Shaykh-ul-Islaam Muhammad bin ´Abdil-Wahhaab (Rahimahu Allaah) amesema:

Allaah ametuma Mitume wote wakiwa ni wenye kutoa bishara njema na kuonya. Dalili ni Kauli Yake (Ta´ala):

رُّسُلًا مُّبَشِّرِينَ وَمُنذِرِينَ لِئَلَّا يَكُونَ لِلنَّاسِ عَلَى اللَّـهِ حُجَّةٌ بَعْدَ الرُّسُلِ ۚ وَكَانَ اللَّـهُ عَزِيزًا حَكِيمًا

“Mitume wenye kutoa bishara njema na waonyaji ili pasikuweko kutoka kwa watu hoja yoyote juu ya Allaah baada ya kuletwa ya Mitume. Hakika Allaah ni Mwenye nguvu kabisa, Mwenye hekima.” (an-Nisaa´ 04:165)

Wa mwanzo wao alikuwa ni Nuuh (´alayhis-Salaam) na wa mwisho wao alikuwa ni Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Dalili juu ya kwamba wa mwanzo wao alikuwa ni Nuuh (´alayhis-Salaam) ni Kauli Yake (Ta´ala):

إِنَّا أَوْحَيْنَا إِلَيْكَ كَمَا أَوْحَيْنَا إِلَىٰ نُوحٍ وَالنَّبِيِّينَ مِن بَعْدِهِ

”Hakika Tumekuletea Wahy kama tulivyomletea Nuuh na Manabii baada yake.” (an-Nisaa´ 04:163)

MAELEZO

Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ametumwa kwa walimwengu wote; majini na watu. Amesema (Ta´ala):

قُلْ يَا أَيُّهَا النَّاسُ إِنِّي رَسُولُ اللَّـهِ إِلَيْكُمْ جَمِيعًا

“Sema: “Hakika mimi ni Mtume wa Allaah kwenu nyinyi nyote.””
(
07:158)

وَمَا أَرْسَلْنَاكَ إِلَّا كَافَّةً لِّلنَّاسِ بَشِيرًا وَنَذِيرًا وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ

“Hatukukutuma isipokuwa kwa watu wote uwe mbashiriaji na muonyaji, lakini watu wengi hawajui.” (34:28)

Yeye (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ndiye Mtume wa mwisho. Hakuna baada yake Mtume mwingine.

Kadhalika Mitume wengine waliosalia walitumwa kwa nyumati zao wakiwa ni wenye kutoa bishara njema na wenye kuonya. Mtume wa kwanza alikuwa ni Nuuh ambaye alitumwa baada ya watu wake kuanza kuabudu masanamu.

Kabla yake Aadam ndiye alikuwa Mtume mwenye kukalifishwa. Allaah alimtuma kwa dhuriya yake ili waweze kumuabudu Allaah kwa Shari´ah aliyokuja nayo baba yao (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam). Dhuriya hiyo waliendelea kuwa waislamu na wenye kuongoka mpaka kulipotokea shirki kwa watu wa Nuuh. Hapo ndipo Allaah aliwatumia Nuuh (´alayhis-Salaam). Yeye ndiye alikuwa Mtume wa kwanza kutumilizwa kwa watu wa ardhini baada ya kujitokeza kwa shirki.

Kila Ummah Allaah aliutumia Mtume. ´Aad walitumiwa Huud. Thamuud walitumiwa Swaalih. Halafu akamtuma Ibraahiym, Luutw na Shu´ayb, wakifuatana. Kisha akatuma Mitume wengine, mmoja baada ya mwingine, akiwemo Muusa, Haaruun, ´Iysaa, Ayyuub, Daawuud na Sulaymaan. Utume ukahitimishwa na Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ambaye ndiye wa mwisho na mbora wao. Allaah (Jalla wa ´Alaa) amesema:

رُّسُلًا مُّبَشِّرِينَ وَمُنذِرِينَ لِئَلَّا يَكُونَ لِلنَّاسِ عَلَى اللَّـهِ حُجَّةٌ بَعْدَ الرُّسُلِ

“Mitume wenye kutoa bishara njema na waonyaji ili pasikuweko kutoka kwa watu hoja yoyote juu ya Allaah baada ya kuletwa ya Mitume.”
(
04:165)

Kusema kuwa ni wenye kutoa bishara njema kunamaanishwa kwamba walikuwa wakiwaahidi wale wenye kuwatii Pepo. Kusema kwamba ni wenye kutoa maonyo kunamaanishwa kwamba wanaonya kumshirikisha na Moto na adhabu yenye kuumiza kwa wale wenye kwenda kinyume na amri ya Allaah.

