79. al-Qummiy upotoshaji wake wa kumi na moja wa Aal ´Imraan

al-Qummiy amesema:

“Kisha akamtaja kiongozi wa waumini na wafuasi wake waumini na akasema:

فَالَّذِينَ هَاجَرُوا وَأُخْرِجُوا مِن دِيَارِهِمْ وَأُوذُوا فِي سَبِيلِي وَقَاتَلُوا وَقُتِلُوا لَأُكَفِّرَنَّ عَنْهُمْ سَيِّئَاتِهِمْ وَلَأُدْخِلَنَّهُمْ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ ثَوَابًا مِّنْ عِندِ اللَّـهِ ۗ وَاللَّـهُ عِندَهُ حُسْنُ الثَّوَابِ

“Basi wale waliohajiri na wakatolewa majumbani mwao na wakaudhiwa katika njia Yangu wakapigana na wakauliwa, bila shaka Nitawafutia makosa yao na Nitawaingiza kwenye mabustani yapitayo chini yake mito – ni thawabu kutoka kwa Allaah; na kwa Allaah ndiko kuna thawabu nzuri kabisa.”[1]

Bi maana kiongozi wa waumini, Salmaan na Abu Dharr waliotimuliwa.”[2]

Tazama upotoshaji huu! Aayah inamuhusu Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah zake ambao walitolewa Makkah na wakahama kwenda al-Madiynah, wakapigana na wakauawa. Raafidhwah wanaikengeusha Aayah ili imlenge tu ´Aliy na wafuasi zake Salmaan na Abu Dharr. Lakini Salmaan hakuhajiri na wala hakufukuzwa kutoka katika mji wake. Hali kadhalika Abu Dharr (Radhiya Allaahu ´anh) hakufukuzwa kutoka katika mji wake. Karibu watu wake wote walisilimu kabla ya kuhama kwenda al-Madiynah. Pengine Raafidhwiy huyu anamaanisha alipohama kwenda ar-Rabadhah. Kama ni hivyo alihama mwenyewe kwa kupenda kwake. Kwa hali yoyote Aayah hii haihusiani na haya ambayo wanaashiria waongo hawa kwa sababu alihama kwenda ar-Rabadhah miaka thelathini baada ya Hijrah.

Aayah inawahusu Muhaajiruun wote wa Maswahabah wa Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambao waliiacha miji yao na mali yao kwa ajili ya Allaah na wakapambana wakiwa bega kwa bega na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na wakamnusuru:

لِلْفُقَرَاءِ الْمُهَاجِرِينَ الَّذِينَ أُخْرِجُوا مِن دِيَارِهِمْ وَأَمْوَالِهِمْ يَبْتَغُونَ فَضْلًا مِّنَ اللَّـهِ وَرِضْوَانًا وَيَنصُرُونَ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ ۚ أُولَـٰئِكَ هُمُ الصَّادِقُونَ

“[Katika ambao wanastahiki kupewa fai ni] mafuqara Muhaajiruun ambao wametolewa kutoka majumbani mwao na [zikataifishwa] mali zao wanatafuta fadhila na radhi kutoka kwa Allaah na wanamnusuru Allaah na Mtume Wake – hao ndio wakweli.” (59:08)

Huu ni mfano mmoja wa namna Allaah anavyowasifia. Lakini maadui wa Allaah wanataka kuibatilisha kwa sababu ya kuwa na chuki dhidi ya Allaah, Mtume Wake Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah zake na kumkadhibisha Allaah na Mtume Wake.

[1] 03:195

[2] Tafsiyr al-Qummiy (1/129).

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: al-Intiswaar li Kitaab-il-´Aziyz al-Jabbaar, uk. 116-117
  • Imechapishwa: 13/04/2017