Miongoni mwa mambo yanayopelekea kumwamini Allaah (Ta´ala) na kumwabudu ni kunyenyekea juu ya hukumu Yake, kuridhia Shari´ah Yake na kurejea katika Kitabu Chake na Sunnah za Mtume Wake wakati wa kutofautiana katika maneno, katika ´Aqiydah, katika magomvi, katika damu na mali na haki nyenginezo mbalimbali. Kwani Allaah ndiye Mwenye kuhukumu na Yeye ndiye ana haki ya kuhukumu. Kwa hivyo ni lazima kwa watawala kuhukumu kwa yale aliyoteremsha Allaah kama ambavo ni wajibu kwa raia kuhukumiana kwa yale aliyoteremsha Allaah katika Kitabu Chake na Sunnah za Mtume Wake. Allaah (Ta´ala) amesema kuhusu watawala:

إِنَّ اللَّـهَ يَأْمُرُكُمْ أَن تُؤَدُّوا الْأَمَانَاتِ إِلَىٰ أَهْلِهَا وَإِذَا حَكَمْتُم بَيْنَ النَّاسِ أَن تَحْكُمُوا بِالْعَدْلِ

“Hakika Allaah anakuamrisheni kurudisha amana kwa wenyewe na pindi mtakapohukumu kati ya watu, basi mhukumu kwa uadilifu.”[1]

Amesema kuhusu raia:

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا أَطِيعُوا اللَّـهَ وَأَطِيعُوا الرَّسُولَ وَأُولِي الْأَمْرِ مِنكُمْ ۖ فَإِن تَنَازَعْتُمْ فِي شَيْءٍ فَرُدُّوهُ إِلَى اللَّـهِ وَالرَّسُولِ إِن كُنتُمْ تُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ ۚ ذَٰلِكَ خَيْرٌ وَأَحْسَنُ تَأْوِيلًا

“Enyi walioamini! Mtiini Allaah na mtiini Mtume na wale wenye madaraka katika nyinyi. Mkizozana katika jambo lolote, basi lirudisheni kwa Allaah na Mtume mkiwa mnamuamini Allaah na siku ya Mwisho. Hivyo ni bora na matokeo mazuri kabisa.”[2]

Halafu akabainisha kuwa imani haikusanyiki pamoja na kuhukumu kinyume na yale aliyoteremsha Allaah. Amesema (Ta´ala):

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ يَزْعُمُونَ أَنَّهُمْ آمَنُواْ بِمَا أُنزِلَ إِلَيْكَ وَمَا أُنزِلَ مِن قَبْلِكَ يُرِيدُونَ أَن يَتَحَاكَمُواْ إِلَى الطَّاغُوتِ وَقَدْ أُمِرُواْ أَن يَكْفُرُواْ بِهِ وَيُرِيدُ الشَّيْطَانُ أَن يُضِلَّهُمْ ضَلاَلاً بَعِيدًا

”Je, huoni wale ambao wanadai kwamba wao wameamini yaliyoteremshwa kwako na yale yaliyoteremshwa kabla yako, wanataka wahukumiane kwa Twaaghuut na hali wameamrishwa wakanushe hiyo na shaytwaan anataka awapoteze upotevu wa mbali kabisa.”[3]

Mpaka pale aliposema (Ta´ala):

فَلَا وَرَبِّكَ لَا يُؤْمِنُونَ حَتَّىٰ يُحَكِّمُوكَ فِيمَا شَجَرَ بَيْنَهُمْ ثُمَّ لَا يَجِدُوا فِي أَنفُسِهِمْ حَرَجًا مِّمَّا قَضَيْتَ وَيُسَلِّمُوا تَسْلِيمًا

“Naapa kwa Mola wako! Hawatoamini mpaka wakufanye wewe [Mtume] ni hakimu katika yale wanayogombana kati yao kisha wasipate katika nyoyo zao uzito katika yale uliyohukumu na wajisalimishe kwa kujisalimisha”[4]

Hivyo (Subhaanah) akakanusha – tena makanusho yaliyoambatana na kiapo – imani  juu ya ambaye hahukumiwi kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), akaridhia hukumu yake na akasajilimisha nayo. Vilevile amewahukumu wale watawala wasiohukumu kwa yale aliyoteremsha Allaah kufuru, dhuluma na ufuska. Amesema (Ta´ala):

