47. Mume na mke kuishi kwa uzuri

39- Uwajibu wa wanandoa kuyafanya vizuri matangamano yao ya ndoa

Ni wajibu kwa mume kutangamana naye kwa uzuri na kumfurahisha kwa yale Allaah aliyomhalalishia – na si kwa yale aliyoharamisha – na khaswa ikiwa kama bado ni mdogo. Kuna Hadiyth zifuatazo juu ya hilo:

1- Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mbora wenu ni yule mbora kwa wake zake na mimi ni mbora kwa wake zangu.”

2-  Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika Khutbah yake ya hajj ya kuaga:

“Tanabahini! Nawausia kuwatendea wanawake kheri. Kwani wao ni wasaidizi wenu na hammiliki juu yao chocote isipokuwa hicho isipokuwa watapofanya uchafu wa wazi[1]. Wakifanya hivo, basi wahameni katika malazi na wapigeni kipigo kisichoumiza. Wakikutiini, basi msitafute njia ya kuwaadhibu bure. Tanabahini! Hakika nyinyi mna haki juu ya wake zenu na wake zenu wana haki juu yenu. Ama haki zenu juu ya wake zenu wasimruhusu mtu msiyempenda kukalia zulia lenu na wala wasimruhusu kuingia nyumbani mwenu yule msiyempenda. Tanabahini! Haki zao juu yenu ni kuwafanyia vizuri katika mavazi yao na katika chakula chao.”[2]

3- Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Muumini mwanamume asimchukie muumini mwanamke. Iwapo atachukia tabia fulani kutoka kwake, basi ataridhishwa na nyingine.”[3]

4- Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Muumini aliye na imani kamilifu ni yule mwenye tabia njema. Mbora wao ni yule ambaye ni mbora kwa wakeze.”[4]

5- ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesimulia: “Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliniita na huku wahabeshi wanacheza mchezo wa kutumia mishale msikitini kaitka siku ya ´Iyd ambapo akanambia: “Ewe chekundu![5] Je, unataka kuwatazama?” Nikajibu: “Ndio.” Kisha akanisimamisha nyuma yake na akayateremsha mabega yake ili nipate kuwatazama. Hivyo nikaweka kidevu changu mabegani mwake na uso wangu ukawa karibu na shavu lake. Nikawatazama kupitia mabegani mwake.” Katika upokezi mwingine imekuja: “… [kichwa changu kikiwa] baina ya sikio lake na mabega yake na huku akisema: “Ee ´Aaishah! Hujatosheka?” Nasema: “Hapana, ili nione cheo changu kwake” mpaka nilipotosheka. Miongoni mwa waliokuwa wakisema ni: “Abul-Qaasim ni mzuri.” Katika upokezi mwingine: “ Hali iliendelea hivo mpaka nilipochoshwa akasema: “Umetosheka sasa?” Nikajibu: “Ndio.” Akasema: “Nenda!” Katika upokezi mwingine imekuja: “Nikasema: “Usiniharakize.” Hivyo akaendelea kunisimamia mpaka aliponiuliza kwa mara nyingine: “Umetosheka?” Nikamwambia: “Usiniharakize.” Nikamuona akibadilisha miguu yake kwa ajili ya kuchoka. Sikuwa ni mwenye kupenda kuwatazama, lakini nilichotaka ni khabari ziwafikie wanawake nafasi alionayo (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) kwangu na nafasi nilionayo kwake ilihali bado nilikuwa msichana mdogo ili wathamini hali ya msichana mdogo mwarabu ambaye anapenda burudani na mchezo. ´Umar akatokeza ambapo watu mpaka watoto wakatawanyika. Akasema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam): “Nimewaona mashaytwaan wa kibinaadamu na wa kijini wakimkimbia ´Umar.” Siku hiyo alisema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam): “Kwa hiyo watambue mayahudi kwamba katika dini yetu kuna nafasi.”[6]

6- ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesimulia tena: “Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alirudi kutoka katika vita vya Tabuuk au vya Khaybar. Chumbani kwake kulikuwa pazia. Upepo ukapeperusha ncha ya pazia iliokuwa imefunika watoto wa sanamu aliokuwa akichezea ´Aaishah. Akasema: “Nini hii, ´Aaishah?” Akasema: “Ni watoto wangu wa kike.” Kati yao aliona farasi mwenye mbawa mbili aliyetengenezwa kwa kitambaa. Akasema: “Ni nini hiki ninachoona katikati yao?” Akajibu: “Ni farasi.” Akasema: “Ni nini hivyo vilivyo juu yake?” Akasema: “Ni mbawa mbili.” Akasema: “Farasi mwenye mbawa mbili?” Akajibu: “Je, wewe hukusikia kuwa Sulaymaan alikuwa na farasi aliye na mbawa?” ´Aaishah anaendelea kusimulia: “Basi akacheka (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) mpaka nikaona magego yake.”[7]

7- ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesimulia tena kwamba alikuwa pamoja na Mtume wa Allaah  (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) katika moja ya safari zake wakati bado alikuwa msichana mdogo. Nilikuwa bado sijakuwa mnene wala sijakuwa na mwili. Akawaambia Maswahabah wake: “Tangulieni mbele!” Kisha akasema: “Njoo nishindane na wewe mbio” ambapo nikamshinda mbio za mguu. Baada ya muda nikatoka naye katika safari nyingine ambapo akawaambia Maswahabah wake: “Tangulieni mbele!” Kisha akanambia: “Njoo nishindane na wewe mbio.” Nilisahau yaliyopita na wakati huo nilikuwa nimeshakuwa na mwili na nimeshanenepa. Nikamwambia: “Vipi nitashindane nawe, ee Mtume wa Allaah, na mimi niko katika hali hii?” Akasema: “Utashindana nami.” Nikashindane naye ambapo akanishinda mbio. Akaanza kucheka na kusema: “Hii ni kulipiza ushindi wako wa mwanzo.”[8]

8- ´Aaishah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesimulia akisema: “Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) alikuwa akiletewa chombo cha maziwa ambapo naanza kunywa mimi ilihali niko na hedhi kisha akiipokea yeye na kuweka midomo yake pale nilipokuwa nimeweka mimi. Wakati mwingine nilikuwa nikichukua kipande cha nyama na kukila kisha anakichukua yeye na kuweka midomo yake pale nilipoweka mimi.”[9]

9- Jaabir bin ´Abdillaah na Jaabir bin ´Umar (Radhiya Allaahu ´anhum) wamesimulia kwamba Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema: “Kila kitu kisichokuwa ndani yake na kumtaja Allaah ni upuuzi na usahaulifu isipokuwa vitu vyenye sifa nne; mtu kucheza na mke wake, mtu kumfunza farasi wake, kutembea baina ya lengo lililokusudiwa na mtu kujifunza kuogelea.”[10]

[1] Kila sifa mbaya basi ni ucafu katika maneno na vitendo.” Tazama “an-Nihaayah”.

Kwa ajili hiyo as-Sindiy amesema katika maelezo yake yake ya chini (Haashiyah):

“Makusudio ni uasi, kumuudhi mume na familia yake kwa mdomo au kwa mwili. Haihusiani na uzinzi kwa sababu [uzinzi] hauendi sambamba na kipigo kisichoumiza. Haya ndio yaliyotajwa katika maneno Yake (Ta´ala):

وَاللَّاتِي تَخَافُونَ نُشُوزَهُنَّ فَعِظُوهُنَّ وَاهْجُرُوهُنَّ فِي الْمَضَاجِعِ وَاضْرِبُوهُنَّ ۖ فَإِنْ أَطَعْنَكُمْ فَلَا تَبْغُوا عَلَيْهِنَّ سَبِيلًا ۗ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلِيًّا كَبِيرًا

“Wale ambao mnakhofu uasi kutoka kwao, basi wanasihini na wahameni katika malazi na wapigeni. Wakikutiini, basi msitafute njia dhidi yao. Hakika Allaah yujuu,  Mkubwa kabisa.” (04:34)

Hadiyth ina maana hii. Makusudio ya kipigo ni cha wastani na si cha sana.”

[2] Ameipokea at-Tirmidhiy (02/204) na akasema:

“Hadiyth ni nzuri Swahiyh”,

Ibn Hibbaan, (01/568-569) kupitia katika Hadiyth ya ´Amr bin al-Ahwasw (Radhiya Allaahu ´anh). Ni Swahiyh kwa mujibu wa Ibn-ul-Qayyim katika “az-Zaad” (04/64).