Allaah amemtuma Muhammad (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) vilevile akiwa ni mwenye kutoa bishara njema na mwenye kuonya. Amesema (Ta´ala):

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ إِنَّا أَرْسَلْنَاكَ شَاهِدًا وَمُبَشِّرًا وَنَذِيرًا وَدَاعِيًا إِلَى اللَّـهِ بِإِذْنِهِ وَسِرَاجًا مُّنِيرًا

“Ee Nabii! Hakika Sisi tumekutuma uwe shahidi na mbashiriaji na mwonyaji na mlinganiaji kwa Allaah kwa idhini Yake na taa lenye kuangaza.” (33:45-46)

مَّا كَانَ مُحَمَّدٌ أَبَا أَحَدٍ مِّن رِّجَالِكُمْ وَلَـٰكِن رَّسُولَ اللَّـهِ وَخَاتَمَ النَّبِيِّينَ ۗ وَكَانَ اللَّـهُ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمًا

“Hakuwa Muhammad baba wa yeyote miongoni mwa wanaume wenu, lakini ni Mtume wa Allaah na ni mwisho wa Manabii. Allaah ni mjuzi wa kila kitu.” (33:40)

Ni wajibu kwa kila Ummah kumfuata Mtume wake na kujisalimisha na ule uongofu waliofikisha. Allaah amemuahidi yule mwenye kufanya hivo furaha duniani na Aakhirah. Hata hivyo viumbe wengi wamewaasi na kwenda kinyume na yale waliyokuja nayo Mitume wao. Amesema (Ta´ala):

وَمَا أَكْثَرُ النَّاسِ وَلَوْ حَرَصْتَ بِمُؤْمِنِينَ

“Wengi wa watu hawatoamini japokuwa utatilia hima.” (12:103)

وَإِن تُطِعْ أَكْثَرَ مَن فِي الْأَرْضِ يُضِلُّوكَ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ

“Kama ukiwatii wengi walioko ulimwenguni, watakupoteza na njia ya Allaah.” (06:116)

وَقَلِيلٌ مِّنْ عِبَادِيَ الشَّكُورُ

“Na wachache miongoni mwa waja Wangu wenye kushukuru.” (34:13)

وَلَقَدْ صَدَّقَ عَلَيْهِمْ إِبْلِيسُ ظَنَّهُ فَاتَّبَعُوهُ إِلَّا فَرِيقًا مِّنَ الْمُؤْمِنِينَ

“Hakika Ibliys alisadikisha dhana yake juu yao. Wakamfuata [wote] – isipokuwa kundi katika waumini wa kweli.” (34:20)

Kila Mtume alikuwa akiuta Ummah wake katika kumpwekesha Allaah, kumtii na kujiepusha na shirki na kumuasi. Amesema (Ta´ala):

وَلَقَدْ بَعَثْنَا فِي كُلِّ أُمَّةٍ رَّسُولًا أَنِ اعْبُدُوا اللَّـهَ وَاجْتَنِبُوا الطَّاغُوتَ

“Hakika Tulituma katika kila ummah Mtume [awaamrishe watu wake] kwamba: “Mwabuduni Allaah na jiepusheni na Twaaghuut.”” (16:36)

Bi maana mtiini, mpwekesheni, shikamaneni na dini Yake na muepukeni Twaaghuut.

  • Mhusika: Imaam ´Abdul-´Aziyz bin ´Abdillaah bin Baaz
  • Mfasiri: Firqatunnajia.com
  • Marejeo: Sharh Thalaathat-il-Usuwl, uk. 56-58
  • Imechapishwa: 12/02/2017