53. Maneno ya maimamu kuhusu ujuu wa Allaah

76 – Abu Bakr ´Abdullaah bin Muhammad ametukhabarisha: Abu Bakr Ahmad bin ´Aliy ametuhadithia: Hibatullaah bin al-Hasan ametuhadithia: Muhammad bin ´Ubaydillaah bin al-Hajjaaj ametuhadithia: Ahmad bin al-Hasan ametuhadithia: ´Abdullaah bin Ahmad ametuhadithia: Baba yangu ametuhadithia: Surayj bin an-Nu´maan ametuhadithia: ´Abdullaah bin Naafiy´ amenihadithia: Maalik amesema:

“Allaah yuko juu mbinguni na ujuzi Wake uko kila mahali – hakuna kinachomfichika.”[1]

77- Abu ´Umar amesema:

“Wanachuoni wa Maswahabah na Taabi´uun ambao tafsiri ya Qur-aan imepokelewa kutoka kwao wamesema walipokuwa wakifasiri maneno ya Allaah (´Azza wa Jall):

مَا يَكُونُ مِن نَّجْوَىٰ ثَلَاثَةٍ إِلَّا هُوَ رَابِعُهُمْ وَلَا خَمْسَةٍ إِلَّا هُوَ سَادِسُهُمْ وَلَا أَدْنَىٰ مِن ذَٰلِكَ وَلَا أَكْثَرَ إِلَّا هُوَ مَعَهُمْ أَيْنَ مَا كَانُوا

“Hauwi mnong’ono wa watatu isipokuwa Yeye ni wa nne wao, na wala watano isipokuwa Yeye ni wa sita wao, na wala chini kuliko ya hivyo na wala wengi zaidi isipokuwa Yeye yupamoja nao popote watakapokuwa, kisha siku ya Qiyaamah atawajulisha yale waliyoyatenda; hakika Allaah juu ya kila jambo ni mjuzi.”[2]

wakasema: ”Yuko juu ya ´Arshi na ujuzi Wake uko kila mahali.” Hakuna yeyote ambaye maneno yake yanazingatiwa ambaye alitofautiana nao.”[3]

78- Imepokelewa kwa cheni ya wapokezi wake kutoka kwa Ma´daan ambaye amesema:

“Nilimuuliza Sufyaan ath-Thawriy kuhusiana na maneno Yake (Ta´ala):

وَهُوَ مَعَكُمْ أَيْنَ مَا كُنتُمْ

”Naye yupamoja nanyi popote mlipo.”[4]

Akajibu:

“Bi maana ujuzi Wake.”[5]

79- Hanbal amesema:

“Nilisema kumwambia Abu ´Abdillaah nini maana ya:

وَهُوَ مَعَكُمْ أَيْنَ مَا كُنتُمْ

”Naye yupamoja nanyi popote mlipo.”

na:

مَا يَكُونُ مِن نَّجْوَىٰ ثَلَاثَةٍ إِلَّا هُوَ رَابِعُهُمْ وَلَا خَمْسَةٍ إِلَّا هُوَ سَادِسُهُمْ وَلَا أَدْنَىٰ مِن ذَٰلِكَ وَلَا أَكْثَرَ إِلَّا هُوَ مَعَهُمْ أَيْنَ مَا كَانُوا

“Hauwi mnong’ono wa watatu isipokuwa Yeye ni wa nne wao, na wala watano isipokuwa Yeye ni wa sita wao, na wala chini kuliko ya hivyo na wala wengi zaidi isipokuwa Yeye yupamoja nao popote watakapokuwa, kisha siku ya Qiyaamah atawajulisha yale waliyoyatenda; hakika Allaah juu ya kila jambo ni mjuzi.”

Akajibu:

”Bi maana ujuzi Wake. Anayajua ya wazi na yaliyofichikana. Ujuzi Wake umekizunguka kila kitu. Ni mjuzi wa yaliyofichikana. Mola wetu yuko juu ya ´Arshi, pasi na kikomo wala kumfikiria.”

