Suufiyyah ilipoanza, hapakuwepo kitu chochote maalum kinachowatofautisha Suufiyyah, bali jambo lilikuwa limefupika juu ya kupetuka mpaka katika kuipa nyongo dunia, kulazimiana na Dhikr na khofu kubwa wakati wa kumdhukuru Allaah, jambo ambalo lilikuwa linaweza kupelekea mpaka mtu akapoteza fahamu au mtu akafa kabisa wakati wa kusikia Aayah iliyotaja matishio ya adhabu. Mfano wa hilo linaweza kuonekana katika kisa cha mkuu wa al-Baswrah Zuraarah bin Awf, ambaye alisoma katika Swalah ya al-Fajr:

فَإِذَا نُقِرَ فِي النَّاقُورِ

“Itakapopulizwa katika baragumu kwa sauti kali.” (al-Muddaththir 74:08)

akaanguka chini na kufa papo hapo. Vilevile kisa cha Abu Jahr ambaye alikuwa kipofu. Alianguka chini na kufa wakati Swaalih al-Murriy alipomsomea. Kuna Wengine walegeuka kuwa mabubu wakati waliposikia Qur-aan inasomwa. Shaykh-ul-Islaam Ibn Taymiyyah aliliwekea hili taaliki na kusema

“Hapakuwepo katika Maswahabah ambao wana hali kama hii. Wakati jambo hilo lilipojitokeza basi kundi katika Maswahabah na Taabi´uun, kama Asmaa´ bint Abiy Bakr, ´Abdullaah bin az-Zubayr na Muhammad bin Siyriyn walilikemea kwa sababu waliona kitendo hicho kuwa ni Bid´ah na kinachoenda kinyume na uongofu wa Maswahabah.”[1]

Ibn-ul-Jawziy amesema katika “Talbiys Ibliys:

“Madhehebu ya Suufiyyah ni njia ambayo mwanzoni wake ilikuwa inahusiana na kuipa nyongo dunia. Kisha wale ambao wanajinasibisha nayo wakaanza kujishughulisha na nyimbo na kucheza. Hivyo wale ambao wanatafuta Aakhirah katika watu wajinga wakajiunga nao kwa sababu ya upaji nyongo dunia uliokuwa ukionekana kutoka kwao na wakajiunga nao wale ambao wanatafuta dunia kwa sababu ya ile raha na michezo iliokuwa ikionekana kwao.”[2]

Abu Zahrah amesema katika kubainisha sababu ya kudhihiri madhehebu ya Suufiyyah na machimbuko yake:

“Chimbuko la kwanza: Baadhi ya wafanya ´ibaadah wa Kiislamu walielekeza juhudi zao zote katika kuipa nyongo dunia na kujishughulisha na ´ibaadah. Hili lilianza mara ya kwanza wakati wa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam), wakati kulikuwa baadhi ya Maswahabah ambao walilazimiana na kusimama usiku mzima kuswali pasi na kulala. Wengine wakaamua kufunga kila siku, wakati wengine wakaamua kutooa wanawake. Wakati khabari zao zilipomfikia Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) akasema:

“Wana nini watu ambao wanasema kadhaa na kadhaa? Lakini mimi mara nafunga na mara nakula, naswali na nalala na naoa wanawake. Anayezipa mgongo Sunnah zangu si katika mimi.”[3]

Isitoshe Qur-aan imekataza uzushi wa utawa. Allaah Amesema:

وَرَهْبَانِيَّةً ابْتَدَعُوهَا مَا كَتَبْنَاهَا عَلَيْهِمْ إِلَّا ابْتِغَاءَ رِضْوَانِ اللَّـهِ فَمَا رَعَوْهَا حَقَّ رِعَايَتِهَا

“Utawa waliouanzisha wao wenyewe. Hatukuwaandikia hayo juu yao isipokuwa tu kutafuta radhi za Allaah. Lakini hawakuuchunga ipasavyo kuchungwa.” (al-Hadiyd 57:27)

Lakini baada ya Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwenda kwa marafiki walioko juu na watu wengi kutoka katika dini zilizotangulia wakaingia ndani ya Uislamu ndipo idadi ya watu wenye kuipa kisogo dunia na neema zake kwa kupindukia ikazidi. Hivyo Suufiyyah wakawa wamepata nafasi katika nyoyo za watu hao kwa sababu imepata ardhi yenye rutuba.

Chimbuko la pili kama nyoyo za watu waliovutikiwa, ilikuwa ni kitu ambacho kilijitokeza baina ya Waislamu katika fikira mbili. Fikira ya kwanza ilikuwa ni ya kifalsafa wakati nyingine asli yake ilikuwa kutoka katika zile dini za kale. Ama kuhusiana na fikira ya kwanza, ilikuwa ni madhehebu ya rai ya taaluma za falsafa kwamba elimu na maarifa inatoka moyoni kwa msaada wa mazoezi ya kiroho na kuipa malezi nafsi. Fikira ya pili, ilikuwa na maana ya kuamini kwamba Allaah amekita katika kila kitu (al-Huluul) na kwamba kila kitu ni Allaah (Wahdat-ul-Wujuud). Madhehebu haya yalianza kupata kidato kati ya mapote ambayo mwanzoni yalikuwa yakijinasibisha na Uislamu kwa uongo wakati Waislamu walipoanza kuchanganyikana na wakristo. Madhehebu haya yalikuwa kati ya Swabaaiyyah na Kaysaaniyyah, kisha kati ya Qaraamitwah, kisha kati ya Baatwiniyyah na hatimaye ikapata sura kati ya baadhi ya Suufiyyuun…

Kuna chanzo kingine ambapo wamechukua na ambapo wamesababisha mwelekeo wa alama ya ki-Suufiy, nayo ni kwamba maandiko ya Qur-aan na Sunnah yana maana ya kiinje na ya kindani… Bila ya shaka inadhihiri kwamba Suufiyyah wamechukua madhehebu haya kutoka kwa Baatwiniyyah.”[4]

Fikira zote hizi zimechanganyika; kuanzia kwenye kupetuka mipaka katika kuipa nyongo dunia, kwenda katika madhehebu ambayo yana maana ya kwamba Allaah Yuko katika kila kitu na kwamba viumbe vyote ni kitu na ndio Allaah. Matokeo ya fikira hizi zilizochanganyika ndipo ikajitokeza Suufiyyah katika Uislamu. Baada ya karne ya nne na ya tano wakashika kasi. Wakafikisha kilele chao na wakawa mbali kabisa na uongofu wa Qur-aan tukufu na Sunnah zilizotwahirika ambapo mtu anaweza kufikia. Ilifikisha daraja ambayo, wafuasi wa Suufiyyah wakawa wanawaita wale wanaofuata Qur-aan na Sunanh “Watu wa Shari´ah” na “Watu wanaofuata ya dhahiri”, na wakawa wanajiita wao wenyewe kuwa ni “Watu wa uhakika” na “Watu wanaofuata yenye kujificha”.

[1] Majmuu´-ul-Fataawaa (06/11).

[2] Talbiys Ibliys, uk. 161.

[3] al-Bukhaariy na Muslim.

[4] Kutoka katika kitabu “Ibn Taymiyyah”, uk. 197-198, cha Abu Zahrah.

  • Mhusika: Shaykh Muhammad bin Rabiy´ bin Haadiy al-Madkhaliy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Haqiyqat-us-Suufiyyah
  • Imechapishwa: 23/12/2019