56. Tawbah ya mwenye kutubia inakubaliwa

Imaam Ahmad bin Hanbal (Rahimahu Allaah) amesema:

“Yule mwenye kukutana na Allaah baada ya kufanya dhambi inayopelekea kuadhibiwa Motoni ilihali ametubia na sio mwenye kuendelea juu yake, Allaah anamsamehe. Anakubali tawbah kutoka kwa waja Wake na anayasamehe madhambi.”

MAELEZO

Allaah (Tabaarak wa Ta´ala) amesema:

قُلْ يَا عِبَادِيَ الَّذِينَ أَسْرَفُوا عَلَىٰ أَنفُسِهِمْ لَا تَقْنَطُوا مِن رَّحْمَةِ اللَّـهِ ۚ إِنَّ اللَّـهَ يَغْفِرُ الذُّنُوبَ جَمِيعًا ۚ إِنَّهُ هُوَ الْغَفُورُ الرَّحِيمُ

“Sema: Enyi waja Wangu ambao wamechupa mipaka juu ya nafsi zao: “Msikate tamaa na rehema ya Allaah, hakika Allaah anasamehe dhambi zote, hakika Yeye ndiye Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.”[1]

Allaah anaipenda tawbah, anawapenda wale wenye kutubia kwa wingi na wale wenye kujisafisha. Tunamtarajia yule mwenye kutubia, lakini hatumkatii Pepo wala Moto. Tunatarajia kwake. Imaam Ahmad (Rahimahu Allaah) amesema:

“Anakubali tawbah kutoka kwa waja Wake na anayasamehe madhambi.”

Kuna Aayah nyingi za Qur-aan na Hadiyth zinazoashiria kuwa Allaah anakubali tawbah ya wenye kutubia na anafurahika nayo.

[1] 39:53

  • Mhusika: ´Allaamah Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Usuwl-is-Sunnah, uk. 432
  • Imechapishwa: 10/12/2017