80- Imepokelewa kutoka kwa Yuusuf bin Muusaa al-Baghdaadiy ya kwamba amesema:

“Kulisemwa kuambiwa Abu ´Abdillaah Ahmad bin Hanbal: “Ni kweli kwamba Allaah (´Azza wa Jall) yuko juu ya mbingu ya saba juu ya ´Arshi Yake, ametengana na viumbe Wake na uwezo na ujuzi Wake uko kila mahali?” Akajibu:

“Ndio. Juu ya ´Arshi na ujuzi Wake uko kila mahali – haufichikani na kitu.”

81- Nimefikiwa na khabari kwamba Abu Haniyfah (Rahimahu Allaah) amesema katika “al-Fiqh al-Akbar”:

“Mwenye kupinga kwamba Allaah (Ta´ala) yuko juu ya mbingu amekufuru.”

82 – ´Abdullaah bin Muhammad ametukhabarisha: Ahmad bin ´Aliy ametuhadithia: Hibatullaah ametuhadithia: Ahmad bin Muhammad bin Hafsw ametuhadithia: Muhammad bin Ahmad ametuhadithia: al-Hasan bin Yuusuf ametuhadithia: Ahmad bin ´Aliy bin Zayd ametuhadithia: Muhammad bin Abiy ´Amr ametuhadithia: ´Amr bin Wahb ametuhadithia: Nimemsikia Shaddaad bin Hakiym akisema kwamba Muhammad bin al-Hasan [ash-Shaybaaniy] akisema kuhusiana na Hadiyth:

“Allaah hushuka katika mbingu ya dunia.”

“Mfano wa Hadiyth kama hizi zimepokelewa na waaminifu. Sisi tunazipokea, tunaziamini na wala hatuzifasiri.”[6]

83 – Imaam Abul-Hasan ´Aliy bin ´Asaakir al-Batwaa-ihiy al-Muqriy’ ametukhabarisha: al-Amiyn Abu Twaalib ´Abdul-Qaadir bin Muhammad bin ´Abdil-Qaadir al-Yuusufiy ametuhadithia: Abu Ishaaq Ibraahiym bin ´Umar al-Barmakiy ametuhadithia: Abu Bakr Muhammad bin ´Abdillaah bin Bakhiyt ametuhadithia: Abu Hafsw ´Umar bin Muhammad bin ´Iysaa al-Jawhariy ametuhadithia: Abu Bakr Ahmad bin Muhammad bin Haaniy’ at-Twaa-iy al-Athram ametuhadithia: ´Aliy bin al-Hasan bin Shaqiyq amenihadithia:

“Nilisemwa kumwambia Ibn-ul-Mubaarak: “Ni vipi tutamjua Mola wetu?” Akasema: “Juu ya mbingu ya saba juu ya ´Arshi Yake. Hatusemi kama wanavosema Jahmiyyah, kwamba yuko hapa na hapa.”[7]

84 – Abu Bakr al-Athram amesema: Muhammad bin Ibraahiym al-Qaysiy amenihadithia:

“Kulisemwa kuambiwa Ahmad bin Hanbal: “Inasemekana kwamba Ibn-ul-Mubaarak aliulizwa ni vipi tutamjua Mola wetu ambapo akajibu: “Juu ya mbingu ya saba juu ya ´Arshi Yake.” Ahmad akasema: “Hayo ndio maoni yetu.”[8]

85 – al-Athram amesema: Abu ´Abdillaah al-Qaysiy ametuhadithia: Nimemsikia Wahb bin Jariyr akisema:

“Wanachokusudia Jahmiyyah kusema ni kwamba hakuna kitu juu ya mbingu.”

86- Amesema:

“Nilisema kumwambia Sulaymaan bin Harb: ”Hammaad bin Zayd alikuwa akisema nini kuhusu Jahmiyyah?” Akasema: ”Alikuwa akisema:

“Wanachokusudia kusema ni kwamba hakuna kitu juu ya mbingu.”

