3- Kufuru ndogo isiyomtoa mtu nje ya Uislamu. Hiyo ni ile kufuru ya kimatendo ambayo imethibiti kuitwa ´kufuru` katika Qur-aan na Sunnah, lakini hata hivyo haijafikia katika kiwango cha kufuru kubwa. Kwa mfano kukufuru neema kulikotajwa katika maneno Yake (Ta´ala):

وَضَرَبَ اللَّـهُ مَثَلًا قَرْيَةً كَانَتْ آمِنَةً مُّطْمَئِنَّةً يَأْتِيهَا رِزْقُهَا رَغَدًا مِّن كُلِّ مَكَانٍ فَكَفَرَتْ بِأَنْعُمِ اللَّـهِ

“Allaah amepiga mfano wa mji uliokuwa katika amani na utulivu, inaifikia riziki yake maridhawa kutoka kila mahali, kisha ukakufuru neema za Allaah.”[1]

Mfano mwingine ni kumuua muislamu kulikotajwa katika maneno yake (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Kumtukana muislamu ni ufuska na kumuua ni ukafiri.”[2]

Vilevile amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Msirudi baada yangu kuwa makafiri baadhi wakipiga shingo za wengine.”[3]

 Mfano mwingine ni kuapa kwa asiyekuwa Allaah. Amesema (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mwenye kuapa kwa asiyekuwa Allaah amekufuru au amefanya shirki.”[4]

Hata hivo Allaah amemfanya mwenye kufanya dhambi kubwa kuwa muumini. Amesema (Ta´ala):

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا كُتِبَ عَلَيْكُمُ الْقِصَاصُ فِي الْقَتْلَى

”Enyi walioamini! Mmeandikiwa Shari´ah ya kisasi kwa waliouawa.”

Hakumtoa muuaji miongoni mwa wale walioamini na akamfanya kuwa ndugu ya wale walipiza kisasi. Amesema:

فَمَنْ عُفِيَ لَهُ مِنْ أَخِيهِ شَيْءٌ فَاتِّبَاعٌ بِالْمَعْرُوفِ وَأَدَاءٌ إِلَيْهِ بِإِحْسَانٍ

“Anayesamehewa na nduguye kwa lolote basi kufuatilizwa kwake kuwe kwa wema na kumlipa kwake iwe kwa ihsaan.”[5]

Kinachokusudiwa pasi na shaka ni udugu wa kidini. Amesema (Ta´ala):

وَإِن طَائِفَتَانِ مِنَ الْمُؤْمِنِينَ اقْتَتَلُوا فَأَصْلِحُوا بَيْنَهُمَا ۖ فَإِن بَغَتْ إِحْدَاهُمَا عَلَى الْأُخْرَىٰ فَقَاتِلُوا الَّتِي تَبْغِي حَتَّىٰ تَفِيءَ إِلَىٰ أَمْرِ اللَّـهِ ۚ فَإِن فَاءَتْ فَأَصْلِحُوا بَيْنَهُمَا

“Ikiwa makundi mawili ya waumini yakipigana, basi suluhisheni baina yao. Lakini moja wapo likikandamiza jengine, basi piganeni na ambalo linakandamiza mpaka lielemee kwenye amri ya Allaah. Likishaelemea, basi suluhisheni kati yao.”[6]

إِنَّمَا الْمُؤْمِنُونَ إِخْوَةٌ فَأَصْلِحُوا بَيْنَ أَخَوَيْكُمْ

“Hakika waumini ni ndugu, hivyo basi suluhisheni baina ya ndugu zenu.”[7]

Tofauti kwa ufupi kati ya kufuru kubwa na kufuru ndogo:

1- Kufuru kubwa inamtoa mtu nje ya Uislamu na inayaharibu matendo. Kufuru ndogo haimtoi mtu nje ya Uislamu na wala haiharibu matendo. Lakini inaipunguza kwa kiasi chake na inamtia mwenye nayo khatarini.

2- Kufuru kubwa inamdumisha mwenye nayo Motoni na kufuru ndogo, mwenye nayo akiingia Motoni, hatodumishwa humo milele. Kuna uwezekano Allaah akamsamehe mwenye nayo na asiingie Motoni.

3- Kufuru kubwa inahalalisha damu na mali na kufuru ndogo haihalalishi damu na mali.

4- Kufuru kubwa inawajibisha uhasama wa kikweli kati yake yeye na waumini. Haijuzu kwa waumini kumpenda na kumfanya akawa rafiki ijapokuwa ni miongoni mwa ndugu wa karibu kabisa. Kuhusu kufuru ndogo haizuii mapenzi moja kwa moja. Bali mwenye nayo anapendwa na anachukiwa kwa kiasi cha ile imani alionayo na anachukiwa na kufanywa adui kwa kiasi cha maasi alionayo.

[1] 16:112

[2] al-Bukaariy (147) na Muslim (218).

[3] al-Bukhaariy (121) na Muslim (220).

[4] Sharh-ut-Twahaawiyyah, uk. 361 Maktat-ul-Islaamiy.

[5] 02:178

[6] 49:09

[7] 49:10

  • Mhusika: Imaam Swaalih bin Fawzaan al-Fawzaan
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: ´Aqiydat-ut-Tawhiyd, uk. 87-89
  • Imechapishwa: 17/03/2020