وَمَن لَّمْ يَحْكُم بِمَا أَنزَلَ اللَّـهُ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْكَافِرُونَ

“Yeyote asiyehukumu kwa yale aliyoyateremsha Allaah, basi hao ndio makafiri.”[5]

وَمَن لَّمْ يَحْكُم بِمَا أَنزَلَ اللَّـهُ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ

“Yeyote asiyehukumu kwa yale aliyoyateremsha Allaah, basi hao ndio madhalimu.”[6]

وَمَن لَّمْ يَحْكُم بِمَا أَنزَلَ اللَّـهُ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْفَاسِقُونَ

“Yeyote asiyehukumu kwa yale aliyoyateremsha Allaah, basi hao ndio mafasiki.”[7]

Ni lazima kuhukumu kwa yale aliyoteremsha Allaah na kuhukumiana kwayo katika mambo yote yanayotokea katika maneno yanayotokamana na Ijtihaad kati ya wanachuoni. Hiyo ina maana kwamba hayakubaliwi isipokuwa tu yale yenye ushahidi wa Qur-aan na Sunnah pasi na kuwa na kasumba za madhehebu, ubaguzi kwa imamu na katika magomvi mbalimbali katika haki zengine. Haihusiani na mambo ya kibinafsi peke yake, kama ilivyo katika baadhi ya nchi zinazojinasibisha na Uislamu. Uislamu unachukuliwa wotewote na si sehemusehemu. Amesema (Ta´ala):

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا ادْخُلُوا فِي السِّلْمِ كَافَّةً

“Enyi walioamini! Ingieni katika Uislamu kikamilifu.”[8]

أَفَتُؤْمِنُونَ بِبَعْضِ الْكِتَابِ وَتَكْفُرُونَ بِبَعْضٍ

”Je, mnaamini sehemu ya Kitabu na mnakanusha sehemu nyingine?”[9]

Vivyo hivyo ni lazima kwa wafuasi wa madhehebu na watu wa mifumo ya kisasa kuyarejesha maneno ya maimamu wao katika Qur-aan na Sunnah. Yale yatayoafikiana navyo, yachukuliwe, na yale yatayokwenda kinyume navyo, yarudishwe bila kuwa na ushabiki wala ubaguzi. Khaswakhaswa katika mambo ya ´Aqiydah. Hakika maimamu (Rahimahumu Allaah) wanausia jambo hilo na haya ndio madhehebu yao wote. Kwa hivyo yule mwenye kwenda kinyume nayo sio mfuasi wao ijapokuwa atajinasibisha nao. Isitoshe ataingia miongoni mwa wale Allaah amesema juu yao:

اتَّخَذُوا أَحْبَارَهُمْ وَرُهْبَانَهُمْ أَرْبَابًا مِّن دُونِ اللَّـهِ وَالْمَسِيحَ ابْنَ مَرْيَمَ

“Wamewafanya wanazuoni wa kiyahudi na watawa wao kuwa ni waungu badala ya Allaah na al-Masiyh, mwana wa Maryam.”[10]

Aayah haiwahusu manaswara peke yao. Bali inaenea kwa kila mwenye kufanya mfano wa matendo yao. Mwenye kwenda kinyume na yale aliyoamrisha Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwa njia ya kwamba akahukumu kati ya watu kwa yale ambayo Allaah hakuteremsha, akaomba kufanyiwa hivo kwa ajili ya kufuata yale anayotamani na kutaka, basi amevua kamba ya Uislamu na imani kutoka shingoni mwake ingawa atadai kuwa ni muumini. Hakika Allaah (Ta´ala) amewakemea wale wenye kufanya hivo na akawakadhibisha juu ya madai yao ya kuamini. Amesema (Ta´ala):

أَلَمْ تَرَ إِلَى الَّذِينَ يَزْعُمُونَ أَنَّهُمْ آمَنُواْ بِمَا أُنزِلَ إِلَيْكَ وَمَا أُنزِلَ مِن قَبْلِكَ يُرِيدُونَ أَن يَتَحَاكَمُواْ إِلَى الطَّاغُوتِ وَقَدْ أُمِرُواْ أَن يَكْفُرُواْ بِهِ وَيُرِيدُ الشَّيْطَانُ أَن يُضِلَّهُمْ ضَلاَلاً بَعِيدًا