87 – ´Abdullaah ametukhabarisha: Ahmad ametuhadithia: Hibatullaah ametuhadithia: Muhammad bin al-Husayn bin Ya´quub ametuhadithia: Da´laj bin ametuhadithia: Ahmad bin ´Aliy al-Abaar ametuhadithia: Muhammad bin Mansuur at-Twuusiy ametuhadithia: Nuuh bin Maymuun ametuhadithia: Bukayr bin Ma´ruuf ametuhadithia, kutoka kwa Muqaatil bin Hayyaan ambaye amesema kuhusiana na maneno Yake (Ta´ala):

مَا يَكُونُ مِن نَّجْوَىٰ ثَلَاثَةٍ إِلَّا هُوَ رَابِعُهُمْ وَلَا خَمْسَةٍ إِلَّا هُوَ سَادِسُهُمْ وَلَا أَدْنَىٰ مِن ذَٰلِكَ وَلَا أَكْثَرَ إِلَّا هُوَ مَعَهُمْ أَيْنَ مَا كَانُوا

“Hauwi mnong’ono wa watatu isipokuwa Yeye ni wa nne wao, na wala watano isipokuwa Yeye ni wa sita wao, na wala chini kuliko ya hivyo na wala wengi zaidi isipokuwa Yeye yupamoja nao popote watakapokuwa, kisha siku ya Qiyaamah atawajulisha yale waliyoyatenda; hakika Allaah juu ya kila jambo ni mjuzi.”

“Yuko juu ya ´Arshi na hakuna kitu kinachofichikana na ujuzi Wake.”

88- Ja´far bin ´Abdillaah ameeleza:

“Kuna mtu alikuja kwa Maalik bin Anas akasema: “Ee Abu ´Abdillaah:

الرَّحْمَـٰنُ عَلَى الْعَرْشِ اسْتَوَىٰ

“Mwingi wa rehema amelingana juu ya ‘Arshi.”[9]

Amelingana vipi?” Sijapatapo kumuona Maalik akichukulia vibaya jambo kama alivoyachukulia maneno haya. Akaanza kutokwa na jasho na huku watu wanasubiri wasikie nini atasema. Halafu akasema: “Namna haijulikani. Kulingana si jambo lisilofahamika. Kuamini hilo ni wajibu na kuuliza kuhusu hilo ni Bid´ah. Mimi nachelea kuwa wewe ni mpotevu.” Akaamrisha akatolewa nje.”[10]

89 – Hibatullaah ametuhadithia: Muhammad bin Ja´far ametuhadithia: Abu ´Abdillaah Naftwuuyah ametuhadithia: Abu Sulaymaan Daawuud bin ´Aliy amenihadithia: ”Tulikuwa kwa Ibn-ul-A´raabiy pindi mtu mmoja alipokuja na kusema: ”Nini maana ya maneno Yake (Ta´ala):

الرَّحْمَـٰنُ عَلَى الْعَرْشِ اسْتَوَىٰ

“Mwingi wa rehema amelingana juu ya ‘Arshi.”

Akajibu: “Yuko juu ya ´Arshi Yake kama Yeye alivoeleza (´Azza wa Jall).”Akasema: “Ee Abu ´Abdillaah! Hii sio maana yake. Maana yake ni kwamba ametawala (استولى).” Akasema: “Kimya. Hakusemwi kuwa kuna mtu amekitawala kitu isipokuwa kunakuwa kupinzana. Anaposhinda mmoja wao ndio kunasemwa kwamba ametawala. Hujamsikia an-Naabighah akisema:

