78. ´Aqiydah ya Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah juu ya waislamu waliokufa katika dhambi kubwa

Imaam Ibn Abiy Daawuud (Rahimahu Allaah) amesema:

وقُلْ يُخرجُ اللهُ الْعظيمُ بِفَضلِهِ

30 – Sema “Allaah mtukufu ataitoa kwa fadhilah Zake

مِنَ النارِ أجْساداً مِنَ الفَحْمِ تُطرحُ

     kutoka Motoni miili iliyoungua na itatupwa

عَلى النهرِ في الفِرْدوسِ تَحْيَا بِمَائِهِ

31 – [Iwekwe] kwenye mto wa Firdaws ambapo itapata uhai kwa maji yake

كَحِبِّ حَمِيلِ السَّيْلِ إذْ جَاءَ يَطْفَحُ

     kama vile punje iliyobebwa na maji ya mafuriko yanapokuja yakiwa yanamiminika kwa wingi”

MAELEZO

Haya ni masuala kuhusu watenda maasi wanaomuabudu Allaah peke yake ambao wana madhambi makubwa chini ya shirki. Hawa wanazingatiwa kuwa ni waumini na wapwekeshaji. Lakini imani na Tawhiyd yao ni pungufu. Licha ya hivyo hawatoki katika Uislamu tofauti na wanavyoonelea Khawaarij na Mu´tazilah. Wako chini ya matakwa; iwapo Allaah atataka atawasamehe na hatowaadhibu na wataingia Peponi pale mwanzoni tu, na Allaah vilevile akitaka atawaadhibu. Lakini ikibidi hivo hawatodumishwa Motoni milele kama watavyodumishwa makafiri na washirikina. Watatolewa ndani ya Moto baada ya kuadhibiwa. Hilo litafanyika ima kutokana na uombezi wa waombezi, fadhilah za Allaah (´Azza wa Jall) au kwa kumalizika kwa adhabu yao. Hawatodumishwa Motoni milele kabisa.

Motoni ataingia kafiri na mshirikina. Kuna uwezekano vilevile muumini na muislamu anayemuabudu Allaah peke yake akaingia humo kutokana na madhambi yake. Lakini kafiri na mshirikina watadumishwa Motoni. Kuhusu mpwekeshaji na muumini hawatodumishwa humo milele ikiwa kama wataingia. Hii ndio ´Aqiydah ya Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah tofauti na wanavyoamini Khawaarij na Mu´tazilah.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh al-Mandhuumat-ul-Haaiyyah fiy ´Aqiydati Ahl-is-Sunnah wal-Jamaa´ah, uk. 169
  • Imechapishwa: 13/01/2024