47. Haikusuniwa kuweka majani au mti juu ya kaburi

Swali: Baada ya kumzika maiti wako watu wanaosoma kutoka ndani ya msahafu Suurah “Yaa Siyn” kwenye kaburi na wanaweka mmea juu ya kaburi kama kakti na juu ya kaburi hupanda shayiri au ngano kwa hoja kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) aliiweka kwenye makaburi mawili ya Maswahabah zake. Ni ipi hukumu ya hilo?

Jibu: Haikuwekwa katika Shari´ah kusoma Suurah “Yaa Siyn” wala nyengineyo kutoka ndani ya Qur-aan juu ya kaburi baada ya kuzika wala wakati wa mchakato wa kuzika. Wala haikuwekwa katika Shari´ah kusoma makaburini. Kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakufanya hivo wala makhaliyfah zake waongofu. Kama ambavo haikuwekwa Shari´ah ya kuadhini wala kukimu katika kaburi. Bali yote hayo ni Bid´ah. Imesihi kutoka kwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ya kwamba amesema:

“Yeyote atakayefanya kitendo kisichoafikiana na amri yetu atarudishiwa mwenyewe.”[1]

Ameipokea Muslim katika “as-Swahiyh” yake.

Vivyo hivyo haikuwekwa katika Shari´ah kupanda miti juu ya makaburi; si kakti, shayiri, ngano wala isiyokuwa hiyo. Kwa sababu Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) hakufanya hivo juu ya makaburi wala makhaliyah zake waongofu (Radhiya Allaahu ´anhum).

Kuhusu yale aliyofanya juu ya makaburi mawili ambayo Allaah alimjuza kuwa yanaadhibiwa ambapo akapanda kuti ni kitu maalum kwake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) na kwa hayo makaburi mawili peke yake. Kwani hakufanya hivo kwa wengine wasiokuwa hao wawili. Isitoshe haifai kwa waislamu kuzusha kitu katika mambo ya kujikurubisha kwa Allaah ambacho hakikuwekwa na Allaah katika Shari´ah kutokana na Hadiyth iliyotajwa. Aidha Allaah (Subhaanah) amesema:

أَمْ لَهُمْ شُرَكَاءُ شَرَعُوا لَهُم مِّنَ الدِّينِ مَا لَمْ يَأْذَن بِهِ اللَّـهُ

“Je, wanao washirika waliowaamuru dini yale ambayo Allaah hakuyatolea kwayo idhini?”[2]

[1] Muslim (1718).

[2] 42:21

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: at-Tahdhiyr min Fitnat-il-Qubuur, uk. 141-142
  • Imechapishwa: 26/07/2022