Ambaye ni mfano wako au wewe ukamtangulia

farasi mwenye mbio zaidi ndiye atatawala (استولى) juu ya goli

90 – Mwana wangu Abul-Majd ´Iysaa bin ´Abdillaah amenihadithia: Shaykh Abu Twaahir al-Mubaarak bin Abiyl-Ma´aaliy bin al-Ma´twuushiy ametuhadithia: Abul-Ghanaa-im Muhammad bin Muhammad bin al-Muhtadiy ametuhadithia: Shaykh Abu Ishaaq Ibraahiym bin ´Umayr al-Barmakiy ametuhadithia: Abul-Fadhwl ´Ubaydullaah bin ´Abdir-Rahmaan az-Zuhriy ametuhadithia: Hamzah bin al-Husayn bin ´Umar al-Bazzaaz amenihadithia: ´Abdullaah bin Muhammad bin ´Ubayd amenihadithia: ´Abbaas bin Dhaqaan amenihadithia kwamba alisema:

“Nilisema kumwambia Bishr al-Haafiy: “Nataka tukae mimi na wewe tu.” Akasema: “Ukitaka.” Siku moja mapema nikamuona anaingia kwenye kuba. Akaswali Rakaa´ nne kwa njia ambayo sikuweza kuswali kama yeye. Nikamsikia akisema katika Sujuud: “Ee Allaah! Hakika Wewe unajua juu ya ´Arshi Yako kwamba mimi napenda zaidi udhalilifu kuliko utukufu. Ee Allaah! Hakika Wewe unajua juu ya ´Arshi Yako kwamba ufukara ni wenye kupendeza zaidi kwangu kuliko utajiri. Ee Allaah! Hakika Wewe unajua juu ya ´Arshi Yako kwamba sitangulizi chochote juu ya kukupenda.” Nilipomsikia akisema hivo nikaanza kulia ambapo akasema: “Unajua kwamba nisingesema hivo endapo ningejua kama uko hapa.”

91 – Shaykh Abu ´Aliy al-Hasan bin Salaamah bin Muhammad al-Harraaniy ametukhabarisha: Abu Ishaaq Ibraahiym bin Muhammad bin Nabhaan al-Ghanawiy ar-Raqqiy´ ametuhadithia: Shaykh-ul-Islaam Abul-Hasan ´Aliy bin Ahmad bin Yuusuf al-Qurashiy al-Hakaariy ametukhabarisha: Ahmad bin ´Aaswim al-Mawsuliy ametukhabarisha: Abul-Qaasim ´Aliy bin al-Qaasim al-Muqriy ametuhadithia Mosul: Niliandika kutoka kwenye kitabu cha Ibn Hishaam al-Baladiy:

بسم الله الرحمن الرحيم

Haya ndio anayousia Muhammad bin Idriys ash-Shaafi´iy… ح

Shaykh-ul-Islaam amesema: Abu Mansuur Muhammad bin ´Aliy bin Muhammad bin al-Hasan bin Sahl bin Khaliyfah ametukhabarisha: Babu yangu Muhammad bin al-Hasan bin Sahl bin Khaliyfah ametuhadithia: Abu ´Aliy al-Husayn bin Hishaam bin ´Umar al-Baladiy ametuhadithia: Huu ni wasia wa Muhammad bin Idriys ash-Shaafi´iy (Radhiya Allaahu ´anh):

“Nausia mtu ashuhudie ya kwamba hapana mungu wa haki isipokuwa Allaah na kwamba Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni mja na Mtume Wake, amuamini Allaah, Malaika Wake, Vitabu Vyake na Mitume Wake. Hatumtofautishi yeyote kati ya Mitume Wake. Swalah yangu na ´ibaadah zengine zote, kuishi kwangu na kufa kwangu ni kwa ajili ya Allaah, Mola wa walimwengu, hali ya kuwa hana mshirika; hayo ndio tumeamrishwa. Allaah atawafufua wale waliyomo ndani ya makaburi. Pepo ni haki. Moto ni haki. Adhabu ya kaburi, hesabu, mizani na njia ni haki. Allaah atawalipa waja kwa matendo yao. Kwa hayo ndio naishi, kwa hayo ndio nakufa na kwa hayo ndio nitafufuliwa – Allaah akitaka.

Nashuhudia ya kwamba imani ni maneno, matendo na kutambua kwa moyo. Inazidi na inapungua.

Qur-aan ni maneno ya Allaah (Ta´ala) na hayakuumbwa.