”Je, huoni wale ambao wanadai kwamba wao wameamini yaliyoteremshwa kwako na yale yaliyoteremshwa kabla yako, wanataka wahukumiane kwa Twaaghuut na hali wameamrishwa wakanushe hiyo na shaytwaan anataka awapoteze upotevu wa mbali kabisa.”[11]

Ndani ya maneno Yake:

يَزْعُمُونَ

“Ambao wanadai.”

kuna kukanushwa imani yao. Mara nyingi mtu anaambiwa kuwa amedai pale anapodai madai ambayo ndani yake kuna uongo kwa sababu ya kwenda kwake kinyume na yanayowajibishwa na kutendea kazi yale yanayopingana nayo. Haya yanahakikiwa na maneno Yake:

وَقَدْ أُمِرُواْ أَن يَكْفُرُواْ بِهِ

“… hali wameamrishwa wakanushe hiyo.”

Kwa sababu kukufuru Twaaghuut  ni nguzo ya Tawhiyd, kama ilivyo katika Aayah ya al-Baqarah[12]. Isipopatikana nguzo hii mtu hawi mpwekeshaji. Tawhiyd ndio msingi wa imani matendo yote yanatengemaa juu yake na yanaharibika kwa kukosekana kwake. Kama yanavyobainika hayo katika maneno Yake:

فَمَن يَكْفُرْ بِالطَّاغُوتِ وَيُؤْمِن بِاللَّـهِ فَقَدِ اسْتَمْسَكَ بِالْعُرْوَةِ الْوُثْقَىٰ

“Basi atakayemkanusha Twaaghuut na akamuamini Allaah, hakika atakuwa ameshikilia imara kishikilio madhubuti.”[13]

Hayo ni kwa sababu kuhukumiana kwa Twaaghuut ina maana mtu anaiamini[14].

Kukanushwa kwa imani kwa yule asiyehukumu kwa yale aliyoteremsha Allaah ni dalili inayoonyesha kuwa kuhukumu kwa Shari´ah ya Allaah ni imani, ´Aqiydah na ni kumwabudu Allaah ambako muislamu anatakiwa akuamini. Asihukumu kwa Shari´ah ya Allaah kwa sababu tu kuhukumu kwayo kunasilihi zaidi kwa watu na kunaidhibiti zaidi amani. Kwani baadhi ya watu wanazingatia upande huu peke yake na wanasahau upande wa kwanza. Allaah (Subhaanah) amemtia dosari yule anayehukumu kwa Shari´ah ya Allaah kwa sababu ya manufaa ya nafsi peke yake pasi na kumwabudu Allaah (Ta´ala) kwa jambo hilo. Amesema (Subhaanah):

وَإِذَا دُعُوا إِلَى اللَّـهِ وَرَسُولِهِ لِيَحْكُمَ بَيْنَهُمْ إِذَا فَرِيقٌ مِّنْهُم مُّعْرِضُونَ وَإِن يَكُن لَّهُمُ الْحَقُّ يَأْتُوا إِلَيْهِ مُذْعِنِينَ

“Wanapoitwa kwa Allaah na Mtume Wake ili awahukumu kati yao, mara hapo kundi miongoni mwao wanapuuza. Na inapokuwa haki ni yao, basi wanamjia hali  ya kuwa ni wenye kutii.”[15]

 Hawatilii umuhimu isipokuwa yale wanayotamani. Yale yanayokwenda kinyume na matamanio yao wanayapa mgongo. Kwa sababu hawamwabudu Allaah kwa kule kuhukumiana kwa Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

[1] 04:58

[2] 04:59

[3] 04:60

[4] 04:65

[5] 05:44

[6] 05:45

[7] 05:47

[8] 02:208

[9] 02:85

[10] 09:31

[11] 04:60

[12] Anamaanisha maneno Yake (Ta´ala):

فَمَن يَكْفُرْ بِالطَّاغُوتِ وَيُؤْمِن بِاللَّـهِ فَقَدِ اسْتَمْسَكَ بِالْعُرْوَةِ الْوُثْقَىٰ

“Basi atakayemkanusha Twaaghuut na akamuamini Allaah, hakika atakuwa ameshikilia imara kishikilio madhubuti.” (02:256)

[13] 02:256

[14] Fath-ul-Majiyd, uk. 467-468.

[15] 24:48-49

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ´Aqiydat-ut-Tawhiyd, uk. 120-123
  • Imechapishwa: 26/03/2020