Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiifanya Sujuud yake kuwa ndefu kukaribia Rukuu´ yake. Wakati mwingine huenda kukatokea jambo na akairefusha zaidi. Swahabah mmoja amesema:

“Wakati mmoja katika mnasaba wa swalah ya mchana Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alitujia akiwa amembeba Hasan au Husayn. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akatangulia mbele na akamuweka upande wa mguu wake wa kulia. Kisha akaleta Takbiyr na tukaanza kuswali. Kisha akatumia muda mwingi katika Sujuud ambapo nikainua kichwa changu na kumuona mvulana akiwa juu ya mgongo wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Nikarudi kwenye Sujuud yangu. Pindi Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alipomaliza kuswali watu wakasema: “Ee Mtume wa Allaah! Hakika umetumia muda mwingi katika Sujuud mpaka tukadhania kuwa kumepitika jambo au umeteremshiwa Wahy.” Akasema: “Hakuna kilichopitika katika hayo. Mjukuu wangu alikuwa amekaa mgongoni mwangu na sikutaka kumsumbua mpaka atosheke.”[1]

Imekuja katika Hadiyth nyingine:

“Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiswali. Pindi aliposujudu al-Hasan na al-Husayn wakapanda juu ya mgongo wake. Watu wanapotaka kuwakataza anawaashiria (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wawaache. Alipomaliza kuswali akawaweka mapajani kwake na akasema: “Yule anayenipenda basi awapende wawili hawa.”[2]

[1] an-Nasaa’iy, Ibn ´Asaakir (4/257/1-2) na al-Haakim aliyeisahihisha na adh-Dhahabiy akaafikiana naye.

[2] Ibn Khuzaymah katika ”as-Swahiyh” (887) kwa mlolongo wa wapokezi mzuri kupitia kwa Ibn Mas´uud. al-Bayhaqiy (2/263) ameipokea pasi na kutaja Swahabah kwenye mlolongo wa wapokezi. Ibn Khuzaymah ameitaja Hadiyth chini ya kichwa cha khabari:

“Mlango unaozungumzia kuashiria kunakofahamika katika swalah hakuharibu swalah.”

Huu ni uelewa ambao unapingwa na Hanafiyyah. Kuna Hadiyth nyenginezo mfano wa hizo zilizopokelewa ikiwa ni pamoja vilevile na al-Bukhaariy na Muslim.

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Swifatu Swalaat-in-Nabiy, uk. 128-129
  • Imechapishwa: 04/08/2017