadiyth Swahiyh:

“Mpaka watapokuwa makaa wataidhinishwa uombezi. Yaje makundi kwa makundi yaliyoungua ambapo yatawekwa kwenye mito ya Peponi. Kisha kusemwe: “Enyi watu wa Peponi! Wapeni [nafasi].” Ndipo watachipuka kama mbegu inavyokuwa kwenye kokwa lake.””[3]

Watawekwa kwenye mto miongoni mwa mito ya Peponi unaoitwa ´mto wa uhai`. Wahuike kama inavyohuika mbegu iliyobebwa kwenye kokwa lake.

[1] al-Bukhaariy (7510) na Muslim (193)

[2] Muslim (78) na (49)

[3] Muslim (306) na (185)

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh al-Mandhuumat-ul-Haaiyyah fiy ´Aqiydati Ahl-is-Sunnah wal-Jamaa´ah, uk. 170-159
  • Imechapishwa: 13/01/2024