Allaah (´Azza wa Jall) ataonekana Aakhirah. Waumini watamuona kwa macho yao, waziwazi, na watayasikia maneno Yake.

Yuko juu ya ´Arshi.

Qadar, kheri na shari yake, ni yenye kutoka kwa Allaah (´Azza wa Jall). Hakukuwi isipokuwa kile Allaah (´Azza wa Jall) alichopanga na kukadiria kiwepo.

Watu bora baada ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni Abu Bakr, ´Umar, ´Uthmaan na ´Aliy bin Abiy Twaalib (Radhiya Allaahu ´anhum). Nawapenda na kuwaombea msamaha wale walioshiriki katika vita vya Swiffiyn, waliopigana na waliouawa na Maswahabah wengine wote wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Watawala wanatakiwa kusikizwa na kutiiwa midhali wanaswali. Haitakiwi kuwaasi watawala. Ukhaliyfah ni kwa Quraysh.

Kile kiwango kidogo kinacholewesha basi kingi chake pia ni pombe.

Mu´tah ni haramu.

Nausia kumcha Allaah (´Azza wa Jall), kufuata Sunnah, mapokezi kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na Maswahabah wake na Bid´ah na matamanio vinatakiwa kuachwa na kuepukwa. Mche Allaah ukweli wa kumcha. Wala msife isipokuwa nyinyi ni waislamu. Huo ndio wasia wa wale wa mwanzo na wa mwisho. Yule anayemcha Allaah basi Allaah humfungulia njia na humruzuku kwa namna asiyoitarajia. Mcheni Allaah kadiri na mnavoweza. Jilazimieni na swalah ya ijumaa na swalah ya mkusanyiko, itekelezeni Sunnah na kuamini na kuwa na ufahamu katika dini. Yule katika nyinyi ambaye atahudhuria wakati wa kukata kwangu roho basi anitamkishe niseme ya kwamba hapana mwabudiwa wa haki isipokuwua Allaah, hali ya kuwa pekee hana mshirika, na nashuhudia ya kwamba Muhammad ni mja na Mtume wake. Nitengenezeni kucha na masharubu kabla ya kufa. Kama atakuwa amehudhuria mwanamke mwenye hedhi, basi asimame.”[11]

92 – Shaykh-ul-Islaam amesema: Abu Ya´laa al-Khaliyl bin ´Abdillaah al-Haafidhw ametukhabarisha: Abul-Qaasim bin ´Alqamah al-Abhariy ametuhadithia: Abu ´Abdir-Rahmaan bin Abiy Haatim ar-Raaziy ametuhadithia, kutoka kwa Abu Shu´ayb na Abu Thawr, kutoka kwa Abu ´Abdillaah Muhammad bin Idriys ash-Shaafi´iy (Radhiya Allaahu ´anh) aliyesema:

“´Aqiydah ambayo mimi nafuata na ambayo nimeona wenzetu, Ahl-ul-Hadiyth kama mfano wa Sufyaan na Maalik, wanafuata ni kukubali ya kwamba hapana mungu wa haki isipokuwua Allaah na kwamba Muhammad ni mja na Mtume wake… na kwamba Allaah yuko juu ya ´Arshi Yake juu ya mbingu Zake. Anawakurubia viumbe Wake vile anavotaka na kwamba Allaah hushuka katika mbingu ya dunia vile anavotaka… “[12]

93 – Kwa cheni hii ´Abdur-Rahmaan bin Abiy Haatim amesema: Yuunus bin ´Abdil-A´laa ametuhadithia: Nimemsikia Abu ´Abdillaah Muhammad bin Idriys ash-Shaafi´iy (Radhiya Allaahu ´anh) akisema wakati alipoulizwa kuhusu sifa za Allaah na kile anachoamini:

