1- Jaahiliyyah: Ni ile hali waliokuwa nayo waarabu kabla ya Uislamu katika kumjahili Allaah na Mtume Wake, nembo za dini, majigambo ya koo, kiburi, jeuri na mengineyo[1]. Ni unasibisho wa ujinga ambao ni kutokuwa na elimu au kutoifuata elimu hiyo. Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah amesema:

“Ambaye haijui elimu ni mjinga mwenye ujinga mdogo. Akionelea kinyume chake basi huyo ni mjinga mwenye ujinga uliopandiana. Akisema kinyume na haki hali ya kuwa ni mwenye kuijua hiyo haki au si mwenye kuijua, huyo ni mjinga pia. Yakishabainika hayo basi watu kabla ya kutumilizwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) walikuwa katika Jaahiliyyah unasibisho wa ujinga. Maneno na matendo waliokuwa juu yake walizuliwa nayo na mjinga na ni yenye kufanywa na mjinga. Vivyo hivyo kila kinachokwenda kinyume na yale waliyokuja nayo Mitume katika uyahudi na unaswara ni Jaahiliyyah. Hiyo ilikuwa ni Jaahiliyyah yenye kuenea. Ama baada ya kutumwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) unaweza kuwa sehemu moja pasi na sehemu nyengine, kama ilivyo katika nchi za makafiri. Vilevile unaweza kuwa kwa mtu mmoja pasi na mtu mwengine, kama mtu ambaye bado hajasilimu yuko katika Jaahiliyyah ijapokuwa anaishi katika nchi ya Kiislamu. Ama katika zama kwa njia ya moja kwa moja hakuna Jaahiliyyah baada ya kutumilizwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Hakutoacha kuwepo kikundi chenye kushinda juu ya haki mpaka kisimame Qiyaamah. Lakini Jaahiliyyah iliyofungamana inaweza kupatikana katika baadhi ya miji ya waislamu na kwa waislamu wengi. Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Mambo mane katika Ummah wangu ni katika Jaahiliyyah… “[2]

Alisema kumwambia Abu Dharr:

“Hakika wewe una chembechembe za Jaahiliyyah.”[3]

na mfano wa hayo.”[4]

Ufupisho wa hayo ni kwamba Jaahiliyyah ni unasibisho wa ujinga ambako ni kutokuwa na elimu na kwamba umegawanyika mafungu mawili:

1- Ujinga ulioenea. Hayo ni yale yaliyokuweko kabla ya kutumilizwa Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na umekwisha kwa kutumilizwa kwake.

2- Jaahiliyyah maalum kwa baadhi ya nchi, kwa baadhi ya miji na kwa baadhi ya watu. Jaahiliyyah aina hii bado ni yenye kuendelea. Kwa haya linabainika kosa la wale wenye kueneza Jaahiliyyah hii leo na wanasema:

“Jaahiliyyah ya zama hizi au Jaahiliyyah ya karne ya ishirini.”

au mfano wa maneno hayo. Usawa ni kusema Jaahiliyyah kwa baadhi ya watu wa karne hii au wengi wa watu wa karne hii. Ama kuieneza ni jambo lisilosihi na wala lisilojuzu. Kwa sababu Jaahiliyyah yenye kuenea imekwisha kwa kutumilizwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam).

[1] an-Nihaayah (01/323) ya Ibn Athiyr.

[2] Muslim (2157).

[3] al-Bukhaariy (30) na Muslim (4289).

[4] Iqtidhwaa´-us-Swiraatw al-Mustaqiym (01/225-227) uhakiki wa Dr. Naaswir al-´Aqil.

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ´Aqiydat-ut-Tawhiyd, uk. 95-96
  • Imechapishwa: 18/03/2020