52. Fadhilah za Maswahabah kumi waliobashiriwa Pepo

Imaam Ibn Abiy Daawuud (Rahimahu Allaah) amesema:

وإنَّهم للرَّهطُ لا ريبَ فيهمُ

17 – Hakika ni kikundi kisichokuwa na shaka yoyote juu yao

على نُجبِ الفردوسِ بالنُّور تَسرحُ

     kwamba watakuwa juu ya vipandwa vya Firdaws vikiwazungusha watakapo

سعيدٌ وسعدٌ وابن عوفٍ وطلحةُ

18 – Sa´iyd, Sa´d, Ibn ´Awf na Twalhah

وعامرُ فهرٍ والزبيرُ الممدَّح

     ´Aamir Fihr na az-Zubayd wenye kusifiwa

MAELEZO

Kikundi kinachokusudiwa hapa ni watu wasiopungua kumi. Wanaokusudiwa hapa ni wale kumi walioahidiwa Pepo[1].

Mtunzi (Rahimahu Allaah) amesema:

“… kwamba watakuwa juu ya vipandwa vya Firdaws… ”

Bi maana juu ya vipandwa vya Peponi vikiwazungusha watakapo.

Pindi alipowataja makhaliyfah wanne (Radhiya Allaahu ´anhum) hapa ndipo akawataja wale kumi walioahidiwa Pepo. Wamebaki sita miongoni mwa wale kumi:

1 – Sa´iyd. Anaitwa Sa´iyd bin Zayd bin ´Amr bin Nufayl. Ni mtoto wa ami yake ´Umar bin al-Khattwaab. Alikuwa ni mume wa dada yake na ´Umar (Radhiya Allaahu ´anhum).

2 – Sa´d. Anaitwa Sa´d bin Abiy Waqqaas az-Zuhriy (Radhiya Allaahu ´anh).

3 – Ibn ´Awf. Anaitwa ´Abdur-Rahmaan bin ´Awf (Radhiya Allaahu ´anh). Alikuwa ni katika Maswahabah matajiri na miongoni mwa wale ambao wanajitolea sana katika njia ya Allaah (´Azza wa Jall).

4 – Twalhah. Anaitwa Twalhah bin ´Ubaydillaah (Radhiya Allaahu ´anh).

5 – ´Aamir. Anaitwa Abu ´Ubaydah ´Aamir bin Jarraah (Radhiya Allaahu ´anh). Yeye ndiye mwaminifu wa Ummah huu.

Fihr alikuwa ni katika babu zake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na katika baba wa ma-Quraysh.

6 – az-Zubayr. Anaitwa az-Zubayr bin ´Awwaam (Radhiya Allaahu ´anh). Alikuwa ni msaidizi wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

Hawa sita, pamoja na wale makhaliyfah wanne, wanakuwa kumi waliobashiriwa Pepo. Wao ndio Maswahabah bora. Wote wanatokamana na kabila la Quraysh.

[1] Abu Daawuud (4650) na (4649), at-Tirmidhiy (3757) na (3748), an-Nasaa´iy (1630), Ibn Maajah (134), Ahmad (01/187-188) na wengineo.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh al-Mandhuumat-ul-Haaiyyah fiy ´Aqiydati Ahl-is-Sunnah wal-Jamaa´ah, uk. 122-123
  • Imechapishwa: 10/01/2024