[3] Ameipokea Muslim (04/178) na (179) na wengineo kupitia Hadiyth ya Abu Hurayrah.

[4] Ameipokea at-Tirmidhiy (02/204), Ahmad (250) na (472), Abul-Hasan at-Twuusiy katika “al-Mukhtasar” yake (01/218) ambaye ameonelea kuwa ni nzuri. at-Tirmidhiy amesema:

“Hadiyth ni nzuri Swahiyh.”

Mlolongo wa wapokezi wake ni mzuri kutoka kwa Abu Hurayrah. Kipande chake cha katikati ni Swahiyh kimekuja kupitia njia Swahiyh kutoka kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Nimekipokea katika “Silsilat-ul-Ahaadiyth as-Swahiyhah” (284).

[5] Ziada hii imepokelewa na an-Nasaa´iy katika “´Ishrat-un-Nisaa´” (01/75). al-Haafidhw amesema katika “al-Fath” (02/355):

“Mlolongo wa wapokezi wake ni Swahiyh. Sijaona Hadiyth yoyote Swahiyh iliyotaja neno “chekundu” isipokuwa Hadiyth hii.”

Hapo utapata kutambua kwamba maneno yaliyosema Ibn-ul-Qayyim katika “al-Manaar”, uk. 34:

“Kila Hadiyth ambayo ndani yake kuna “chekundu” au kumetajwa “chekundu” ni uongo na dhaifu.”

Haya si kweli moja kwa moja. Hivyo usidanganyike nayo. Halafu nikamuona az-Zamakshariy akisema katika “al-Mu´tabar” (19/20):

“Mwalimu wetu Ibn Kathiyr ambaye naye amepokea kutoka kwa mwalimu wake Abul-Hajjaaj al-Miziy ya kwamba amesema:

“Kila Hadiyth iliyotaja “chekundu” ni batili isipokuwa Hadiyth kuhusu swawm iliyoko katika Sunan an-Nasaa´iy.”

Hadiyth nyingine inapatikana katika “an-Nasaa´iy”:

“Wahabeshi waliingia msikitini na huku wakicheza mchezo wa kutumia mishale ambapo akanambia: “Ewe chekundu![5] Je, unataka kuwatazama?” Mlolongo wa wapokezi wake ni Swahiyh.

[6] Ameipokea al-Bukhaariy, Muslim, an-Nasaa´iy, Ahmad na wengineo.

[7] Ameipokea Abu Daawuud katika “Sunan” yake (02/305), an-Nasaa´iy katika “´Ishrat-un-Nisaa´” (01/75) kwa mlolongo wa wapokezi mzuri na Ibn ´Uday (01/182 kwa kifupi.

[8] Ameipokea al-Humaydiy katika “al-Musnad” yake (261), Abu Daawuud (01/403), an-Nasaa´iy katika “´Ishrat-un-Nisaa´” (02/74) na siyaaq ni yake, Ahmad (06/264), at-Twabaraaniy (47/23), Ibn Maajah (01/610) kwa kifupi na mlolongo wa wapokezi wake ni Swahiyh alivosema al-´Iraaqiy katika “Takhriyj al-Ihyaa´” (02/40). Nami nimeipokea Hadiyth hiyo katika “Irwaa´-ul-Ghaliyl” na nimetaja njia zake na baadhi ya matamshi yake. Arejee huko yule anayetaka (1497).

[9] Ameipokea Muslim (01/168-169), Ahmad (06/62) na wengineo.

[10] Ameipokea an-Nasaa´iy katika “´Ishrat-un-Nisaa´” (02/74), at-Twabaraaniy katika “al-Mu´jam al-Kabiyr” (02/89/01), Abu Nu´aym katika “Ahaadiyth Abil-Qaasim al-Aswam” (17-18) kwa mlolongo wa wapokezi Swahiyh. al-Mundhiriy na al-Bayhaqiy wameipa nguvu. Nimezungumza kwa upambanuzi katika “Silsilat-ul-Ahaadiyth as-Swahiyhah” (309).

  • Mhusika: Imaam Muhammad Naaswir-ud-Diyn al-Albaaniy
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Aadaab-uz-Zafaaf, uk. 223-278
  • Imechapishwa: 02/05/2018