“Allaah (Ta´ala) ana majina na sifa ambazo zimetajwa katika Kitabu Chake na zimeelezwa na ambazo Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amewaeleza Ummah wake. Hakuna yeyote katika viumbe wa Allaah (Ta´ala) ambaye atafikiwa nazo ana haki ya kuzirudisha. Kwa sababu Qur-aan ndio imeteremka nazo na zimesihi kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kupitia wapokezi waaminifu. Atakayepingana na hayo baada ya kusimamikiwa na hoja basi huyo ni kafiri. Kabla ya hapo ni mwenye kupewa udhuru kwa sababu hayo hayatambuliki kwa kutumia akili, kuonekana wala kufikiria. Hatumkufurishi yeyote kwa sababu ya ujinga wa kutoyajua isipokuwa baada ya kusimamikiwa na hoja. Tunazithibitisha sifa hizi na tunazikanushia ufanano kama ambavo Yeye mwenyewe amejikanushia pale aliposema:

لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ ۖوَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ

“Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.”

Ukhaliyfah wa Abu Bakr ulikuwa wa sawa. Allaah aliuhukumu mbinguni Kwake na akazikusanya nyoyo za Maswahabah wa Mtume Wake (Swala Allaahu ´alayhi wa sallam) juu yake.”

94 – Abul-Fath Muhammad bin ´Abdil-Baaqiy´ bin Ahmad bin Sulaymaan ametukhabarisha: Abu Bakr Ahmad bin ´Aliy bin al-Husayn bin Zakariyyaa at-Twuuraythiythiy ametuhadithia: Abul-Qaasim Hibatullaah bin al-Hasan ametuhadithia: Muhammad bin al-Mudhwaffar al-Muqriy’ ametuhadithia: Abu Muhammad ´Abdur-Rahmaan bin Abiy Haatim ametuhadithia … ح

Nilimsomea Abul-Fadhwl ´Abdullaah bin Ahmad bin Muhammad bin ´Abdil-Qaahir at-Twuusiy huko Mosul: Abul-Hasan ´Aliy bin Muhammad bin ´Aliy bin Muhammad bin al-´Allaaf amekukhabarisheni: Abul-Qaasim bin Bishraan ametuhadithia: Abul-Hasan ´Aliy bin ´Abdil-´Aziyz ametuhadithia: Abu Muhammad ´Abdur-Rahmaan bin Abiy Haatim ametuhadithia:

“Nilimuuliza baba yangu na Abu Zu´rah kuhusu ´Aqiydah ya Ahl-us-Sunnah wal-Jamaa´ah na yale waliyokuta wanachuoni wakiamini katika misingi ya dini, yale waliyowakuta wanachuoni wote ulimwenguni na yale ambayo wawili hao wanaamini kuhusu hilo. Wakasema:

“Tuliwakuta wanachuoni wa ulimwenguni kote Hijaaz, Shaam na Yemen na ´Aqiydah yao ilikuwa:

1- Imani ni maneno na vitendo, inapanda na inashuka.

2- Qur-aan ni maneno ya Allaah ambayo haikuumbwa kwa njia zake zote.

3- Qadar, kheri na shari yake, ni yenye kutoka kwa Allaah (´Azza wa Jall).

4- Watu bora wa Ummah huu baada ya Mtume wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ni Abu Bakr as-Swiddiyq, ´Umar bin al-Khattwaab, ´Uthmaan bin ´Affaan na ´Aliy bin Abiy Twaalib (Radhiya Allaahu ´anhum). Hawa ndio makhaliyfah waongofu.

5- Wale kumi ambao Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliwataja na akawashuhudia Pepo ni haki.

6- Allaah (´Azza wa Jall) yuko juu ya ´Arshi Yake, ametengana na viumbe Wake. Hivo ndivo alivojieleza Yeye mwenyewe kupitia Kitabu Chake na kupitia Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hayafanyiwi namna. Ujuzi Wake umekizunguka kila kitu:

لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ ۖوَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ

“Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.”[13]

95- Abul-Qaasim at-Twabariy amesema:

