Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

1- Ubayd bin Ka´b (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Msitukane upepo. Mtapoona mnachokichukia basi semeni:

اللَّهُمَّ إنا نسألك خيرها وخيرَ مَا فِيها وخيرَ ما أُرْسِلَتْ بِهِ وَ نعُوذُ بِكَ مِنْ شَرِّها وَشر مَا فِيهَا وشَرَّ ما أُرسلت به

“Ee Allaah! Tunakuomba kheri za upepo huu, kheri ya yale yaliyomo ndani yake na kheri ya yale yaliyoamrishwa kuvileta. Na tunajilinda Kwako kutokamana na shari ya upepo huu, shari ya yaliyomo ndani yake na shari ya yale yaliyoamrishwa kuvileta.”[1]

Ameisahihisha at-Tirmidhiy.

MAELEZO

Pale ilipokuwa kutukana upepo na viumbe vyenginevyo ni upungufu katika imani na kuiponda Tawhiyd, ndipo mwandishi akataka kulizindua hilo ili muumini ajue kuwa maasi mengine yote yanaipunguza na kuidhoofisha Tawhiyd na imani. Imani inapanda na inashuka. Tawhiyd inapanda na inashuka. Kutukana upepo kunaipunguza imani kwa sababu upepo umeumbwa na ni wenye kuendeshwa. Unatumwa kwa kheri na shari. Hivyo hautakiwi kutukanwa. Badala yake muumini anatakiwa kutendea kazi yale aliyofundisha Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika Hadiyth:

1- Ubayd bin Ka´b (Radhiya Allaahu ´anh) amesimulia kwamba Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Msitukane upepo. Mtapoona mnachokichukia basi semeni:

اللَّهُمَّ إنا نسألك خيرها وخيرَ مَا فِيها وخيرَ ما أُرْسِلَتْ بِهِ وَ نعُوذُ بِكَ مِنْ شَرِّها وَشر مَا فِيهَا وشَرَّ ما أُرسلت به

“Ee Allaah! Tunakuomba kheri za upepo huu, kheri ya yale yaliyomo ndani yake na kheri ya yale yaliyoamrishwa kuvileta. Na tunajilinda Kwako kutokamana na shari ya upepo huu, shari ya yaliyomo ndani yake na shari ya yale yaliyoamrishwa kuvileta.”

al-Bukhaariy na Muslim wamepokea kutoka kwa ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) ambaye kasimulia kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akisema wakati wa upepo:

اللَّهُمَّ إِني أَسْأَلك خيرها وخيرَ مَا فِيها وخيرَ ما أُرْسِلَتْ بِهِ وَأَعُوذُ بِكَ مِنْ شَرِّها وَشر مَا فِيهَا وشَرَّ ما أُرسلت به

“Ee Allaah! Mimi nakuomba kheri za upepo huu, kheri ya yale yaliyomo ndani yake na kheri ya yale yaliyoamrishwa kuvileta. Na najilinda Kwako kutokamana na shari ya upepo huu, shari ya yaliyomo ndani yake na shari ya yale yaliyoamrishwa kuvileta.”[2]

Kuhusiana na haya kumekuja du´aa vilevile inayosema:

اللهم لا تجعلها ريحا، و اجعها رياحا، و اجعلها رحمة، و لا تجعلها عذابا

“Ee Allaah! Usiufanye upepo mmoja, zifanye pepo nyingi, na ufanye kuwa rehema na usiufanye kuwa adhabu.”[3]

Haya ndio yaliyowekwa katika Shari´ah kwa muumini kuyafanya wakati wa upepo. Amuombe Allaah pepo nyingi na sio upepo mmoja. Kwa sababu Allaah alituma upepo mmoja kwa ajili ya kuwaangamiza watu wa Huud na akatuma pepo nyingi kwa ajili ya bishara na rehema:

وَمِنْ آيَاتِهِ أَن يُرْسِلَ الرِّيَاحَ مُبَشِّرَاتٍ وَلِيُذِيقَكُم مِّن رَّحْمَتِهِ وَلِتَجْرِيَ الْفُلْكُ بِأَمْرِهِ وَلِتَبْتَغُوا مِن فَضْلِهِ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ

“Katika ishara Zake ni kwamba anapeleka pepo zenye bishara nzuri na ili akuonjesheni katika huruma Zake na ili vyende vyombo kwa amri Yake na ili watafute katika fadhila Zake na ili mpate kushukuru.” (ar-Ruum 30:46)

Ni miongoni mwa ukamilifu wa Tawhiyd na imani kutekeleza maamrisho ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na mtu asiutukane upepo wala kiumbe mwingine yeyote ambaye Allaah hakuweka katika Shari´ah watukanwe.

[1] at-Tirmidhiy (2252), Ahmad (21176) na al-Bukhaariy katika ”al-Adab al-Mufrad” (719). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”as-Silsilah as-Swahiyhah” (2756).

[2] al-Bukhaariy (4829) na Muslim (899).

[3] at-Twabaraaniy (11533) na Abu Ya´laa (2456). Dhaifu kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Dhwa´if-ul-Jaami´” (4461).

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Kitaab-it-Tawhiyd, uk. 161
  • Imechapishwa: 08/11/2018