57. Uwajibu wa mtu kuikagua nafsi yake juu ya sifa za Allaah

77- Ibn ´Abbaas (Radhiya Allaahu ´anhumaa) amesema:

“Ufanano wa vilivyoko Peponi juu ya vilivyoko duniani ni inapokuja katika majina pekee.”[1]

78- Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Peponi kuna ambavyo havijaonwa na macho, havijasikiwa na masikio wala havijapita kwenye moyo wa mtu.”[2]

Tumetambua kwamba ndani ya Pepo kuna matunda, mitende, makomamanga na vyenginevyo. Vitu hivi si kama vile vilivyoko duniani kwa njia yoyote ile. Ufanano uliopo baina yavyo ni katika majina pekee. Ufanano uliopo kati ya sifa za Muumba na sifa za viumbe ni katika majina ya sifa. Sifa zote ni za kihakika, sio Majaaz, japokuwa ni zenye kushirikiana katika majina.

Je, huoni kuwa neno (عين) linaweza kukusudiwa jicho la mwanadamu, chemchem na jasusi? Midhali neno limetajwa kwa njia ya kuegemezwa au maalum, basi unaondoka ushirikiano ambapo maneno yanakuwa na maana ya kihakika yanayofahamika udhahiri kwa yule msikilizaji. Hayo yanabainika kwa mfano pale unasema kwamba umeona chemchem ya maji (عين ماء) au chemchem inayobubujika (عين جارية). Amesema (Ta´ala):

فِيهَا عَيْنٌ جَارِيَةٌ

“Humo mna chemchem inayobubujika.”[3]

Vilevile mtiririko wa maneno unaweza kubainisha maana na kuondosha ushirikiano. Kwa mfano unaposema kwamba umeogelea ndani ya chemchem (عين) au umeona chemchem (عين) na samaki wengi. Vivyo hivyo kuhusiana na maneno mengine yote.

Hii ndio ´Aqiydah yetu. Zingatia kila pale ambapo sifa imethibitishwa ndani ya Qur-aan na Sunnah na ikague nafsi yako kwa uadilifu na inswafu.

Ninamuomba Allaah atuongoze sisi na nyinyi katika njia ilionyooka na atutunuku uongofu. Kila mmoja wetu anajua kwamba mwenye kuacha matamanio basi anajibidisha uongofu na haki. Tunamuomba Allaah atujaalie sisi na nyinyi miongoni mwa wale aliowatunuku kushikamana barabara na Sunnah. Hapana nguvu wala namna isipokuwa kwa msaada wa Allaah Mtukufu.

[1] Tazama ”az-Zuhd” (1/51/8) ya Hannaad na ”Tafsiyr al-Qur-aan al-´Adhwiym” (1/64) ya Ibn Kathiyr.

[2] al-Bukhaariy (8/515) na Muslim (4/2175).

[3] 88:12

  • Mhusika: Imaam Shams-ud-Diyn Muhammad bin Ahmad adh-Dhahabiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ithbaat-ul-Yad li-Laah Swifatan min Swifwaatih, uk. 46-47
  • Imechapishwa: 18/07/2019