“Nimesoma kwenye vitabu vya Abu Haatim Muhammad bin Idriys bin al-Mundhiriy al-Handhwaliy kutoka kwa ambaye alisikia kutoka kwake: Madhehebu yetu na chaguo letu ni kumfuata Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), Maswahabah wake na wale waliokuja baada yao waliowafuata, kushikamana barabara na madhehebu ya Ahl-ul-Athar, akiwemo Abu ´Abdillaah Ahmad bin Hanbal, Ishaaq bin Raahuuyah, Abu ´Ubayd al-Qaasim bin Sallaam na ash-Shaafi´iy, na kushikamana na Qur-aan na Sunnah. Tunaamini kwamba Allaah yuko juu ya ´Arshi Yake na ametengana na viumbe Wake:

لَيْسَ كَمِثْلِهِ شَيْءٌ ۖوَهُوَ السَّمِيعُ الْبَصِيرُ

“Hakuna chochote kinachofanana Naye – Naye ni Mwenye kusikia, Mwenye kuona.”

96 – Abul-Mutwahhar al-Qaasim bin al-Fadhwl bin ´Abdil-Waahid as-Saydaliy ametuhadithia: Ahmad bin ´Aliy bin Khalaf ametuhadithia: al-Haakim Abu ´Abdillaah ametuhadithia: Nimemsikia Muhammad bin Swaalih bin Haaniy’ akisema: Nimemsikia Abu Bakr Muhammad bin Ishaaq bin Khuzaymah amesema:

“Yule asiyekubali kwamba Allaah (´Azza wa Jall) yuko juu ya ´Arshi Yake na amelingana juu ya mbingu Zake saba basi huyo ni kafiri. Anatakiwa kuambiwa kutubia. Akitubia ni sawa. Vinginevyo ikatwe shingo yake. Baada ya hapo kiwiliwili chake kitupwe kwenye jalalani ili waislamu na wale makafiri walio na mkataba wa amani na waislamu wasije kuudhika kutokana na harufu ya mzoga wake. Mali yake inakuwa fai. Hakuna muislamu yeyote atayefaa kumrithi kwa sababu muislamu hamrithi kafiri. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Muislamu hamrithi kafiri wala kafiri hamrithi muislamu.”[14]

97- Abu ´Umar bin ´Abdil-Barr amesema:

“Mtume wa Allaah  (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mola wetu (Tabaarak wa Ta´ala) hushuka katika mbingu ya chini ya dunia pale kunapobaki theluthi ya mwisho ya usiku na anasema: “Nani anayeniomba Nimpe? Ni nani anayeniuliza Nimpe? Ni nani anayenitaka msamaha Nimsamehe? Ni nani anayetaka nimsamehe Nimghufurie?”[15]

Hadiyth hii imethibiti na cheni ya wapokezi wake ni Swahiyh. Ahl-ul-Hadiyth hawatofautiani juu ya kusihi kwake. Imesimuliwa kupitia njia nyingi. Wapokezi waaminifu wameipokea kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Katika Hadiyth hii kuna dalili vilevile inayoonyesha kwamba Allaah (´Azza wa Jall) yuko juu ya mbingu, juu ya ´Arshi na juu ya mbingu saba, kama walivosema Mkusanyiko. Ni dalili yao dhidi ya Mu´tazilah na Jahmiyyah ambao wanasema kuwa Allaah (´Azza wa Jall) yuko kila mahali na hayuko juu ya ´Arshi. Dalili inayoonyesha kwamba Ahl-ul-Haqq ndio wamepatia ni maneno ya Allaah (´Azza wa Jall):

الرَّحْمَـٰنُ عَلَى الْعَرْشِ اسْتَوَىٰ

“Mwingi wa rehema amelingana juu ya ‘Arshi.”[16]

إِلَيْهِ يَصْعَدُ الْكَلِمُ الطَّيِّبُ وَالْعَمَلُ الصَّالِحُ يَرْفَعُهُ

”Kwake pekee linapanda neno zuri na tendo jema analitukuza.”[17]

يَخَافُونَ رَبَّهُم مِّن فَوْقِهِمْ وَيَفْعَلُونَ مَا يُؤْمَرُونَ

”Wanamkhofu Mola wao Aliye juu yao na wanafanya yale wanayoamrishwa.”[18]

98- Abu ´Umar bin ´Abdil-Barr amesema:

“Ahl-us-Sunnah ni wenye kukubaliana na kuamini zile sifa zote zilizothibiti katika Qur-aan na Sunnah na kuzichukulia kama ni za kweli na si Majaaz. Hata hivyo hawaifanyii namna sifa yoyote na wala kuitilia kikomo sifa maalum.

Kuhusu Ahl-ul-Bid´ah kama vile Jahmiyyah, Mu´tazilah na Khawaarij, ni kwamba wanazipinga na hawachukulii hata moja kwamba ni ya ukweli. Wanadai kwamba yule mwenye kuzithibitisha ni Mushabbih. Upande mwingine wanaonelea kuwa yule mwenye kuzithibitisha amemkana mwabudiwa. Haki iko pamoja na wale wanaonukuu yale yanayosemwa na Kitabu cha Allaah na Mtume Wake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hawa ndio maimamu wa mkusanyiko.”[19]

99- Katika sehemu ya mwisho ambako kuna Hadiyth za Ja´far bin Muhammad bin Nusayr al-Khuldiy nimekuta kisa kilichoandikwa kwa hati ya mkono ya mwandishi wa sehemu hiyo akisema:

“Nimesoma kwenye juzu ya mwisho na nimeona vilevile hati ya mkono ya Abu Bakr bin Shaadhaan. Mwanangu al-Hasan amesikia kisa hiki na akasema kwamba alimsikia mtu mwaminifu akisema: “Tulikuwa tukimwosha maiti naye alikuwa kwenye kitanda chake. Tulipomfunua nguo yake tukamsikia akisema: “Yuko juu ya ´Arshi pekee. Yuko juu ya ´Arshi pekee.”Tukaingiwa na woga sana kutokana na yale tuliyosikia na tukakimbia kutoka pale. Kisha tukarudi na kumuosha.”

[1] al-Laalakaa’iy (2/401), ´Abdullaah bin Ahmad katika ”as-Sunnah” (1/107) na al-Aajurriy katika ”ash-Shariy´ah”, uk. 289.

[2] 58:07

[3] at-Tamhiyd (7/138-139).

[4] 57:04

[5] at-Tamhiyd (7/142) na al-Laalakaa’iy (2/401).

[6] al-Laalakaa’iy (2/433).

[7] ´Abdullaah bin Ahmad katika ”as-Sunnah” (1/111), al-Bukhaariy katika ”Khalq Af´aal-il-´Ibaad”, uk. 8, na ad-Daarimiy katika ”ar-Radd ´alaal-Jahmiyyah”, uk. 9. Swahiyh kwa mujibu wa al-Bayhaqiy katika ”al-Asmaa’ was-Swifaat”, uk. 538.

[8] Twabaqaat-ul-Hanaabilah (1/267).

[9] 20:05

[10] al-Laalakaa’iy (2/398) na al-Asmaa’ was-Swifaat, uk. 516, ya al-Bayhaqiy.

[11] adh-Dhahabiy amesema:

”Wasia wa ash-Shaafi´iy uliopokelewa kutoka kwa al-Husayn bin Hishaam al-Baladiy si sahihi.” (Siyar A´laam-in-Nubalaa’ (10/79))

[12] adh-Dhahabiy amesema:

”Cheni ya wapokezi ni dhaifu.” (al-´Uluww, uk. 120)

[13] 42:11

[14] al-Bukhaariy (6764) na Muslim (1614).

[15] al-Bukhaariy (7494) na Muslim (758).

[16] 20:05

[17] 35:10

[18] 16:50 at-Tamhiyd (7/128-129).

[19] at-Tamhiyd (7/128).

  • Mhusika: Imaam Muwaffaq-ud-Diyn bin Qudaamah al-Maqdisiy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Ithbaatu Swifat-il-´Uluww, uk. 166-190
  • Imechapishwa: 05/07/2018